• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 6:39 PM
AFYA: Ni muhimu kupumzika

AFYA: Ni muhimu kupumzika

Na MARGARET MAINA

[email protected]

KUTOKANA na mabadiliko ya mtindo wa maisha, watu wengi hawapati muda wa kutosha wa kupumzika.

Ni wazi kuwa wengi hawafahamu umuhimu wa kupumzika, ndiyo maana hawatengi muda wa kutosha wa kupumzika.

Ni ukweli kuwa kupumzika kuna manufaa makubwa sana kwenye miili na utendaji wetu wa kazi kila siku.

Huongeza uwezo wa kumbukumbu

Ubongo wa mwanadamu unahitaji kupumzika ili uweze kujijenga na kufanya kazi vyema. Ikiwa mtu hatapata muda wa kutosha wa kupumzika, uwezo wake wa kumbukumbu utapungua.

Huondoa hatari ya kupata kiharusi

Kiharusi ni ugonjwa unaosababishwa na kupasuka kwa mishipa midogo ya damu kwenye ubongo; hili husababisha damu kuvuja ndani ya ubongo.

Uchovu hasa ule unaoambatana na msongo wa mawazo unaweza kusababisha kupasuka kwa mishipa inayopeleka damu kwenye ubongo na kisha kusababisha ugonjwa wa kiharusi.

Hulinda afya ya moyo

Kupumzika kuna manufaa makubwa kuimarisha afya ya moyo wako. Ni wazi kuwa kasi ya usukumaji wa damu wakati wa kufanya shughuli mbalimbali ni tofauti na wakati unapokuwa umepumzika.

Hivyo basi, unapopata muda wa kupumzika unaupa moyo wako nafasi ya kupunguziwa mzigo wa kusukuma damu kwa kasi, ambao umeubeba wakati ulipokuwa unafanya shughuli mbalimbali.

Hutoa muda wa mwili kujijenga

Miili yetu inahitaji kujijenga kila mara hasa baada ya shughuli nyingi. Kwa njia ya kupumzika utaweza kuupa mwili wako nafasi nzuri ya kujijenga na kurejesha tena nguvu iliyotumika wakati wa shughuli mbalimbali.

Huimarisha misuli

Tunapopumzika misuli yetu inajijenga na kurudisha ute wake uliopotea wakati wa shughuli mbalimbali. Hivyo ni muhimu kuhakikisha kila baada ya kazi tunapata muda wa kutosha wa kupumzika ili tuboreshe afya za miili yetu.

Huondoa msongo wa mawazo

Chanzo kimojawapo cha msongo wa mawazo ni uchovu, na chanzo kimojawapo cha maradhi mbalimbali ni msongo wa mawazo.

Hivyo ni muhimu kuhakikisha tunapumzika ili akili na fikra zetu zijisafishe na kutuepusha na tatizo la msongo wa mawazo.

Hutuwezesha kula vizuri

Ni ukweli kuwa tukiwa tumechoka hatuwezi kula vizuri. Hivyo kupata muda mzuri na wakutosha wa kupumzika kutakuwezesha kula chakula vyema.

  • Tags

You can share this post!

AKILIMALI: Uuzaji samaki wawezesha mjane kujijengea ploti

Real Madrid yadidimiza matumaini ya Inter Milan kusonga...