Afya na Jamii

Kinachosababisha magamba kichwani mwa watoto wachanga

Na WANGU KANURI February 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MWAKA jana, Linet Njeri, aliona kichwa cha mtoto wake kikiwa na ngozi laini iliyokuwa na magamba.

Mwanzoni, alidhani ni kwa sababu hakuwa anamuosha mwanawe vyema.

“Nilihisi nikune sehemu hiyo ya kichwa chake ili magamba hayo yaondoke lakini nikashauriwa na mamangu kuosha tu na kupaka mafuta mengi,” anakumbuka.

Baada ya muda, Bi Njeri anasema ngozi ya mtoto wake ilikuwa sawa.

Dkt Quek Meichi, daktari anayeshughulikia masuala ya ngozi kwa watoto katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha Aga Khan, anasema ‘cradle cap’, hali inayosababisha magamba kutokea kwenye ngozi husababishwa na kuzalishwa kwa mafuta kupita kiasi kwenye tezi za mafuta za mtoto.

“Panapokuwa na mafuta, fangasi mdogo anayefahamika kama Malassezia furfur, ambaye kwa kawaida huishi kwenye ngozi, huyatumia mafuta hayo kama chakula,” anaeleza.

Mafuta hayo yanapokuwa mengi sana, fangasi hao huzaana, na mtoto anapojikuna ni kutokana na uchafu wanaotoa fangasi hao.

Hali kadhalika, baadhi ya watoto hupata maeneo yanayoonekana meupe zaidi kwenye ngozi ya kichwa ambako fangasi huyu yupo kwa wingi, jambo linalofanya sehemu zilizoathirika kuonekana zaidi.

Unafaa kumuosha vipi mtoto wako?

‘Cradle cap’ inaweza kujitokeza mapema kuanzia wiki mbili baada ya kuzaliwa, lakini Dkt Meichi anasema wazazi wanapaswa kuangalia ukubwa wake, kama ni sehemu ndogo au imeenea kwenye ngozi yote ya kichwa.

Jeni pia inaweza kuathiri kiwango cha tezi za mafuta za mtoto kutoa mafuta.

“Kwa mfano, kama mama au baba ana mba kwenye masharubu au nyusi, basi mtoto anaweza kuwa nayo ‘cradle cap’ zaidi,” anasema.

Hata hivyo, hali hiyo si ugonjwa bali ni hatua ya kawaida wakati ngozi ya mtoto inapojirekebisha na kujifunza kudhibiti uzalishaji wa mafuta.

Ili kusafisha magamba hayo, Dkt Meichi anashauri mtoto kuoshwa angalau mara moja kwa siku kwa kutumia sabuni.

“Lowesha ngozi ya kichwa kwa mafuta mengi kwa dakika mbili hadi tatu, kisha sugua kwa brashi au kichanuo magamba yakianza kuinuka,” anasema.

Ikiwa eneo lililoathirika ni kubwa, zingatia utaratibu huu kila siku au kila baada ya siku moja hadi magamba yapungue.
Magamba yanaweza enea sehemu nyingine kando na kichwani?

‘Cradle cap’ wakati mwingine inaweza kuenea zaidi ya ngozi ya kichwa. Dkt Meichi anasema hali hii inaweza kuwa kutokana na kuzalishwa kwa mafuta mengi kupita kiasi, au kwa sababu mtoto amevalishwa nguo nyingi huku ngozi yake ikibaki na joto na yenye unyevunyevu, hali inayoruhusu fangasi kustawi.

Wakati mwingine, fangasi wanaweza kuchangia kutoka kwa nywele kwa sehemu mbalimbali. Matibabu ya magamba hayo hutegemea ukubwa wake na kama kuna dalili nyingine.

“Kama ni ya kawaida tu kwenye ngozi ya kichwa, na si zaidi ya sentimita tano kwa upana, na hakuna nywele zimepotea, na sehemu zingine za mwili zinaonekana sawa, basi unaweza kuendelea kufuata utaratibu niliorodhesha hapo awali nyumbani,” anasema.

“Lakini ukianza kuona kipande cha nywele kimepotea kichwani, au madoadoa ya kubadilika rangi usoni, kifuani au mwilini, basi tunahitaji kutibu.”

Magamba yanaweza kuibuka tena?

Ingawa ‘cradle cap’ haiambukizi, hali hiyo ikiwa imeenea, inaweza kuhitaji shampuu zenye dawa, dawa za kupaka, na wakati mwingine dawa za kumeza.

Dkt Meichi anaongeza kuwa ‘cradle cap’ inaweza kurudi hata baada ya matibabu, na jeni huwa sababu muhimu. Baadhi ya watoto wanaweza baadaye kupata ugonjwa unaofanya ngozi kuhisi mwasho, na kuparara (seborrhoeic dermatitis) wanapokuwa watu wazima, ambayo mara nyingi hujitokeza kama mba kichwani au ngozi inayopukutika kwenye nyusi au ndevu.

“Hatuwezi kufanya mengi kuhusu uzalishaji wa mafuta kwa sababu madhara yake yanazidi faida,” anasema.