Afya na Jamii

Je, unafahamu manufaa ya chai ya ‘strungi’ kwenye mwili?

Na WANGU KANURI March 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MIAKA kumi iliyopita, Grace Muthoni, 33, alipata mzio (allergy) kutokana na unywaji maziwa ya ng’ombe na kuanza kunywa chai ya mkandaa.

Hivi sasa, yeye hunywa chai ya mkandaa angalau mara mbili kwa siku; asubuhi na usiku na huongeza tangawizi, limau, chungwa na mchaichai mara kwa mara ili ionje tofauti.

“Siwezi sema mimi ni mraibu wa ‘strungi’ kwani siku ambazo siinywi sipati madhara yoyote,” anasema.

Maryanne Wanza, mtalaamu wa lishe bora katika kliniki ya KINU Wellness, anaeleza kuwa chai ya mkandaa hutokana na majani na yale yanayochipuka ya mmea wa Camellia sinensis.

Kuweka majani ya chai kwenye maji hutengeneza kinywaji kisichokuwa na kalori, bila protini, wanga au mafuta kwa kiwango kikubwa.

“Lakini chai ya mkandaa huwa na kizimua oksijeni huru (antioxidants) kama flavonoids na polyphenols ambavyo vinaweza kusaidia afya na ustawi. Vizimua hivyo husaidia afya ya moyo, hupunguza uvimbe mwilini, hushusha viwango vya kolesteroli na huboresha afya ya njia ya chakula.”

Ni wakati gani ambapo chai ya mkandaa haina faida kwa mwili?

Chai ya mkandaa hukoma kuwa kinywaji chenye afya iwapo utainywa kwa wingi kwani inahusishwa na kafeini kupita kiasi, utaongeza sukari au krimu nyingi.

Pia, Bi Wanza asema iwapo utainywa kwa kiwango kikubwa karibu na muda wa kula chakula, utaathiri ufyonzwaji wa virutubisho mwilini.

Pia aongeza kuwa ikiwa utakuwa na mazoea na kuiotegemea kupita kiasi ili kuwa sawa basi haifai mwili wako.

Isitoshe, watu wanaopaswa kuwa waangalifu wanapokunywa chai ya mkandaa mara kwa mara ni pamoja na watu wenye kiwango cha chini cha madini ya chuma mwilini hasa walaji mboga tu.

“Hii ni kwa sababu chai ya mkandaa ina kemikali za tannins, ambazo hupunguza ufyonzwaji wa madini mwilini, kama vile madini ya chuma kutoka kwa mimea.”

Pili, watu wanaoathiriwa na kafeini wanaweza kupata wasiwasi, mapigo ya moyo kwenda kasi au kutotulia. Watu wanaotatizika kulala, na wanawake wajawazito.

Kina mama wajawazito, Bi Wanza anaeleza, hawapaswi kunywa zaidi ya vikombe viwili au vinne vya chai ya mkandaa kwa kiwango cha juu, sawa na miligramu 200 kwa siku.

Hii ni kwa sababu, kuzidisha viwango hivyo kunamtia kwenye hatari ya mimba kuharibika haswa mapema kwenye ujauzito wake. Ndio maana ni muhimu kudhibiti viwango vya kafeini.

Je, kunywa chai ya mkandaa usiku kunaweza kuathiri usingizi?

“Ndiyo. Kafeini iliyomo kwenye chai ya mkandaa huchochea mfumo wa fahamu, huchelewesha usingizi, na hupunguza ubora wa usingizi. Hata viwango vidogo tu (miligramu 40–50 za kafeini kwenye kikombe) vinaweza kuwaathiri watu wengine. Ni vyema kutokunywa kafeini saa 6–8 kabla ya kulala.”

Madhara ya chai ya mkandaa kupita kiasi ni pamoja na kukosa usingizi, wasiwasi, mapigo ya moyo kwa kasi, maumivu ya kichwa na kutotulia.

Isitoshe, Bi Wanza anasema kuwa wengine hupata matatizo ya umeng’enyaji wa chakula wanapohisi kuwa na gesi nyingi inayojaa tumboni hadi kooni.na ufyonzwaji wa madini ya chuma.

Ni njia ipi bora ya kuandaa chai ya mkandaa?

“Tumia majani mapya ya chai. Usitumie tena ‘tea bag’ kwani inaweza kushika ukungu, hasa ikihifadhiwa vibaya. Lowesha kwenye maji moto kwa dakika 3–5, epuka kunywa chai iliyo moto sana na kuinywa unapokula iwapo una upungufu wa madini ya chuma na punguza sukari au krimu zenye mafuta mengi.”

Hata hivyo, Bi Wanza anasema kuwa kwa ujumla, unapaswa tu kunywa angalau vikombe vitatu hadi vitano vya chai ya mkandaa kila siku.

“Kikombe kimoja cha chai ya mkandaa huwa na takriban miligramu 40–50 za kafeini. Miongozo mingi ya afya inapendekeza watu wazima wenye afya wasizidishe miligramu 400 za kafeini kwa siku.”