Habari

Wapinzani wangu wataonea mamlaka dirishani – Ruto

Na SHABAN MAKOKHA  June 16th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto ameapa kutowapokeza mamlaka ya uongozi wa taifa kwa viongozi wa upinzani aliowataja kama watu wasio na ajenda madhubuti ya kuendeleza serikali.

Akiongea jana katika kaunti ya Kakamega, Dkt Ruto aliwataka vinara wa upinzani kama vile aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, kiongozi wa chama cha People Liberation Party (PLP) na mawaziri wa zamani Eugene Wamalwa na Fred Matiang’i kama watu waliochanganyikiwa na hawana sifa zozote za uongozi.

Kiongozi wa taifa alidai kuwa haja kuu ya viongozi hao ni kumwondoa mamlakani na hawana mipango ya kuimarisha maslahi ya Wakenya na kutekeleza maendeleo nchini.

“Ajenda yao kuu ni “Ruto Must Go” (Sharti Ruto aondoke). Hawana lolote lingine.. “Ruto Must Go” itawasaidia vipi Wakenya wanaokabiliwa na changamoto za kugharamia mahitaji yao ya kimatibabu, masomo ya watoto wao miongoni mwa changamoto zingine?”, akauliza.

Dkt Ruto alisema hayo alipohudhuria hafla ya kanisa na mkutano wa kila mwaka wa Kanisa la Friends Quakers na Matete Christiano Fellowship katika uwanja wa Shule ya Kivaywa Comprehensive School, eneo la Lugari, kaunti ya Kakamega.

Alisema upinzani hauna mipango ya kuzalisha nafasi za ajira kwa vijana, hawafahamu namna ya kufadhili mipango ya elimu, na kuendeleza sekta za kilimo na afya.

“Wamejawa na hasira kiasi kwamba hawana mpango wa kufanya chochote chenye manufaa kwa Wakenya. Hatuwezi kuwapokeza mamlaka watu wasio na mipango yoyote. Kila mara huenekana wenye hasira kana kwamba kuna mtu aliyewakosea.

“Wakome kuwasumbua Wakenya wengine na wakabiliane nami moja kwa moja endapo wanahisi wanazo tofauti zozote name. Nitapambana nao vilivyo,” akasema Dkt Ruto.

Kiongozi wa taifa alisema huku akiweka mipango ya kuwabadilisha maisha ya Wakenya wote chini ya serikali jumuishi, lengo la viongozi wa upinzani ni kusambaratisha mipango ya kufikiwa kwa ahadi ambazo aliwapa Wakenya wakati wa kampeni za kuelekea uchaguzi mkuu uliopita.

“Kabla ya uchaguzi uliopita, nilizunguka kote nchini nikizungumza na Wakenya na kuweka mikakati ya kushughulikia mahitaji yao. Ninajua kile Wakenya wanahitaji na namna ya kuitimiza. Lakini wakiendelea kuniwekea vikwazo, nitakabiliana nao bila huruma kwa sababu lengo lango ni kuona Wakenya wote wakiishi bila matatizo,” akasema.

Kauli ya Rais Ruto inaonekana kuakisi ile ya mtangulizi wake Uhuru Kenyatta ambaye, kabla ya uchaguzi mkuu wa 2022, aliapa kutopokeza mamlaka kwa kiongozi ambaye alimtaja kama “mwizi”.

Hata hivyo, baada ya Rais Ruto kutawazwa mshindi katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022, Bw Kenyatta alijitokeza mnamo Septemba 13, 2022 na kumpokea mamlaka kwa amani.

Jana, Rais Ruto aliahidi kuwa serikali yake itakamilisha miradi yote ya maendeleo iliyokwama katika kaunti ya Kakamega na maeneo mengine ya nchi.

Alisema baadhi ya miradi hiyo ilianzishwa na serikali kuu zama za mwaka wa 2014 na mengine yaliyoanzishwa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2022.

Rais Ruto alisema miradi hiyo ilikwama kutokana na mipango mibaya wakati wa ugavi wa fedha za bajeti katika miaka ya nyuma.

“Mipango mibaya ilipelekea pesa za mgao wa bajeti kuisha mapema kabla ya miradi yenyewe kukamilika. Wakati humo tunayo mipango mizuri ya bajeti na tunawahakikisha watu wa Kakamega kwamba miradi yote iliyoanzishwa kama vila miradi ya barabara, umeme na maji itakamilika hivi karibuni,” akasema.