Afya na Jamii

Watafiti watoa matumaini mapya kwa wanawake wanaougua kichocho cha uzazi

Na PAULINE ONGAJI June 13th, 2025 Kusoma ni dakika: 4

KATIKA eneo la Msambweni, Kaunti ya Kwale, Bi Mwanaisha Abdalla, 35, anaendelea kupata nafuu baada ya kupokea matibabu kutokana na maradhi yaliyomsumbua kwa miongo miwili.

Tangu awe na miaka 15, Bi Abdalla aliugua Female Genital Schistosomiasis (FGS) au kwa Kiswahili kichocho cha uzazi, hali ambayo ilikuwa kitendawili kigumu hata kwa wahudumu wa afya na madaktari.

Alianza kugundua kwamba kila alipoenda haja ndogo, mkojo ulikuwa ukitoka ukiwa umeandamana na ute mweupe na damu. Dalili hizo zilizoanza akiwa msichana mdogo ziliendelea kuwa mbaya zaidi huku zikiambatana na maumivu makali wakati wa hedhi, na baada ya kuolewa, uchungu mwingi wakati wa tendo la ndoa.

“Sikujua ni nini,” anasema.

“Hata hospitali hazikujua. Walidhani ni ugonjwa wa zinaa na walinipa dawa ambazo hazikusaidia.”

Kichocho cha uzazi ni ugonjwa unaosababishwa na vimelea vya maji machafu vinavyojulikana kama Schistosoma haematobium.

Kulingana na Dkt Robinson Karuga, mtafiti mkuu wa LVCT Health Kenya, japo maradhi haya huwakumba pia wanaume, wanawake ndio huathirika zaidi.

“Hii ni kwa sababu wasichana na wanawake ndio hukumbwa na majukumu mengi ya nyumbani yanayohusisha kugusa maji. Kwa hivyo, wanapogusa maji machafu—hasa wakati wa shughuli za kila siku kama kuosha vyombo au kuchota maji—vimelea hivi huingia mwilini kupitia ngozi na kusafiri hadi kwenye viungo vya uzazi,”aeleza.

Ugonjwa huu huwakumba zaidi wasichana walio katika umri wa kubalehe, na unaweza kusababisha maumivu ya kudumu katika sehemu ya nyonga na hata kusababisha utasa. Kwa wanawake wa vijijini nchini Kenya—ambapo huduma bora za afya ni adimu—madhara yake ni makubwa zaidi.

“Kwa wanawake, hali hii husababisha vidonda katika sehemu za siri, maumivu wakati wa kukojoa, kutokwa na ute usio wa kawaida, na hata utasa. Dalili zake hufanana sana na za magonjwa ya zinaa au saratani ya lango la kizazi, jambo linalofanya iwe ngumu kwa maradhi haya kugundulika kwa urahisi,” aeleza Dkt Karuga.

Kwa Bi Abdalla, kwa zaidi ya miaka kumi, aliteseka kimya kimya, akijaribu kila aina ya dawa—zikiwa ni pamoja na zile za kienyeji—bila mafanikio.

Dalili zake zilikuwa mbaya zaidi kadri alivyoendelea kukomaa, na alipofika umri wa kuolewa, shida hii ilizidi kiwango cha kuathiri maisha yake ya ndoa.

Alikuwa anakumbwa sana na maumivu wakati wa hedhi na tendo la ndoa, kiwango cha kuwa wakati mmoja hangeweza kuvumilia kabisa. Hangeweza kumweleza mumewe, aliyedhani kuwa kila mara alikumbwa na maambukizi.

“Ndoa yangu ilikuwa karibu kuvunjika,” anakumbuka.

 “Mume wangu aliniletea dawa, lakini hakuna kilichosaidia.”

Hata hivyo, mwaka 2023, kila kitu kilibadilika. Kuna wakati ambapo wahudumu wa afya walipita kijijini na kutangaza kwamba kulikuwa na huduma ya kuwapima wasichana na wanawake bila malipo. Bi Abdalla alihudhuria mkutano huo na kutambua kuwa dalili zilizotajwa ni zile alizokuwa nazo.

“Nilipoenda kupimwa, haikuchukua hata dakika tano kugundua kuwa nilikuwa naugua kichocho cha uzazi,” asema.

