Makala

Mwanamfalme Andrew aachiliwa uchunguzi ukiendelea

Na REUTERS, WINNIE ONYANDO February 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ANDREW Mountbatten-Windsor, kakake Mfalme Charles wa Uingereza, aliyekamatwa Februari 19, 2026 kwa utovu wa maadili akiwa kazini ameachiliwa huru uchunguzi ukiendelea.

Haya yanajiri huku Mfalme Charles akisisitiza kuwa mkondo wa sheria lazima ufuatwe.

Mwanamfalme huyo alikamatwa kutokana na madai kwamba alituma stakabadhi muhimu za serikali kwa Jeffrey Epstein.

Mountbatten-Windsor, ambaye ana umri wa miaka 66, alikuwa akihojiwa siku nzima na wapelelezi kutoka Polisi wa Bonde la Thames.
Kukamatwa kwake ni jambo ambalo halikuwa likitarajiwa katika nyakati za kisasa.

“Nimepokea kwa huzuni habari kuhusu kukamatwa kwa Andrew Mountbatten-Windsor na tuhuma za utovu wa nidhamu katika ofisi ya umma,” Mfalme Charles alisema katika taarifa huku akisisitiza kuwa sheria utafuatwa.

Shahidi wa Reuters alimuona mkuu huyo wa zamani akitoka kituo cha polisi huko Aylsham, mashariki mwa Uingereza, ambapo alikutana na waandishi wa habari.

Picha ya Reuters iliyopigwa baada ya kuachiliwa kwake inamuonyesha ameketi ndani ya gari, akionekana kutetemeka.

Polisi wa Bonde la Thames walisema baadaye Alhamisi kwamba “mtu aliyekamatwa aliachiliwa uchunguzi ukiendelea.’

Epstein ndiye mhusika mkuu wa sakata ya kushtua ya ngono na watoto na ambaye alijiua akiwa jela akitumikia kifungo cha makosa hayo nchini Amerika.

Polisi wa Uingereza kwa kawaida huwa hawataji washukiwa ila walitoa maelezo yaliyomfichua mwanamfalme huyo wa zamani, ambaye amekuwa akichunguzwa kwa madai kwamba alituma stakabadhi hizo kwa Epstein alipokuwa anafanya kazi kama balozi wa biashara.

Mwanamfalme huyo, mvulana wa pili wa marehemu Malkia Elizabeth amekuwa akikanusha kutenda maovu katika uhusiano wake na Epstein.

Lakini hajakuwa akijibu maombi ya kuzungumzia sakata hiyo haswa katika siku za hivi karibuni ambapo stakabadhi nyingi zimetolewa na serikali ya Amerika zikieleza kwa kina kuhusu sakata hiyo ya watu mashuhuri duniani walivyoshiriki karamu za ngono na watoto kwa miaka mingi, almaarufu The Epstein Files.

Iwapo Andrew atapatikana na hatia anaweza kufungwa maisha gerezani na kesi yake itaendeshwa na Mahakama ya Kifalme ambayo huhusika na makosa makubwa ya jinai.

Mnamo 2022, Andrew alishtakiwa na mwanamke Mwamerika Virginia Giuffre ambaye alidai alimdhulumu kimapenzi akiwa tineja.

Hata hivyo, kukamatwa kwa Andrew kwa sasa hakuhusiani na kosa la kingono.

Mwanamfalme huyo wa zamani alilazimika kujiondoa kwenye majukumu yake ya kifalme 2019 kuhusiana na uhusiano wake na Epstein na kakake mkubwa akamvua uanamfalme kabisa mwaka jana Oktoba pale ufichuzi zaidi ulipopatikana kuhusiana na aina ya shughuli alizokuwa akijihusisha nazo na Epstein.

Mapema mwezi huu, Mfalme Charles alimlazimisha kaka yake, Mountbatten-Windsor, kuondoka katika nyumba yake ya muda mrefu wa Royal Lodge karibu na Windsor Castle.

Mountbatten-Windsor alihamishiwa katika makazi ya muda katika Wood Farm Cottage kwenye Sandringham Estate ya mfalme mashariki mwa Uingereza.

Alitarajiwa kuhamia katika nyumba ambayo kwa sasa inafanyiwa ukarabati.