Jinsi ya kutambua dalili za polio kwa watoto na hatua za kuchukua
MARADHI ya polio yanayojulikana kama Poliomyeliti kwa lugha ya Kiingereza, ni ya kuambukiza, na husababishwa na virusi vinavyoingia mwilini kupitia mdomoni.
Ugonjwa huu ni hatari kwani, unaweza sababisha ulemavu na hata wakati mwingine kifo. Ishara za ugonjwa huu huanza kujitokeza kati ya siku tatu au tano baada ya maambukizi.
Asilimia 95 ya visa vya maambukizi ya virusi vya polio huwa na ishara nyepesi zisizo na madhara mengi, huku asilimia tano ya maambukizi yakiwa na ishara kali na hata kusababisha kupooza kwa sehemu fulani mwilini kama vile mikono na miguu.
Dalili
Kuna ishara myingi za maradhi haya na hivyo si kila mtu atakuwa na dalili sawa.
Aidha, dalili hizi hutegemea na aina ya polio
· Kuumwa na kichwa, kichefuchefu Kutapika,·maumivu mwilini, homa kali, uchovu, maumivu na kukazika kwa misuli, kutetemeka, udhaifu, au kufunga choo.
Ugonjwa huu husambaa vipi?
· Watu ambao hawajapaata chanjo dhidi ya maradhi haya au wenye kinga dhaifu mwilini, wanaweza ambukizwa na watu ambao wanapata chanjo kupitia njia ya mdomo.
· Kupitia vyakula na maji yaliyo na virusi hivi
· Ikiwa utagusa kinyesi cha mtu aliyeambukizwa. Hatari ya kuambukizwa ugonjwa huu huwa kubwa siku chache kabla na baada ya ishara kujitokeza.
Je, ugonjwa huu waweza kuepukwa?
. Polio yaweza zuiwa kwa kutoa chanjo kwa watoto wote wenye afya njema, kati ya umri wa wiki sita hadi miaka 18.
. Watu wanaoonyesha ishara hizi, wanapaswa kutengwa hadi uchunguzi wa kiafya ufanywe na kubaini iwapo ni ugonjwa huu.
. Wale ambao tayari wameambukizwa, hawafai kuzuru maeneo ya umma na maeneo yenye watu wengi
. Ikiwa mgonjwa anashuku kuambukizwa ugonjwa huu, awasiliane na mhudumu wa kiafya, ili kuwe na mpango wa kupata matibabu, bila kuhatarisha usalama wa wengine.