Habari

Watumishi wa umma wakosa matibabu serikali ikichelewesha kuachilia ada za SHA

Na MERCY CHELANGAT June 24th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WATUMISHI wa umma wanatatizika kupata matibabu baada ya serikali kukosa kuwasilisha michango yao kwa Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA) kwa wakati.

Ingawa asilimia 2.75 ya mishahara yao hukatwa kila mwezi, pesa hizo hazifiki kwa SHA kwa wakati unaofaa. Matokeo yake ni kwamba mfumo wa SHA, huwazuia kupokea huduma za afya.

Hali hii imegeuka kuwa donda ndugu linalowaumiza maelfu ya watumishi wa umma nchini.

Hata baada ya kuchangia kwa uaminifu kila mwezi, wanapohitaji huduma za afya, iwe ni kwa dharura au uchunguzi wa kawaida, wanaambiwa hawawezi kuhudumiwa kwa sababu ‘hawajasajiliwa kikamilifu’ au michango yao ‘haijapokewa’.

Mfumo unaoonekana kuwa wa haki na wa kitaifa umekuwa kikwazo cha maisha ya wale unaopaswa kuwalinda.

Kile kinachofanya mgogoro huu kuwa mbaya zaidi ni kwamba baadhi ya waathiriwa ni wafanyakazi wa Wizara ya Afya yenyewe, wanaosimamia utekelezaji wa SHA.

Wanalazimika kulipia matibabu kwa pesa zao binafsi, licha ya kuwa wamechangia kupitia mishahara yao. Hali hii imewafanya wengi kuhisi kusalitiwa na mfumo wanaotumikia kwa bidii.

Kwa mujibu wa takwimu kutoka kwa Katibu wa Idara ya Huduma za Matibabu, Dkt Ouma Oluga, kati ya waajiri 98,112 walioandikishwa kwenye mfumo wa SHA, ni 53,000 pekee wanaozingatia masharti ya kuwasilisha michango.

Zaidi ya waajiri 44,000 hawazingatii, hali inayoathiri mamia ya maelfu ya wafanyakazi. Katika Kaunti ya Nairobi pekee, waajiri 12,900 wanadaiwa jumla ya Sh4.7 bilioni.

SHA sasa imeanzisha kampeni ya wiki sita ya kwenda ‘mlango kwa mlango’ kwa waajiri hao wasiotii, ili kushinikiza ulipaji wa madeni na kurejesha haki za afya za wafanyakazi.

Mkurugenzi Mkuu wa SHA, Dkt Mercy Mwangangi, alitangaza Jumatatu kuwa maafisa wa mamlaka hiyo wataanza kuwatembelea waajiri ambao hawazingatii sheria moja kwa moja ili kuhakikisha wanalipa michango.

“Kuanzia leo hadi wiki sita zijazo, tutakuwa tukitembelea waajiri nchi nzima kuhakikisha kwamba wanazingatia ulipaji wa michango kwa SHA,” alisema Dkt Mwangangi wakati wa uzinduzi wa mpango wa matokeo ya haraka wa kufuatilia ulipaji wa michango.

Hata hivyo, watumishi wa umma wengi bado hawana imani na hatua hiyo, wakihisi imechelewa mno na haiwezi kurekebisha mateso wanayoyapitia kila mwezi.

“Kila mwezi wanakata pesa zetu kwa uangalifu mkubwa. Lakini tarehe 10 ikifika, tunafungiwa nje ya mfumo. Tunafukuzwa na hospitali, tunalazimika kulipa pesa taslimu. Sisi ni watumishi wa umma waaminifu, lakini wakati tunapohitaji huduma, mfumo wetu wenyewe unatugeuka. Huu ni usaliti wa imani,” alisema mtumishi wa umma aliyeomba asitajwe jina.

Kwa sasa, watumishi wa umma wameachwa kwenye hali ya sintofahamu huku wakiendelea kuchangia kwa mfumo ambao hauwatendei haki.

Wanadai mabadiliko ya haraka, si maneno au mikutano, bali suluhu ya kweli inayoweka afya na utu wa wafanyakazi mbele ya urasimu na uzembe wa kiutawala.