AI inavyomsaidia kukuza stroberi zinazovutia masoko ya hadhi ya juu
AKIWA ndani ya kivungulio chake Mwihoko, Kaunti ya Kiambu, Anthony Ngatia anasimama kando ya mistari ya mimea ya stroberi akiwa na simu mkononi—si kwa mazungumzo, bali kuchanganua afya ya mimea yake kwa kutumia akili unde ndiyo kwa Kiingereza Artificial Intelligence (AI).
Kupitia teknolojia hiyo, anaweza kubaini dalili za magonjwa, upungufu wa virutubisho na hata viwango sahihi vya maji kwa haraka kabla ya tatizo kuenea.
Kisha ndipo anaanza kuvuna—akichagua kwa makini matunda yaliyoiva kikamilifu, tayari kwa soko la wateja wa hadhi ya juu.
Ni majira ya saa sita mchana, na licha ya joto linaloongezeka ndani ya kivungulio (greenhouse), mkulima huyu mwenye umri wa miaka 30 anaonekana kuwa na udhibiti kamili wa mazingira ya uzalishaji wake.
Matunda yake yanajitokeza kwa ubora; mekundu yaliyokolea, magumu yakiguswa na yenye umbo la kuvutia—sifa zinazowavutia wanunuzi wa masoko ya kifahari katika Kaunti za Kiambu, Nairobi na maeneo jirani.
“Hiki ndicho chanzo changu kikuu cha mapato. Na AI imenisaidia kuboresha uzalishaji na ubora wa mazao yangu,” Ngatia anasema.
Ngatia, ambaye ana shahada ya Uhandisi wa Umeme na Mawasiliano kutoka Chuo Kikuu cha Multimedia, anaunganisha taaluma yake na kilimo kwa njia ya kipekee.

Safari yake ya kulima stroberi ilianza miaka miwili iliyopita baada ya kufanya utafiti wa kina mtandaoni, hasa kupitia majukwaa ya kidijitali.
Alipokuwa akichambua mazao mbalimbali, aligundua kuwa stroberi zina uwezo mkubwa wa kuzalishwa mwaka mzima, tofauti na mazao mengine ya msimu kama pilipili hoho na mimea ya kunukia.
Kwa mtaji wa Sh60,000 kutoka akiba yake na msaada wa mama yake, alianza kilimo katika kipande cha ardhi cha thumni moja (1/8). Alianza na miche 300, lakini sasa ameongeza hadi 1,300 kupitia uzalishaji wake binafsi.
Teknolojia imekuwa kiini cha ukuaji wake. “Kupitia AI hupata mwongozo wa haraka kuhusu changamoto za mimea—kuanzia wadudu, magonjwa, hadi viwango vya joto na unyevunyevu,” anaelezea.
“Badala ya kusubiri mtaalamu aje shambani, ninaweza kupata ushauri papo hapo na kuchukua hatua mapema,” anaongeza, akibainisha kuwa hatua hiyo imepunguza gharama na kuongeza ufanisi.
Mbali na AI, anatumia pia maarifa yake ya uhandisi kutengeneza mifumo ya Mtandao wa Vitu (IoT) inayomwezesha kufuatilia hali ya udongo na kudhibiti umwagiliaji kwa njia ya kiotomatiki.
Kwa sasa, anatumia mfumo wa umwagiliaji wa matone (drip irrigation), akitegemea maji ya mvua, kisima na hifadhi ya tangi ili kuhakikisha mimea inapata kiwango sahihi cha maji kila wakati.

Kijana Ngatia hulima stroberi aina ya San Andreas, inayojulikana kwa uzalishaji wa mwaka mzima na matunda yenye ladha tamu na ubora wa juu—hali inayomuwezesha kuvutia wateja wa masoko ya hadhi ya juu.
Katika kuboresha udongo, anatumia mbinu za kilimo hai kama samadi, biochar na chokaa ya kilimo, pamoja na virutubisho vya majani na mfumo wa fertigation.
Licha ya mafanikio hayo, anakiri kuwa changamoto bado zipo, hasa upatikanaji wa wataalamu na udhibiti wa wadudu kwa njia rafiki kwa mazingira.
Aidha, mabadiliko ya tabianchi yalimsukuma kuhamia kwenye kilimo cha greenhouse baada ya mvua nyingi kusababisha kuenea kwa magonjwa ya mimea shambani.
Matokeo ya uwekezaji wake katika teknolojia yanaonekana wazi. “Uzalishaji umeongezeka kutoka kilo sita kwa mwezi hadi kati ya kilo 50 na 60, kutegemea hali ya hewa na ustawi wa mimea,” akaambia Akilimali Dijitali kwenye mahojiano ya kipekee.
Masoko yake sasa yamepanuka na kujumuisha maduka makubwa, mikahawa na wauzaji wa vyakula Nairobi na Kiambu, ambapo kilo moja ya stroberi huuzwa hadi Sh1,200.
Leo hii, mradi wake umebadilika kutoka jitihada za mtu mmoja hadi biashara inayotoa ajira, huku akiajiri mfanyakazi mmoja na kupanga kupanua zaidi uzalishaji wake—akiongozwa na nguvu ya teknolojia ya kisasa. Isitoshe, sasa anatoa huduma kupitia kampuni yake inayojulikana kama Sunberry Farm .