Walioiba bastola ya mlinzi wa Gavana Barasa wakamatwa Kisumu, kushtakiwa
HATIMAYE polisi wa Kisumu wamewakamata washukiwa wanne na kukomboa bastola moja inayoaminika ilinyang’anywa mlinzi mmoja wa Gavana wa Kakamega Fernandes Barasa siku ya mazishi ya waziri mkuu wa zamani Raila Odinga, Bondo, Siaya.
Kwenye taarifa jana, Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) ilisema wanne hao walikamatwa kufuatia operesheni kali iliyoendeshwa na maafisa wa polisi katika Kaunti Ndogo ya Kisumu Mashariki.
“Baada ya kupashwa habari na umma, maafisa wetu walivamia nyumba moja katika kitongoji duni cha Manyatta “B” katika eneo la Mbeme na kuwakamata washukiwa wanne. Walitambuliwa kama; Timothy Odhiambo, David Beckham Odhiambo, Tony Blair Omondi na Harun Ibrahim,” DCI ikasema kwenye taarifa kwenye akaunti yake ya mtandao wa X (zamani, twitter).
Baada ya kuhojiwa, washukiwa waliwaongoza maafisa wa upelelezi katika maficho mengine ambapo walipata bastola aina ya Jericho ikiwa na risasi 14.
“Uchunguzi umebaini kuwa bastola iliyopatikana ni ile iliyonyang’anywa afisa mmoja wakati wa mazishi ya Mheshimiwa Raila Amolo Odinga mnamo Oktoba 19, 2025 Bondo, kaunti ya Siaya. Washukiwa hao wanazuiliwa kabla ya kuwasilishwa kortini kujibu mashtaka,” DCI ikaeleza.
Baadhi ya kutamatika kwa ibada ya mazishi ya Odinga katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Jaramogi Oginga Odinga (JOOUST), afisa wa GSU ambaye ni mmoja wa walinzi wa Gavana Barasa alinyang’anywa bunduki hiyo akiwa na wenzake wakiondoka na bosi wao.
Aliyetwa silaha hiyo alitoweka ndani ya umati mkubwa wa watu waliohudhuria ibada hiyo.
Duru zilisema wahuni waliwapora mali ya watu kadhaa wakati na baada ya ibada hiyo iliyovutia waombolezaji kutoka sehemu mbalimbali nchini na ng’ambo.