Afya na Jamii

Familia yaonewa na kansa jamaa sita wakipitia mahangaiko makuu ndani ya miaka 31

Na HELLEN SHIKANDA February 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

ULIMWENGU unapoadhimisha siku ya kansa mwaka huu, Brian Tende Mwakuro na mwanawe Harold Tende wanajua ukweli wa maumivu ya ugonjwa huo unaoandama familia yao.

Wanaonekana wenye afya nzuri, ajabu kwa watu waliopitia mapambano mengi ya saratani—si yao pekee, bali pia ya wanafamilia wao kwa kipindi cha zaidi ya miongo mitatu.

Kwa Brian, saratani imekuwa mgeni asiyealikwa katika maisha yake tangu 1993, wakati mke wake wa kwanza alipogunduliwa na saratani ya matiti. Alikuwa amegundua uvimbe kwenye titi lake la kulia alipokuwa akimnyonyesha binti yao mchanga.

Wakati huo, habari kuhusu saratani zilikuwa haba sana ikilinganishwa na ilivyo leo. Alifariki dunia mwaka huo huo aliogunduliwa kuwa na ugonjwa huo.

Miaka kadhaa baadaye, mama yake Brian aligunduliwa na saratani ya mlango wa uzazi. Baba yake naye alifuata na saratani ya tezi dume. Hata hivyo, hakuna kilichomuandaa kwa kile kilichofuata.

Mnamo 2015, Harold alianza kupata matatizo ya mara kwa mara ya shingo. Akiwa shule ya upili, alianza kutokwa damu puani mara kwa mara na maumivu ya kichwa.

Familia ilikuwa na matumaini kuwa ziara za hospitali zingepungua kadri muda ulivyosonga.

Harold aliporudi nyumbani kutoka chuo kikuu wakati wa likizo, Brian aliona uvimbe kwenye shingo ya mwanawe na akasisitiza aonekane na daktari wa masikio, pua na koo.

Daktari huyo alichukua sampuli na kuzituma kwa mtaalamu wa maabara.

“Daktari alinipigia simu kuniarifu matokeo, na iligunduliwa alikuwa na saratani ya kichwa na shingo” anakumbuka Brian. Wakati huo, Harold alikuwa na umri wa miaka 19 pekee.

Harold alikamilisha matibabu yake na kusubiri kwa miaka mitano ili madaktari watangaze kuwa hana saratani.

Kufikia mwaka wa tano, hakukuwa na dalili zozote za saratani mwilini mwake.

Alirejea katika maisha ya kawaida, akaanza kucheza raga na kuwa ushahidi hai kuwa watu wanaweza kupona saratani.

Hata hivyo, mwaka wa saba, dalili za ajabu zilirejea, zilizoanza kama mafua ya kawaida. Alienda hospitalini peke yake na ndipo alipopata taarifa kuwa alikuwa na saratani ya mapafu.

Alikamilisha matibabu kwa mara ya pili. Katika yote hayo, utulivu wa Harold ulimpa baba yake nguvu. Alikataa kuhurumiwa.

“Huyu kijana ni askari wa saratani. Imani yake ni ndefu kama kimo chake,” anasema Brian.

Baada ya Harold kumaliza matibabu yake na kuanza tiba ya kinga mwilini ambayo husaidia mwili kupambana na seli za saratani, Brian naye aligunduliwa kuwa na saratani ya tezi dume katika hatua ya kwanza.

“Nimekuwa na kisukari kwa takribani miaka 17 na nilikuwa na matatizo ya kukojoa, lakini sikujua ningepata saratani,” anasema.

Hali yake iligunduliwa kwa bahati. Alikuwa amelazwa hospitalini kutokana na matatizo ya kisukari alipomweleza daktari wake kuhusu changamoto za kukojoa, naye akapendekeza vipimo zaidi.

Moja ya vipimo hivyo vilithibitisha alikuwa na saratani.

Awali, Brian alipata matibabu Mombasa kabla ya kuhamishiwa Nairobi. Alizunguka hospitali kadhaa kabla ya kuamua Aga Khan University Hospital matibabu. Mwezi Desemba mwaka jana, alimaliza matibabu yake.

Licha ya baba na mwana kupitia matibabu yanayofanana,uzoefu wao ulitofautiana sana.

Brian alifaidika na mashine mpya iitwayo ‘linear accelerator’, ambayo ilisababisha athari chache na muda mfupi wa kulazwa hospitalini.

Alipata maumivu ya sehemu ya chini ya mgongo na muwasho pekee. Matibabu ya Harold yalikuwa makali zaidi—yaliathiri sauti yake, ngozi, sauti na yakakausha tezi zake za mate.

“Mwanangu amepitia hali mbaya zaidi, na hilo ndilo linanipa matumaini. Kuwa na saratani sio mwisho wa maisha. Tunahitaji tu kuishi kwa mtazamo chanya,” anasema Brian.

Kaulimbiu ya Siku ya Dunia ya Saratani mwaka huu, iliyoandaliwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) ni: “Tumeunganishwa kwa Upekee”, ikikumbusha kuwa ingawa saratani ni tishio la kimataifa, kila nchi, jamii na mtu aliyeathirika hukumbana na hali tofauti.

Dkt Angela Waweru Daktari wa Saratani, anaeleza kuwa, mashine ya linear accelerator huwezesha matibabu kwa usahihi wa hali ya juu.

Anaeleza kuwa wagonjwa wa saratani ya tezi dume ambao awali walihitaji wiki nane za matibabu sasa hukamilisha awamu zao tano pekee ndani ya wiki mbili, huku wakipata athari chache.

Kwa wagonjwa wa saratani ya matiti, matibabu ambayo awali yalichukua wiki tano hadi sita sasa yanahitaji wiki moja tu.