Afya na Jamii

Jinsi upatikanaji rahisi wa chapati umeanza kutia hofu wataalamu wa afya

Na WANGU KANURI May 30th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

CHAPATI huvutia Wakenya wengi kuizoea au kuitegemea kutokana na gharama yake nafuu, uwezo wake wa kushibisha kwa muda mrefu, na nafasi yake katika tamaduni za familia nyingi.

Aidha, urahisi wa upatikanaji wake; iwe kama unga au chapati zilizopikwa tayari katika vibanda na maduka, pamoja na uwezo wake wa kuliwa pekee au kuambatana na chakula au kinywaji chochote, huifanya chapati kuwa chaguo la wengi.

Ripoti ya Hali ya Uchumi ya mwaka huu ilionyesha kuwa uzalishaji wa unga wa ngano uliongezeka kutoka tani 1,495.7 elfu hadi tani 1,523.3 elfu.

Hata hivyo, mauzo ya pakiti 12 za kilo mbili yalipungua kutoka 2,508.4 mwaka wa 2023 hadi 2,283.4 mwaka jana — ishara kuwa kupungua kwa bei kuliwachochea wengi kununua unga huu kwa wingi.

Hata hivyo, uraibu wa chapati unaweza kuathiri afya, huku Bi Maryanne Wanza, mtaalamu wa lishe bora, akieleza kuwa utegemezi huu huanzia kwenye mazoea ya lishe yanayochochewa na ratiba, upatikanaji rahisi, au ukosefu wa mabadiliko katika mlo wa kila siku.

Katika hali kama hizi, watu hula chapati nyingi au mara kwa mara kila siku, bila kula vyakula vingine vyenye virutubisho muhimu.

“Kutegemea sana chapati kama chakula kikuu ni hali inayoonekana kwa chakula hicho kupatikana kwa urahisi au sehemu ya mila. Utegemezi huu pia unaonekana kwa vyakula vinavyovutia ladha kama keki, biskuti au krispi,” anasema Bi Wanza.

Mara nyingi, kutegemea huku kwa vyakula hivi huambatana na kupuuzwa kwa vyakula vya protini, mboga au matunda, huku mtu akila chapati 3–5 kwa kila chakula.

Hata hivyo, utegemezi huu wa hali ya juu wa chapati huenda ukawa ishara ya tatizo pana kama ulaji wa kutuliza kihisia au upungufu wa virutubisho.

Bi Wanza anasema, “Watu wanaokumbwa na msongo wa mawazo huweza kutumia chakula kupata faraja—hii huweza kuwa mtindo usiofaa wa ulaji. Pia inaweza kuwa ishara ya ukosefu wa aina tofauti ya vyakula au upatikanaji mdogo wa vyakula vingine vyenye virutubisho muhimu.”

Je, kuna madhara ya kiafya ya muda mfupi na mrefu ya kula chapati kupita kiasi—kila siku au mara kadhaa kwa siku?

Chapati nyingi hutengenezwa kwa unga mweupe wa ngano, chumvi na mafuta, hivyo ni muhimu kuzingatia athari za kiafya haswa vinapotumika kupita kiasi.

“Kula chapati nyingi hasa zilizotengenezwa kwa unga mweupe kunaweza kusababisha ongezeko la ghafla la sukari kwenye damu, kuvimba au kuhara, na kuhisi uchovu mwingi,” anasisitiza.

Unapozidi kula chapati kwa muda mrefu, Bi Wanza anasema unaweza ukaongezea uzito wako, mwili ukakosa virutubisho vya kutosha, viwango vya vya sukari kwenye damu vikawa juu na mwili ukawa na mafuta mengi hasa kama chapati hizo zinapikwa kwa mafuta mengi.

Ishara zitakazoashiria kuwa ulaji wa chapati unakuwa tatizo kiafya ni wapo unaongezea uzito bila sababu au unashindwa kupunguza uzito huo.

“Pia, iwapo unavimba tumbo au unapata maumivu ya baada ya kula, unahisi uchovu baada ya kula, au unatamani chapati kila mara hata kama huna njaa,” anasema Bi Wanza.

Zaidi ya hayo, dalili zingine ni pamoja na kutokula vyakula vingine kama mboga, protini au matunda badala yake unakula chapati tu.

Je, unaweza kula chapati ukizingatia afya njema?

Kwa mtu anayeona hawezi kuacha kula chapati kila siku, Bi Wanza anapendekeza kubadilisha unga mweupe na ule wa ngano usiosindikwa (whole grain) au nafaka zingine kama mtama, mahindi au viazi vitamu.

“Pili, punguza kiasi – badala ya chapati tatu, jaribu ule mbili tu na uongezee mboga na protini isiyo na mafuta kwenye mlo wako. Mwisho, kula kwa kuzingatia viashiria vya kushiba ili kuepuka kula kupita kiasi.”

Isitoshe, unaweza ukafurahia chapati yenye afya bora ikiwa utatumia unga wa ngano usiosindikwa, au kuongeza unga wenye viazi vitamu ili kupata vitamini A.

Pia, unaweza ukachanganya na mayai, maziwa au mboga kama karoti ili kuongeza protini na unyuzinyuzi.

Bi Wanza anashauri kupika bila mafuta mengi au kutumia kikaangio kisicho na mafuta au mafuta kidogo.

“Mwisho, unaweza ukatengeneza chapati ndogo ndogo ili kudhibiti kiasi unachokula.”