Afya na Jamii

Kinachosababisha uke kuwasha siku kadhaa baada ya kushiriki tendo la ndoa

May 27th, 2024 1 min read

NA PAULINE ONGAJI

TATIZO la sehemu ya uke kuwasha siku kadhaa baada ya kushiriki tendo la ndoa hukumba wanawake wengi.

Kuna sababu kadha wa kadha ambazo husababisha haya. Kwanza, huenda mwasho huu unasababishwa na ukavu katika sehemu hii au msuguano mwingi.

Ikiwa basi hii ndio sababu, mwasho utatokomea baada ya siku kadhaa ikiwa utaepuka tendo la ndoa.

Ikiwa mwasho utaendelea, huenda tatizo hili linatokana na ukavu katika sehemu ya uke, shida ambayo yaweza kusababishwa na kukaukiwa kutokana na matumizi ya dawa za kihomoni, kwa sababu ya maradhi ya kisukari, au matumizi ya sabuni zilizo na harufu kali.

Pia, huenda hii ikatokana na mzio wa aina fulani ya kondomu au mafuta ya kulainisha uke wakati wa tendo la ndoa.

Mwasho pia waweza kutokana na maambukizi hasa iwapo utaambatana na harufu mbaya, au majimaji yasiyo ya kawaida.

Litakuwa jambo la busara kumuona daktari na ufanyiwe uchunguzi wa kimatibabu ili kubaini iwapo una maambukizi, na hivyo upate tiba.

Ikiwa kuna maambukizi, mwenzako pia atalazimika kutibiwa ili kuzuia maambukizi mapya.

Ikiwa uke wako haujalainika vilivyo au unakumbana na ukavu ukeni kutokanana sababu moja au nyingine, unaweza kutumia mafuta ya kulainisha uke wakati wa tendo la ndoa.