Makala

Ajabu aliyekuwa kamishna wa IEBC akitapeliwa Sh6 milioni na mganga akisaka kazi

Na DOMNIC OMBOK May 31st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA kamishna wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), Bi Margaret Wanjala Mwachanya, amewasilisha kesi mahakamani baada ya kupoteza zaidi ya Sh6 milioni kwa mganga wa kienyeji aliyemuahidi kazi ya hadhi ya juu kwa njia za “kiroho”.

Kesi hiyo ya kushtua iliwasilishwa katika mahakama ya Vihiga ambapo Bi Mwachanya, ambaye pia aliwahi kuwa Naibu Balozi wa Kenya nchini Pakistan, alieleza kwa majonzi jinsi alivyotapeliwa kupitia tangazo la ajabu alilopata kwenye simu yake mapema mwaka 2024.

“Mara kwa mara tangazo hilo lilikuwa likijitokeza likisema kuna nafasi za kazi. Niliamua kupiga namba hiyo,” alieleza mahakamani.

Huo ulikuwa mwanzo wa safari ya majonzi iliyoanzia na kulipa ada ya ushauri ya Sh3,000 na baadaye akanunua dawa ya mitishamba ya Sh12,500. Lakini haikukoma hapo.

Wiki moja baadaye, mganga huyo alimwambia ataje umri wake. Aliposema ana miaka 53, aliambiwa aongeze sufuri nne, kisha atoe Sh530,000 kwa ajili ya tambiko. Alikabidhi pesa hizo kwa kijana aliyedaiwa kuwa mwana wa mganga huyo, na pesa hizo zikawekwa kwenye sanduku na kufungwa kitambaa. Alielekezwa kuomba kwa siku 21.

“Baada ya kufungua sanduku hilo, pesa zote zilikuwa zimepotea,” alisema kwa mshangao.

Mganga alimtuliza kwa kumwambia “pesa zilikuwa salama”. Lakini kabla ya siku 21 kuisha, aliombwa tena Sh380,000 kwa tambiko la pili, ambapo sanduku lililotumika lilitupwa mtoni.

Baadaye, aliitwa kwenye duka lenye mwangaza hafifu magharibi mwa Kenya. Hakuwahi kumuona mganga usoni kwani alikuwa akizungumza kutoka nyuma ya pazia akizungukwa na mishumaa.

“Niliposema nilikuwa na Sh1,000 pekee, aliniambia niziweke kwenye sanduku la mbao,” alisema.

Baada ya kutamka maneno ya ajabu, msaidizi wake aliinua sanduku juu ya kichwa chake. Lilipofunguliwa, lilionekana kujaa pesa.

“Niliambiwa ni pesa nilizopoteza tangu kuzaliwa, Sh18.3 milioni. Ili nizipate, nilitakiwa kutoa Sh1.8 milioni nyingine,” alisema.

Alitii tena na kuweka pesa hizo katika sanduku hilo. Tena akaambiwa asilifungue kwa siku 21. Lakini kabla ya muda huo kuisha, mganga alimpigia simu na kumtambulisha kwa wazee wawili.

“Wazee hao waliniita ‘mwanamke wa chuma’ na kudai pesa zangu sasa ziliongezeka hadi Sh48 milioni,” alieleza.

Hili likawa tangazo la kutakiwa kutoa Sh3.33 milioni zaidi ili “kuondoa vizuizi vya mwisho.” Hakuishia hapo – aliambiwa atume Sh75,000 kwa mtu aliyesafiri Tanzania kufanya tambiko la mwisho. Alitii tena.

Hatimaye, alialikwa kwa tambiko la mwisho na kuagizwa atie sanduku lake kwenye moto. Alitekeleza hilo kwa imani kuwa utajiri wake ungetumwa benki.

“Lakini nilipoomba nisubiri ili kuthibitisha, nilipewa vitisho. Mganga aliniambia nikimbie niokoe maisha yangu,” alisema kwa huzuni.

Kwa sasa, baada ya kupoteza zaidi ya Sh6 milioni, Bi Mwachanya ameamua kutafuta haki kupitia mahakama. Kesi hiyo itaendelea kusikizwa mnamo Julai 7, 2025.