Habari

Walimu watishia kuondoka SHA changamoto zikizidi

Na MERCY SIMIYU, LYNET IGWADAH February 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WALIMU kote nchini wanakumbwa na changamoto kubwa za kupata huduma za afya chini ya Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA), huku vyama vya walimu vikionya kuwa vinaweza kuwataka wasusie mpango huo endapo matatizo hayo hayatashughulikiwa kwa dharura.

Vyama hivyo vinasema vimepokea malalamishi mengi kutoka maeneo mbalimbali ambapo walimu wamenyimwa matibabu katika hospitali kubwa kutokana na ucheleweshaji, taratibu zisizoeleweka na ukosefu wa idhini kwa wakati chini ya mfumo wa SHA.

Mwenyekiti wa kitaifa wa Chama cha Walimu wa Sekondari na Vyuo (Kuppet), Bw Omboko Milemba, aliambia Taifa Jumapili kuwa mkataba wa matibabu wa walimu chini ya SHA umefikia wakati wa kupitiwa upya ili malalamishi kuzingatiwa.

Bw Milemba alisema Kuppet ilikubaliana na taasisi husika kuwa utekelezaji wa mpango huo ungechukuliwa kama majaribio, kisha mapitio yafanywe baada ya miezi mitatu kipindi ambacho alisema sasa kimekamilika.

“Baada ya majaribio ya miezi miwili, tulikubaliana kufanya mapitio baada ya miezi mitatu. Kwa mtazamo wetu, miezi hiyo imeisha na tunataka mapitio hayo yafanyike ili changamoto zinazojitokeza zishughulikiwe,” alisema.

Aliongeza kuwa walimu wanakabiliwa na matatizo mengi chini ya mpango huo mpya.

Maafisa wa chama walitaja visa ambapo walimu waliopata ajali walinyimwa huduma katika Hospitali ya Nairobi, Avenue, Guru Nanak na Hospitali ya Chuo Kikuu cha Aga Khan, huku hospitali hizo zikisubiri uthibitisho au idhini chini ya mfumo wa SHA.

Naibu Katibu Mkuu wa Kuppet, Bw Moses Nthurima, alionya kuwa chama hicho kinaweza kuwaelekeza wanachama wake kujiondoa kwenye mpango huo endapo hali haitarekebishwa.

“Tunakutana wiki ijayo tujadili hali ya SHA, na kama hawatarekebisha matatizo haya, tutawaambia walimu wetu wasusie mpango huo na waondoke. Huu ni mpango wa serikali lakini haijulikani walimu waende wapi. Hospitali zinawakataa na wengine hata wanapoteza maisha,” alisema Bw Nthurima.

Hata hivyo, Mamlaka ya Afya ya Jamii imekanusha madai kuwa walimu wanakumbwa na changamoto kubwa za kupata huduma za afya chini ya Mpango wa Bima ya Matibabu ya Mwalimu.

Katika majibu yake, Afisa Mkuu Mtendaji wa SHA Dkt Mercy Mwangangi, alisema visa vilivyoripotiwa ni vichache na si vya jumla.

Kulingana na data ya SHA, zaidi ya walimu 225,000 pamoja na jamaa wanaowategemea tayari wamepata huduma chini ya mpango huo.

Mamlaka hiyo ilisema inaendelea kuchambua matumizi na madai ya bima ili kubaini mapungufu ya upatikanaji wa huduma, kufuatilia utendakazi wa watoa huduma na kuboresha utoaji wa huduma.