Nyasi ya ‘juncao’ inayokomaa upesi yaibuka kimbilio kwa wenye mifugo
WAKULIMA nchini wamelazimika kubadili mbinu zao za kilimo na kukumbatia teknolojia zinazostahimili athari za mabadiliko ya tabianchi, kuanzia ukame wa muda mrefu, mafuriko hadi wadudu na magonjwa yanayoharibu mazao.
Kwa Abdirahman Ali Hassan, mfugaji kutoka Kaunti ya Wajir, ukame unapotajwa humkumbusha hasara aliyokadiria miaka minne iliyopita.
Hassan ambaye pia ni mwalimu, aliachwa akikadiria hasara kubwa kutokana na ukame wa 2021–2022, alipopoteza mifugo yenye thamani ya mamilioni ya pesa.
Kaunti ya Wajir, mojawapo ya kaunti kame nchini (ASAL), wakazi ambao hutegemea ufugaji kujiendeleza kimaisha na mbinu za zamani kulisha mifugo wao, haikusazwa na ukame.
Hassan anafichua kwamba alipoteza zaidi ya ng’ombe 100 na ngamia wapatao 60.
“Hasara haikuwa ya kiuchumi pekee, bali pia ya kibinafsi,” anakumbuka. “Ilikuwa huzuni kubwa. Kila siku unaamka kuhesabu hasara ya wanyama waliofariki.”
Wizara ya Kilimo na Maendeleo ya Mifugo inakadiria kuwa zaidi ya wanyama milioni 2.5 walipotea, wenye thamani ya mabilioni ya pesa. Malisho yalikauka, na vyanzo vya maji vikapungua.
Hali hiyo ilimlazimu Hassan kutafuta suluhisho la kudumu.
Mwaka 2023 alitembelea mradi mmoja wa mifugo Malindi na kushuhudia ufugaji wa kisasa wa ng’ombe wa maziwa unaotegemea malisho yaliyopandwa.
Hapo ndipo alipokutana na nyasi maalum inayojulikana kama Juncao, ambayo hukomaa upesi na yenye asili yake China.
“Niliona walivyokuwa na malisho ya kijani hata wakati wa ukame. Nikajua lazima nibadilishe mbinu zangu za ufugaji,” anasema.
Alianza kwa ekari moja, ambapo alitoa mbegu za upanzi kutoka Nakuru. Juncao, mbegu yake ni vipande vya matawi ya nyasi hiyo.
Leo hii, Hassan ana ekari 10 za malisho hayo, pamoja na nyasi ya Brachiaria na viazi vitamu, hatua ambayo imemsaidia kupiga jeki mradi wake wa ufugaji.
Hali kadhalika, amewekeza kwenye mashine za kukatakata majani na kuongeza thamani kama chaff cutter, pelletizer na hay baler, pamoja na maghala mawili ya sileji yenye uwezo wa kuweka akiba ya tani 90 kila moja.
Wakati wa kiangazi cha mwaka huu, wakulima wenza wakiteseka kutafutia mifugo wao chakula, wake hawakuhangaika kupata malisho.
“Niliuza malisho ya ziada na kupata karibu Sh1.7 milioni,” anasema.
Sasa shamba lake ni uga wa mafunzo kwa wakulima wengine. Wajir, jamii zinazoishi humo ni zile za kuhamahama kutafutia mifugo chakula.
Isitoshe, Hassan amepunguza kiwango cha mifugo na kukumbatia ng’ombe walioboreshwa wa maziwa – chotara wa Sahiwal wanaotoa lita 14 hadi 16 za maziwa kwa siku.
Kwingineko jijini Nairobi, Kevin Mwangi Kamau anatumia nyasi ya Juncao kwa njia tofauti – ukuzaji wa uyoga.
Baada ya kupoteza kazi wakati wa Covid-19 mwaka 2021, alianza na mtaji wa Sh15,000 pekee kukuza zao hilo la familia ya fungi.
Awali, Kevin alikuwa akitumia majani ya ngano na kuzalisha kilo 100 pekee za uyoga kila baada ya wiki mbili.
Leo hii, kwa kutumia Juncao, huzalisha hadi kilo 2,000 za uyoga aina ya oyster na kilo 800 za button kila mwezi.
“Juncao inasaidia uyoga kukua haraka,” anasema. Biashara yake pia imeajiri hadi watu 10, wengi wao wanawake.
Asili ya Juncao ni China, ilikobuniwa na Profesa Lin Dongmei Zhanxi wa Fujian Agriculture and Forestry University.
Prof Lin kwenye mahojiano Jijini Nairobi na Akilimali, alitaja teknolojia ya Juncao kama ‘mwokozi’ kwa wakulima na wafugaji haswa kipindi hiki ulimwengu unalemewa na athari za tabianchi.
“Mbali na kuwa chakula cha mifugo na kulima uyoga, hutumika pia kuhifadhi mazingira, kudhibiti mafuriko na uzalishaji wa nishati inayotokana na majani,” Prof Lin akasema, akiainisha tija za nyasi hii maalum.
Serikali ya Kenya kwa ushirikiano na shirika la Umoja wa Mataifa la masuala ya uchumi – United Nations Department of Economic and Social Affairs (UNDESA), inahamasisha ukumbatiaji na ukuzaji wa nyasi ya ‘Juncao’ kupitia mradi wa kutekeleza malengo endelevu ya kuinua jamii.