Jaribu vyakula hivi unapotatizwa na harufu mbaya kinywani
TATIZO la kutoa harufu mbaya kinywani hutokana na mambo mengi.
Hata hivyo, kuna baadhi ya vyakula ambavyo husaidia kukabiliana na shida hii. Kwa mfano:
Maji
Kunywa maji ndio mbinu sahili ya kukabiliana na tatio hili. Unapokunywa maji, unasuuza chembechembe za masalio ya chakula na seli zilizokufa, na hivyo kuzuia bakteria zinazosababisha harufu mbaya zisizaane kinywani mwako.
Mboga na matunda
Mboga na matunda kama vile tufaha, karoti na pea husaidia kuzalisha mate mdomoni ambayo husaidia kusafisha bakteria zinazosababisha harufu mbaya kinywani.
Tikiti maji na matunda jamii ya machungwa yana viwango vya juu vya vitamini C husaidia kusafisha kinywa na kuzuia bakteria zinazosababisha maradhi na matatizo mengine ya kinywani kama vile halitosis na gingivitis.
Kwa upande mwingine, matunda ya cheri husaidia kuondoa harufu ya gesi ya methyl mercaptan, ambayo hupatikana katika vyakula kama vile vitunguu na chizi, na ambayo husababisha harufu mbaya kinywani.
Tangawizi
Tangawizi ina kiungo kinachoitwa 6-gingerol, ambacho huchochea kimeng’enyo kwenye mate ambacho husaidia kuvunjavunja madini ya sulfur kinywani. Jaribu kuchanganya tangawizi, juisi ya ndimu na maji moto kusuuza mdomo.
Chai ya kijani
Tafiti zinaonyesha kwamba viungo vilivyo kwenye kinywaji hiki husaidia kukabiliana na bakteria zinazosababisha harufu mbaya kinywani.
Chingamu isiyo na sukari
Chingamu isiyo na sukari husaidia kuyeyusha na kuondoa chembechembe za masalio ya chakula na seli zilizokufa kwenye meno, ambazo husababisha harufu mbaya kinywani.
Chlorophyll
Kiungo hiki kinapatikana kwenye mboga ya majani ya kijani au yaweza patikana kama kijalizo. Kiungo hiki husaidia kupunguza harufu mbaya kinywani.
Yogurt iliyo na probiotics
Aina hii ya yogurt huwa na bakteria nzuri na yaweza saidia kukabiliana na bakteria zinazosababisha harufu mbaya mdomoni.