Akili Mali

Akili Mali: Siri ya kuwa milionea kwa kukuza vitunguu

Na SAMMY WAWERU April 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VITUNGUU ni kati ya mimea inayochukua muda mfupi kukomaa inayokuzwa na wakulima wengi nchini hasa wenye chanzo cha maji, japo hawajaweza kuziba pengo la uzalishaji.

Hilo, linalazimu wafanyabiashara kuagiza kutoka nje hususan nchi jirani ya Tanzania.

Mtaalamu Mishack Wachira kutoka Farm Rescue Agri Ventures Ltd, anaeleza kuwa kilimo cha vitunguu nchini Kenya kimekua kwa kasi na kuwa miongoni mwa biashara zenye matumaini makubwa kwa wakulima.

Kwa miaka ya hivi karibuni, wakulima wengi wameanza kutumia mbegu za kisasa (hybrid), hatua ambayo imeongeza uzalishaji, ubora na ushindani wa vitunguu vya Kenya katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Kupitia mafunzo ya kilimo, maonyesho na uboreshaji wa ujuzi katika vitalu, matumizi ya mbolea na udhibiti wa magonjwa, wakulima wameendelea kuimarisha uzalishaji wao.

“Licha ya ongezeko la uzalishaji wa ndani kwa ndani, bado soko la vitunguu linaongozwa na kiwango cha mahitaji na usambazaji,” Wachira anasema.

Wakati uzalishaji unapopungua, nchi huagiza vitunguu kutoka nje, lakini wakati wa ziada, Kenya pia huuza katika nchi jirani, jambo ambalo mtaalamu huyu anaamini likitiliwa mkazo litaletea taifa mapato tele.

Hata hivyo, Wachira anaona kilimo cha vitunguu kama fursa kubwa kwa vijana, kwani kinahitaji mtaji wa wastani na kina soko lenye ushindani mkuu mwaka mzima, kutokana na matumizi yake katika kila boma na familia, hoteli na viwanda vya chakula.

“Mtu anaweza kuwa milionea kupitia kilimo cha vitunguu iwapo kitafanywa kwa weledi na kwa utaalamu,” anaelezea.
Kuwa milionea kupitia kilimo cha vitunguu? Haya basi vipi?

Anajibu akitoa ufafanuzi, “Kilo moja ya mbegu zilizoboreshwa (hybrid) inaweza kupandwa kwenye ekari moja, ambayo inaweza kutoa tani 18 hadi 25 za vitunguu chini ya usimamizi mzuri. Gharama ya uzalishaji kwa ekari ni karibu Sh150,000. Ikiwa mkulima atavuna tani 20 na kuuza kwa Sh50 kwa kilo, atapata Sh1 milioni, na baada ya kutoa gharama, atabaki na faida ya karibu Sh850,000.”

Endapo atauza wakati uhaba unashuhudiwa kwa Sh120 kwa kilo, mapato yanaweza kugonga Sh2.4 milioni, na faida ya zaidi ya Sh2 milioni.

Ili kuafikia mafanikio hayo, mkulima anapaswa kuzingatia mbinu bora za kilimo kama vile kutumia mbegu bora, kuandaa kitalu vizuri, kupanda kwenye nafasi sahihi, kuweka mbolea kulingana na hali ya udongo, kudhibiti wadudu na magonjwa, pamoja na umwagiliaji wa maji ya kutosha.

Uvunaji kwa wakati ufaao na uhifadhi sahihi, Wachira anasema pia huongeza ubora na kurefusha muda wa kuhifadhi vitunguu.

Hata hivyo, changamoto kama mabadiliko ya tabianchi yanayosababisha ukame na magonjwa, bei zisizotabirika na kupunjwa na madalali bado zinaathiri wakulima.

Kukabiliana na hali hii, matumizi ya teknolojia kama vile umwagiliaji wa maji kwa njia ya matone, upimaji wa udongo kujua kiwango cha asidi, alkali na virutubisho, pamoja na suluhisho za kuhifadhi unyevunyevu kama Reon yamekuwa yenye manufaa makubwa.

Teknolojia hizi, Wachira anasema husaidia kuongeza kiwango cha uzalishaji na kupunguza hatari za hasara.

Aidha, kuchakata au kuongeza thamani ya vitunguu kwa kuvikausha au kutengeneza unga wake kunafungua masoko mapya na kuongeza faida.

Wachira anasisitiza kuwa ushirikiano wa wakulima kupitia vyama vya ushirika ni muhimu ili kupata masoko bora, mikopo nafuu na nguvu ya kujadiliana bei.

Kupitia mikakati hii, kilimo cha vitunguu kinaweza kuwa njia bora kujikwamua kiuchumi na hata kuwa milionea.