Waziri akemea uharibifu uliotokea wakati wa maandamano ya Gen Z
WAZIRI wa Huduma ya Umma, Geoffrey Ruku, amekashifu vikali uharibifu ulioshuhudiwa kote nchini katika maandamano ya Gen Z majuzi.
Akizungumza Alhamisi Mbeere Kaskazini, Kaunti ya Embu, wakati wa shughuli ya kushirikisha umma, Bw Ruku alishutumu upinzani kwa kula njama ya alichotaja “ugaidi uliopangwa, machafuko, na msururu wa uharibifu” kwa kisingizio cha maandamano ya amani.
Alishutumu kundi la kisiasa lililojitenga kwa kuhujumu umoja wa nchi ili kujinufaisha binafsi kisiasa, akionya Wakenya hawatastahimili jaribio lolote la kuzua misukosuko nchini kwa kisingizio cha uanaharakati.
“Wakenya hawataruhusu watu wenye ubinafsi kuvuruga amani na utulivu ambao tumejitahidi kujenga,” alisema Bw Ruku.
“Huwezi ukapata uongozi kwa kugawanya nchi. Hakuna manufaa yoyote kusaka mamlaka kupitia uchochezi na kusambaratisha taifa.”
Waziri alihimiza upinzani kutafuta mamlaka kwa njia ya heshima kwa kuwasilisha maono na mipango yao kwa Wakenya badala ya kujihusisha na siasa duni zinazochochea taharuki na utengano.
Waziri aliwapongeza wanajamii ya Mbeere kwa kujituma kushiriki midahalo ya maendeleo akisisitiza serikali imejitolea kuimarisha shughuli kama hizo katika kaunti zote.
Alitoa wito kwa Wakenya kukataa siasa za migawanyiko na badala yake kufanya kazi kujenga jamii yenye ushikamano na ujumuishaji.
Kuhusu suala la vijana kukosa ajira na kujumuishwa kiuchumi, Waziri aliangazia juhudi mpya za serikali kuimarisha vijana kupitia ujuzi wa maendeleo na mipango ya ajira.
Alitangaza kuwa wizara yake inafanya kazi kwa ushirikiano na mashirika mengineyo ya serikali kuimarisha na kupanua Mpango wa Kitaifa kuhusu Mafunzo ya Kazi.
“Tumejitolea kuhakikisha vijana nchini humu hawaachwi nyuma. Mpango wa mafunzo ya kazi utaboreshwa kutoa tajriba na kufungua mikondo ya ajira kwa vijana wetu,” alisema.