Hali inayochangia ugonjwa wa bawasiri
IWAPO unatumia simu yako unapoenda haja kubwa, huenda ukawa kwenye hatari ya kuathiriwa na kuvimba kwa mishipa ya damu iliyopo ndani au katika eneo linalozunguka njia ya haja kubwa.
Ugonjwa huu unafahamika kwa kimombo kama hemorrhoids, au bawasiri/hemoroidi kwa Kiswahili.
Dkt Mark Siboe, daktari wa upasuaji, anasema kuwa kutumia nguvu nyingi kuenda haja kubwa, na kutokula vyakula vyenye nyuzinyuzi husababisha hali hii.
Isitoshe, kuketi kwa muda mrefu, kama wanavyofanya madereva wa malori na wafanyakazi ofisini angalau kwa zaidi ya saa sita kwa siku, huongeza shinikizo kwenye sehemu ya haja.
“Kazi za kubeba mizigo mizito, kuwa na uzito kupindukia, mazoezi yenye kutumia nguvu nyingi ya mara kwa mara pia yanachangia ugonjwa huu,” anasema Dkt Siboe.
Hata hivyo, ili kuendelea kufanya mazoezi kwenye ukumbi wa mazoezi, Dkt Siboe anashauri kutoa pumzi wakati unainua zaidi ya kilo 25 na kuepuka kuinua uzito mkubwa kama unatatizika mara kwa mara.
Ugonjwa huu huathiri kina nani zaidi?
“Ugonjwa huu huathiri hadi asilimia 40 ya watu wazima, hasa walio na umri wa zaidi ya miaka 50. Lakini aibu na wasiwasi wa kijamii huwakwamisha wengi—hasa wanaume—kutafuta matibabu,” anaeleza.
Dkt Siboe, anasema kuwa hii ni kwa sababu, kadri miaka inavyosonga, hasa kati ya umri wa miaka 40 hadi 60, uzee au jenetiki huleta udhaifu kwenye tishu za mwili.
“Kudhoofika kwa tishu za kolajeni na elastini kutokana na sababu ya umri au jeni—kama sofa yako uipendayo inavyoanza kulegea. Tishu zako huwa dhaifu vivyo hivyo.”
Dalili za ugonjwa huu ni pamoja na kutokwa na damu wakati wa haja, kuwashwa karibu na sehemu ya haja, uvimbe kwenye tupu ya nyuma, na maumivu—hasa katika sehemu zilizofura na kujaa damu (thrombosed).
Je, krimu na matibabu ya kinyumbani husaidia?
“Krimu za dukani au tiba za nyumbani husaidia kutuliza maumivu tu kwa muda mfupi. Hata hivyo, iwapo dalili za mgonjwa zinazidi baada ya wiki moja, ni bora kufika hospitalini kwa ukaguzi,” anaeleza Dkt Siboe.
Isitoshe, hufai kutumia krimu hizi kwa zaidi ya siku saba lakini unaweza kalia maji ya vuguvugu mara mbili hadi tatu kwa siku kwa dakika 10.
Zaidi ya hayo Dkt Siboe anaonya dhidi ya kutumia tiba zisizothibitishwa kama mafuta ya tea tree, mshubiri (aloe vera), au tangawizi na kitunguu saumu iliyosagwa.
Kando na krimu na tiba za kinyumbani, Dkt Siboe anasema kuwa matibabu mengine ambayo mgonjwa hupokea hulingana na uvimbe kwenye tupu yake ya nyuma.
“Kuna wagonjwa ambao tunashauri kunywa angalau lita 1.5 hadi 2 za maji kila siku, waongezee ulaji wa vyakula vyenye nyuzinyuzi, tunawapa dawa za kulainisha haja yao kubwa na kuwashauri kukalia maji ya vuguvugu.”
Kwa walioathiriwa sana au wanaopata ugonjwa huu mara kwa mara, Dkt Siboe anaeleza kuwa hufanyiwa upasuaji.
Kuzuia uvimbe kwenye tupu ya nyuma
Ili kuzuia uvimbe huu kwenye tupu ya nyuma, Dkt Siboe anashauri kula vyakula vyenye nyuzinyuzi kama sukuma, spinachi, mboga za malenge, brokoli, maharagwe, ndengu, na matunda kama machungwa, na mananasi miongoni mwa mengine.
Pili, unapaswa kusimama kila baada ya dakika 30-45 na kutembeatembea kidogo.
“Kunywa maji mengi badala ya soda, chai au kahawa,” anasema na usikae msalani kwa zaidi ya dakika tano.
Pia, Dkt Siboe anashauri kuwa na mazoea ya kuenda haja kubwa wakati unahisi haja na usitumie nguvu nyingi unapokuwa msalani.
“Zoea kufanya mazoezi kila mara lakini usivute pumzi unapoinua chuma na uhakikishe kuwa uzito wako upo wastani.”
Je, ugonjwa huu huathiri tendo la ndoa?
Ingawa ugonjwa huu hauathiri moja kwa moja uwezo wa kushiriki ngono, usumbufu na aibu vinaweza kuathiri maisha ya karibu ya kimapenzi.
“Maumivu wakati wa shughuli fulani huweza kusababisha kuepuka tendo la ndoa, na hivyo kuathiri mahusiano,” anasema Dkt Siboe, hali hii ikichangia upweke kati ya wapenzi au wanandoa.