Wazazi kote nchini wahangaika kutafuta chanjo kila hospitali ikikaukiwa
WAZAZI kote nchini wanapitia wakati mgumu kufuatia uhaba mkubwa wa chanjo za watoto wachanga, hali inayolazimu baadhi yao kuzunguka hospitali mbalimbali kusaka chanjo ya kwanza ya watoto wao, bila mafanikio.
Bi Naomi Wesonga, mama aliyejifungua mtoto wake wa kwanza Jumatano, Mei 28 katika Hospitali ya MP Shah, ni miongoni mwao.
Akiwa na hofu na mshtuko, alieleza kuwa wauguzi wa hospitali hiyo walimwambia hawana hata chanjo ya msingi kama BCG na polio.
“Niliambiwa watoto wote waliozaliwa hapa wiki mbili zilizopita bado hawajapata chanjo. Wametwambia turudi Alhamisi kuona kama dozi 20 za BCG walizokuwa wakisubiri zitakuwa zimefika,” alisema Naomi kwa huzuni.
Naomi alilazimika kutafuta chanjo hiyo katika hospitali nyingine kama Aga Khan, Mbagathi, na hata Kenyatta University Teaching and Referral Hospital (KUTRRH), lakini alipata majibu yale yale ya kukosa chanjo.