Jinsi anavyounda jemu ya stroberi
SIRI ya kilimo ipo katika uchakataji wa mazao, hii ndiyo kauli ya Jimmy Aluvisia.
Kitaaluma, barobaro huyu amesomea Shahada ya Usimamizi wa Biashara ya Kilimo na kiutendakazi ni mkulima na mshirika wa uongezaji bidhaa za shambani thamani.
Mwaka 2020, alipokuwa katika mwaka wake wa nne katika Chuo Kikuu cha Great Lakes, Kisumu, Aluvisia alifanya uamuzi ambao umebadilisha kabisa mwelekeo wa maisha yake kitaaluma na kibiashara.
Kilichoanza kama mradi mdogo wa mwanafunzi kutafiti na kutatua changamoto za kilimo, leo hii kimekua na kuwa biashara imara ya usambazaji wa stroberi na uchakataji jamu inayosambazwa kwenye maduka ya kijumla, hoteli na maduka ya kuoka keki katika kaunti kadhaa nchini.
Mjasiriamali huyu kutoka Kakamega, anakumbuka kana kwamba ilikuwa jana tu wazo hilo lilianza wakati wa mafunzo katika Shirika la Ukaguzi wa Afya ya Mimea Kenya (KEPHIS).
Aluvisia, kwenye mahojiano na Akilimali, alisema akiwa huko, alihusika katika shughuli za uzalishaji wa miche, jambo lililomfumbua macho kuhusu pengo lililokuwepo katika uzalishaji wa stroberi.
“Nikiwa KEPHIS niligundua kuwa stroberi ni tunda lenye thamani kubwa sokoni, lakini wakulima wachache sana nchini hulima zao hilo,” anasema.
Anaongeza kuwa mahitaji yapo, lakini changamoto kubwa ni upatikanaji wa miche bora na yenye ustahimilivu wa hali ya hewa haswa athari za mabadiliko ya tabianchi.
Anasimulia kwamba alianza na kitalu kidogo mara tu aliporejea chuoni. Lengo lake lilikuwa kuzalisha miche safi ya stroberi, iliyoafikia ubora, kuziba pengo alilotambua akiwa KEPHIS na kuisambaza kwa wakulima maeneo ya Nyanza na Magharibi mwa Kenya.
“Huduma nilizotoa zilipata umaarufu kwa haraka,” anadokeza.
Isitoshe, alishirikiana pia na mashirika yasiyo ya kiserikali yanayopiga jeki wakulima.
Hata hivyo, aligundua kuwa biashara hiyo ilitegemea sana msimu wa mvua.
Mahitaji ya miche yaliongezeka wakati wa mvua na kushuka wakati wa kiangazi na ukame, hali iliyomwacha bila mapato ya kutegemewa.
“Changamoto hiyo ilinisukuma kwenye harakati za uchakataji stroberi,” Aluvisia anasema.
Hapo ndipo Aluvision Farm Enterprise ilipozaliwa. Ni biashara iliyosajiliwa rasmi inayojihusisha na usambazaji wa stroberi na utengenezaji wa jemu ya matunda hayo.
Kwa sasa, anashirikiana na wakulima watano wa kandarasi kutoka eneo la Kati na Bonde la Ufa wanaomsambazia stroberi kila wiki.
Matunda huratibiwa kwa madaraja, ambapo daraja la kwanza huenda sokoni na la pili huchakatwa kuwa jamu.
Anafichua kwamba kampuni yake husambaza zaidi ya kilo 600 za stroberi kila mwezi kwa zaidi ya maduka 25 ya jumla nchini.
Alianza kuchakata jemu mwaka 2023 baada ya kuhudhuria maonyesho ya biashara ya kilimo.
Kutoka kilo 20 kwa mwezi, sasa huzalisha zaidi ya kilo 200 za jemu.
Kilo ya jemu huuza Sh1,000, ikiwa katika aina tatu: yenye sukari, isiyo na sukari na ya asili inayotumia asali kama kiungo cha kuongeza utamu.
Anasema kuongeza thamani hurefusha muda wa kuhifadhi bidhaa, hatua inayomuwezesha kusaka bei bora hivyo kuunda faida nono.
Ameandikisha ukuaji kwani sasa ameajiri mtaalamu wa sayansi ya chakula kusimamia viwango vya ubora, huku akipata mafunzo kutoka Taasisi ya Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Kenya (KIRDI).
Licha ya changamoto za mtaji kupanua biashara yake na ucheleweshaji wa malipo kutoka kwa maduka makubwa, Aluvisia ameendelea kujikakamua, akisisitiza umuhimu wa uchakataji katika sekta pana ya kilimo.