Afya na Jamii

Je, ni kawaida kupata usingizi mzito baada ya kushiriki mapenzi?

February 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

Mpendwa Daktari,

Mpenzi wangu hulala fofofo baada ya kushiriki tendo la ndoa. Huu ni ugonjwa?
Mellissa, Nairobi

Mpendwa Mellissa,

Kulala fofofo baada ya tendo la ndoa si ugonjwa kwa watu wengi; mara nyingi husababishwa na mabadiliko ya homoni kama oxytocin na prolactin pamoja na uchovu wa mwili baada ya shughuli ya kimapenzi.

Hali hii ni ya kawaida zaidi kwa wanaume lakini inaweza kutokea pia kwa wanawake.

Hata hivyo, kama usingizi huo unaambatana na uchovu kupindukia, kukosa hamu ya tendo la ndoa, au dalili nyingine za kiafya, ni vyema mpenzi wako amuone daktari kwa uchunguzi zaidi.

Nimekuwa na maumivu sehemu nyeti kwa miezi miwili, shida ni nini?

Mpendwa Daktari,

Nimekuwa nikihisi uchungu katika uume wangu. Tatizo lilianza baada ya kushiriki tendo la ndoa bila kinga na binti mmoja niliyekutana naye mtandaoni miezi miwili iliyopita. Tatizo laweza kuwa nini?
Ahmed, Mombasa

Mpendwa Ahmed,

Uchungu kwenye uume baada ya tendo la ndoa bila kinga unaweza kusababishwa na mambo kadhaa, hasa maambukizi ya zinaa kama vile kisonono, klamidia, kaswende au herpes, ambayo mara nyingine huanza kwa maumivu, kuashwa au kutokwa na uchafu.

Pia huenda ikawa ni maambukizi ya njia ya mkojo au jeraha dogo lililotokea wakati wa tendo.

Kwa kuwa dalili zimeendelea kwa muda wa miezi miwili, ni muhimu sana uende hospitalini haraka kwa vipimo vya maambukizi ya zinaa na upate matibabu sahihi.

Usijitibu mwenyewe na pia jiepushe na tendo la ndoa bila kinga hadi ufanyiwe tathmini kamili.