Jinsi konokono huzalisha bidhaa zinazowaniwa katika maduka ya urembo
KONOKONO wameibuka kuwa viumbe ambao wanaweza kumpatia mkulima kipato kizuri.
Teknolojia inapoendelea kukua, mengi yanaendelea kuvumbuliwa, ambayo ni pamoja na bidhaa zitokanazo na konokono.
Hii imefanya ufugaji wake kuwa njia mbadala ya kujipatia mapato mbali na kutegemea ufugaji wa kawaida kama wa ng’ombe, mbuzi au kondoo.
Sekta hii inaweza kuwa msaada mkubwa katika juhudi za kubuni nafasi za ajira, iwapo itapiga jeki kwa rasilmali.
Juhudi hizo zinaweza kusaidia uundaji wa aina nyingi za bidhaa kutokana na viumbe hawa ambao watu wengi wanawachulia kuwa kero.
“Kwa mfano bidhaa za urembo kama vile sabuni na manukato ya bei ghali kwa ajili ya matumizi mbalimbali,” asema Dkt Paul Kinoti.
Dkt Kinoti ambaye ni mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo na Teknolojia cha Jomo Kenyatta (JKUAT), anasema huu ni mradi ambao ulianzishwa rasmi na chuo hicho mnamo 2019.
Anasema konokono wanafaa kufugwa katika sehemu maalum iliyotengwa ili waweze kuzaana kwa wingi.
“Chuo kiliamua kujikita kwenye uongezeaji wa thamani kwa bidhaa zinazotokana na konokono kwa sababu matumizi ya konokono kwa jamii nyingi za Kiafrika sio mengi. Hii ndio sababu ya kuanzisha teknolojia ambayo ingechakata konokono kwa ajili ya kutengeneza mbolea,manukato na sabuni.”
Kupitia usaidizi wa chuo, walipata mtaji ambao ulitumika kufanikisha shughuli yenyewe na sasa bidhaa zao zimeidhinishwa kwa ajili ya matumizi.
Anasema inahitaji juhudi, bidii na utafiti wa kina kujikita kwenye mradi kama huu ambao mara nyingi unalenga kutimiza mahitaji ya soko kwa kutumia uvumbuzi.
Kulingana na Dkt Kinoti, ni jambo la kimsingi kwa taasisi za kiufundi na vyuo vikuu kuwekeza kwenye teknolojia ambazo zinalenga kupiga jeki shughuli za kilimo.
Anasema ili kuanzisha mradi, walihitaji sehemu maalum ya kuwafugia konokono ambayo ni mbali na makazi ya watu ili kutoa mazingira sahihi ya ukuaji.
Kisha wakatafuta jinsi ya kuwapata viumbe hawa kwa ajili ya kuzaana.
Anashauri kwamba ili kuwekeza kwenye mradi huu, mkulima anatakiwa kupata kibali kutoka kwa idara husika ambayo inashughulika na wanyamapori.
Aidha, leseni yenyewe huratibu sio tu sehemu ya kufugia, bali pia mtindo wa kuwakuza na kuwalea.
Katika sehemu maalum ya kuwafugia, viumbe hawa hufanya vyema endapo mkulima atahakikisha wanapata lishe ya kutosha ambayo aghalabu ni mabaki ya mimea.
Kwa upande mwingine Dkt Kinoti anawasaidia wakulima kuwekeza kwenye mradi huu na hatimaye huwanunua kwa ajili ya kuwaongezea thamani.
Anasema bidha ya majimaji inayofahamika kama slime inayotokana na konokono hununuliwa kwa zaidi ya Sh1,400 kwa lita moja.
“Ni shughuli ambayo ni nyepesi kufanya kwa sababu wakulima wengi wamepokea mafunzo namna ya kukamua utomvu wenyewe.”
Bidhaa hizi zinapatikana kwa wingi kwenye maduka ya kijumla nchini na pia miongoni mwa maduka yanayopatikana kwenye chuo kikuu.
Wakulima wengi ambao wameonyesha ari ya kujitosa kwenye mradi huu wanatoka kaunti za Embu, Kiambu, Nairobi na Kirinyaga.
Anasema changamoto kubwa ni jinsi ya kuwahifadhi konokono kwa sababu inahitaji vyombo vya kisasa kama vile majokofu ambayo hutumia kiwango kikubwa cha umeme.
Miaka kadhaa kutoka sasa anaona Wakenya wengi wakikumbatia matumizi ya bidhaa zinazotokana na konokono.
Bidhaa hizo zinasifiwa kwa kusaidia kuimarisha afya ya ngozi miongoni mwa faida nyingine.