Habari

Walioteuliwa IEBC kupigwa msasa bungeni lakini watasubiri kesi kujua hatima yao

Na JOSEPH WANGUI May 29th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

Mahakama Kuu imeruhusu Bunge kuendelea na mchakato wa kuwapiga msasa watu saba walioteuliwa na Rais William Ruto kusimamia Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).

Hata hivyo, mahakama imezuia uteuzi wao kuchapishwa rasmi na kuapishwa kwao hadi kesi inayopingwa kuteuliwa kwao itakaposikilizwa na kuamuliwa.

Kesi hiyo iliwasilishwa na wapiga kura wawili, Kelvin Roy Omondi na Boniface Mwangi, ambao wanapinga uteuzi huo kwa madai kuwa Rais Ruto hakuzingatia usawa wa kikanda katika uteuzi wa mwenyekiti na makamishna sita, na kuna maswali kuhusu uhalali wa baadhi yao.

Jaji Lawrence Mugambi alisema kuwa kuzuia kuapishwa ni muhimu ili kesi isifanyike kuwa ya bure, kwani  ikigunduliwa baadaye kuwa mchakato ulikuwa na makosa, kuondolewa kwa makamishna wa tume hiyo si kazi ya mahakama bali ni mchakato wa kikatiba unaohusisha Bunge.

“Wapiga kura wameonyesha kuwa kesi yao ina msingi imara na maswali makubwa ya kikatiba yanahitajika kujibiwa,” alisema jaji Mugambi.

Kesi inaeleza kuwa baadhi ya walioteuliwa Erastus Edung Ethekon (mwenyekiti), Hassan Noor Hassan, Mary Karen Sorobit na Anne Nderitu, hawastahili kuteuliwa kutokana  na uhusiano wao wa kisiasa na kazi walizofanya awali.

Aidha, wanalalamika kuwa Rais  hakushirikisha vyama vya upinzani katika mchakato wa uteuzi kama ilivyoainishwa katika ripoti ya Kamati ya Mdahalo wa Kitaifa (NADCO) na Sheria ya Marekebisho ya IEBC ya mwaka 2024.

Maswali mengine yanayoibuliwa ni iwapo uteuzi huo ulizingatia usawa wa kikanda, kwani wawili walioteuliwa wanatoka katika eneo la Rift Valley huku maeneo kama Mashariki yakikosa kuwakilishwa.

Jaji Mugambi pia alibainisha kuwa kuna maswali kuhusu iwapo Rais na Kamati ya Uteuzi walitakiwa kufichua hadharani ripoti ya mahojiano na utendaji wa wawaniaji, jambo ambalo halikufanyika.

Kesi imepelekwa kwa Jaji Mkuu Martha Koome ili ateue jopo la majaji kuisikiliza.