• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 7:12 PM
MAPOZI: Eve D’Souza

MAPOZI: Eve D’Souza

Na PAULINE ONGAJI

SURA yake sio geni katika uwanja wa burudani nchini ambapo ametupambia skrini zetu za televisheni kwa vipindi mbali mbali.

Anafahamika kama Eve D’Souza, mmojawapo wa waigizaji ambao wamejiundia umaarufu kupitia vipindi kwenye televisheni na hivyo kuorodheshwa miongoni mwa utumbuizaji wanaotambulika sana nchini Kenya.

Mchango wake katika ulingo wa burudani unadhihirika kupitia vipindi na filamu ambazo ameshiriki.

Hasa amefanikiwa kunasa macho ya wengi kupitia mchango wake kama mwigizaji mkuu katika kipindi Auntie Boss kinachopeperushwa kwenye kituo cha televisheni cha NTV ambapo anaigiza kama Varshita, kando yake Maqbul Mohammed.

Katika kipindi hiki Maqbul anajipata amekwama katika uhusiano mbaya na Varshita, fungamano linalozidi kukera kila kuchao.

Sio katika kipindi hicho tu anacholeta ladha ya ucheshi kwani pia katika kipindi Varshita kinachopeperushwa kupitia kituo cha Maisha Magic East, mkondo ni huo huo, suala ambalo linalodhihirisha ucheshi wake.

Lakini mbali na vipindi hivi viwili, ameshiriki katika Freelance, Big  Brother Africa 3, MCEE Africa, Vibe City, Travel Diaries ambapo aliigiza kama yeye mwenyewe na pia Mentality.

Na katika harakati hizo amepata fursa ya kufanya kazi na baadhi ya waigizaji wanaong’aa nchini ikiwa ni pamoja na Nyce Wanjeri, Grace Muna, Maqbul Mohammed, David Opondoe na Sandra Dacha miongoni mwa wengine.

Lakini hata anavyozidi kung’aa kama muigizaji, D’Souza hajatamba tu katika fani hiyo kwani pia amehusika katika nafasi mbali mbali kama vile produsa, msimamizi wa uundaji vipindi na mtangazaji wa redio.

Ustadi wake kama mtangazaji ulidhihirika alipojishinda tuzo ya mtangazaji bora wa kike kwenye tuzo za Chat Awards mfululizo katika mwaka wa 2003 na 2004.

Alizaliwa miaka 39 iliyopita katika Kaunti ya Mombasa kama mwanawe Andrew na Martina D’Souza ambapo alisoma katika shule za Loreto Convent na Aga Khan, Mombasa.

Baadaye alijunga na Chuo Kikuu cha Catholic University of Eastern Africa (Cuea) jijini Nairobi ambapo alisomea ualimu wa lugha ya Kingereza na fasihi ya Kiingereza.

Safari yake katika ulingo wa burudani iling’oa nanga mwaka wa 2001 alipojiunga na kituo cha redio cha 98.4 Capital FM, nafasi aliyohudumu hadi Novemba 2010 ambapo alikuwa mtangazaji mkuu wa vipindi Hits not Home work, The East African Chart na Capital in the Morning.

Lakini ufanisi huu haujamhepusha na majanga kwani wakati mmoja alifichua kwamba yeye ni mhanga wa ubakaji. Tukio hilo lililotokea mwaka wa 2005 baada ya kutekwa nyara, suala lilimuathiri kwa miaka.

Lakini licha ya hayo, hakuacha nyota yake ididimie kwani muigizaji huyu ameendelea kutumbuiza.

Kwa sasa kando na kuigiza katika vipindi mbali mbali, D’Souza anaendesha kampuni ya kuunda vipindi ya Moonbeam Productions kinachohusika katika kurekodi kipindi cha ucheshi cha Auntie Boss.Pia, yeye ni balozi wa kampuni ya mavazi ya Store 66, jijini Nairobi.

Japo hajapata tuzo yoyote kutokana na uigizaji licha ya kufumu katika fani hii kwa takriban miongo miwili, haina shaka kwamba amechangia pakubwa katika sekta ya kuzalisha vipindi nchini.

Sasa swali kuu ni iwapo atapanua himaya yake na kuongeza mawazo mengine kwenye kazi zake, kando na ucheshi tu!

You can share this post!

AUNTY POLLY…: Mbona navamiwa na chunusi usoni?

SWAGG: Angela Bassett

adminleo