“Nilikuwa na vidonda na nilikuwa nimeanza kupata uvimbe mdogo. Walianza matibabu papo hapo.”

Matibabu ya kwanza yalihusisha tembe sita za dawa ya praziquantelinayopendekezwa kwa schistosomiasis, na alianza kufuatiliwa kila mwezi. Kwa sasa, hali yake imeimarika kwa kiasi kikubwa, na leo hii, anasaidia wanawake wengine.

“Tayari nimewashawishi marafiki zangu wawili kupimwa—na wote walipatikana na maradhi haya na kutibiwa mapema,” aeleza.

Ingawa maradhi ya kichocho cha uzazi yamekithiri sana katika sehemu nyingi nchini, yamekuwa yakipuuzwa na kutofahamika kwa muda mrefu. Lakini utafiti unaoendelea sasa umeanza kuleta mwanga kuhusu ugonjwa huu, na hivyo kuwapa wanawake kama Bi Abdalla, matumaini mapya.

Dkt Karuga na timu yake wamefanya utafiti kwa zaidi ya miaka mitano katika kaunti za Kwale, Kilifi na Homa Bay—maeneo ambapo maradhi haya yamekithiri, na ambayo yanakumbwa na tatizo la huduma duni za afya.

Lengo kuu, Dkt Karuga asema, ni kushirikisha uchunguzi na matibabu ya kichocho cha uzazi  kwenye huduma za afya ya uzazi.

“Tuliwapima wanawake zaidi ya 2,200 na kugundua kwamba asilimia 35 ya waliohusika kwenye uchunguzi huu, walikuwa na maradhi haya. Hiyo ni idadi kubwa sana,” asema Dkt Karuga.

Matokeo ya utafiti huu yaliwasilishwa kwa maafisa wa afya wa kaunti na taifa, na tayari yameanza kubadilisha mipango ya afya na sera.

Kulingana na mtaalamu huyu, katika utafiti wao waligundua kwamba tatizo la wahudumu wengi wa afya hawakuwa na ufahamu kuhusu maradhi haya, na hivyo walishindwa kutofautisha  dalili za maradhi haya na magonjwa ya zinaa.

“Hii mara nyingi iliwasababisha kuwapa wagonjwa dawa zisizofaa. Lakini habari njema ni kwamba baada a mafunzo, waliweza kutambua maradhi haya na kuanza kutoa matibabu sahihi,” asema Dkt. Karuga.

Kufikia sasa, wahudumu zaidi ya 600 kutoka kaunti hizo tatu wamepokea mafunzo kuhusiana na maradhi ya kichocho cha uzazi, na jinsi ya kuyatibu.

Kulingana na wataalam wa masuala ya kiafya, maradhi haya ni tatizo kubwa kwa afya ya umma. Tafiti zinaonyesha kuwa wanawake wanaougua ugonjwa huu wanakumbwa na hatari mara nne zaidi ya kuambukizwa virusi vya HIV au virusi vya human papilloma virus HPV—vinavyosababisha kansa ya lango la kizazi.

Hata hivyo, takwimu kuhusu maradhi haya bado hazipo nchini Kenya na Afrika Mashariki kwa ujumla, na hazinakiliwi katika rekodi za hospitali, jambo linalozuia mipango bora ya afya.

“Ukosefu wa takwimu ni tatizo kubwa kwani hatuwezi kufanya mipango ya kutoa huduma za afya, kuwapa wahudumu mafunzo sahihi, au kujumuisha matibabu katika hospitali za umma.”

Kwa sasa, kutokana na jitihada za Dkt Karuga na timu yake, kaunti kama Kwale sasa zimeanza kujumuisha kichocho cha uzazi katika mipango ya afya ya uzazi. Hata hivyo, bado kuna changamoto hasa za ufahamu na kufikia matibabu.

Ndiposa wataalamu wanatoa wito kwa serikali kuanzisha huduma za kutoa tiba ya maradhi haya kitaifa, kuyajumuisha katika mafunzo ya kitabibu, na kuimarisha ukusanyaji wa takwimu hospitalini.

“Tukijumuisha uchunguzi wa kichocho cha uzazi katika ukaguzi wa afya wa kawaida, hasa kwa wanawake na wasichana, hatutatibu tu ugonjwa—tutazuia madhara ya muda mrefu kama saratani ya lango la uzazi na maambukizi ya virusi vya ukimwi VVU.”