Habari

Magunia ya bangi yanaswa Nakuru

July 24th, 2018 1 min read

NA PETER MBURU

Polisi mjini Nakuru Jumanne walinasa gari lililokuwa likisafirisha bangi kuelekea upande wa Nairobi, ikihofiwa kutoka taifa jirani.

Gari hilo aina ya Fielder (KBZ 676Z) lilikamatwa eneo la Mbaruk, kilomita chache baada ya kupita mji wa Nakuru likiwa limejaa magunia na misokoto ya bangi.

Maafisa wa usalama waonyesha mbinu ambazo walanguzi huweka bangi wakati wa usafirishaji. Picha/ Peter Mburu

Kulingana na naibu wa kamishna wa kaunti eneo la Nakuru Mjini Mashariki Herman Shambi, bangi hiyo ina dhamana ya Sh1.3milioni na ilipitia sehemu za magharibi mwa nchi.

Bw Shambi aliwaonya wale wanaotumia barabara hiyo kusafirisha bidhaa haramu kwa watakamatwa na polisi wa kaunti hiyo ambao wako macho kila wakati.

Maafisa wastaajabu kuona maelfu ya misokoto ya bangi iliyonaswa Nakuru. Picha/ Peter Mburu

“Watafute njia mbadala kwa kuwa hapa lazima tutawakamata, hivi ni vita ambavyo tutapambana navyo kwa kuwa askari wetu wako imara na wamejipanga vizuri,” akasema Bw Shambi.

Afisa huyo aidha aliwatahadharisha wazazi kuwa makini kuchunguza mienendo ya watoto wao haswa wakati huu ambapo likizo ya shule inaelekea, akisema baadhi ya wanafunzi wamekuwa walengwa wa soko la mihadarati.

Magunia ya bangi yaliyonaswa mjini Nakuru. Picha/ Peter Mburu

“Hii bangi inauziwa wakenya na imeharibu watoto wengi sana, wazazi tuangalie maadili na mienendo ya watoto wetu. Huenda baadhi ya visa vya utovu wa nidhabu tunavyosikia kutoka shule nyingi vinatokana na mambo haya,” akasema Bw Shambi.

Bidhaa hizo zilipelekwa katika makao makuu ya idara ya ujasusi Nakuru, huku polisi wakisisitiza kuwa uchunguzi mkali tayari umeanzwa kuwakamata waliokuwa kwenye gari hilo kwani walitoroka kwa miguu.

Polisi waliongeza kuwa watachunguza na kumkamata mmiliki wa gari hilo, ili asaidie katika uchunguzi.