Akili Mali

Tabibu mstaafu aliyejitosa katika kilimo cha ‘yacon’

Na JOHN NJOROGE April 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 3

DAVID Njoroge alipostaafu kama daktari wa mifupa mwaka wa 2023 baada ya kufanya kazi kwa miaka 30, hakuanzisha kliniki kama vile wengi wa madaktari wenzake wangeamua kufanya.

Yeye aliamua kujitosa katika kilimo mseto katika shamba lake la Ribot mjini Elburgon, Kaunti ya Nakuru ambapo alifuga kondoo, ng’ombe na kuku.

Tulipofika katika shamba lake hivi majuzi, Dkt Njoroge alisema baada ya muda, alianza ukulima wa matunda ya yacon katika sehemu moja ya shamba lake.

Dkt David Njoroge akishikilia mizizi ya yacon ambayo yamkini huliwa mbichi, kilo moja ikiuzwa Sh200. PICHA|JOHN NJOROGE

“Nilisoma makala katika chapisho la “Daily Nation” ambapo mkulima alikuwa akilima na kutangaza mizizi yake ya yacon mtandaoni. Kwa vile nilivutiwa na matunda hayo, nilijadiliana naye kuhusu bei na tukakubaliana Sh500 kwa kila kipande,” anasema Dkt Njoroge, akiongeza kuwa alinunua mizizi mitatu ya yacon ambayo aliipokea mara tu baada ya kulipa.

Kwa Sh6,000 alizokuwa nazo kama mtaji, mkulima huyu alitayarisha sehemu ya shamba lake alilopangia kupanda mmea wake mpya.

Alichimba mashimo yenye kina cha futi 3 na kuweka nafasi ya mita 3 kwa upana wa mita 6 ili kuwezesha mizizi ya yacon kuenea na kuifanya izae mizizi zaidi ambayo hutoa matunda.

Baadaye, alimwaga mbolea kutoka kwa mifugo wake na kupanda kabichi kwenye nafasi ya kati.

Mkulima anasema kuwa mazao ya yacon yanahitaji mvua ya wastani.

“Zao hili hustawi katika udongo wenye maji mengi, hasa wakati wa mvua. Kwa wakati wa kiangazi, mimi humwagilia mizizi yangu kila wiki nikitumia maji ya mvua ninayohifadhi kwenye matangi makubwa yaliyoko hapa shambani,” anasema Dkt Njoroge, akiongeza kuwa aliendelea kuyatunza mazao yake kwa kupalilia na kutumia mbolea zaidi ili kuongeza ukuaji na uzalishaji wa mimea yake.

Kukabili wadudu

Anaeleza kuwa zao hilo hushambuliwa na vidukari weupe hasa wakati wa kiangazi. Hapa, anatumia dawa za wadudu ili kudhibiti na kuangamiza wadudu hao.

Anasema kwamba mimea ya yacon huchanua maua baada ya miezi sita, ambayo ni ishara ya kukomaa na tayari kuvunwa.”

“Mmea mmoja wa yacon kwenye mzizi mmoja unaweza kuwa na uzito wa hadi kilo 1.5 na kutoa kati ya mizizi 10 na 15 (matunda) kwa wastani wa kati ya kilo 15 na 20 kwa kila mmea. Baada ya kuvuna, mizizi huanza kuchipuka tena ili kutoa matunda mengine,” anaeleza.

“Wakati wa mavuno yangu ya kwanza ya matunda ya yacon, nilivuna kilo 45 kutoka kwa mizizi mitatu niliyopanda na kuiuza kwa Sh350 kwa kilo katika soko la ndani. Kwa kuwa aina hii ya ukulima ni geni hata sokoni, kwa sasa, mimi huuza matunda yangu kwa Sh200 kwa kilo,” anasema akiongeza kuwa soko ndilo changamoto kubwa kwake kwa sababu wakulima katika eneo hilo hawajafahamu kilimo cha yacon.

Anawaomba wakulima kukumbatia kilimo hiki kwa kuwa hakihitaji nguvu wala kazi nyingi na kinaweza kufanywa hata kwenye eneo ndogo la shamba.

Pia anahimiza serikali ya Kaunti kuwawezesha na kuwahamasisha wakulima kuhusu kilimo cha yacon na kutafuta soko bora kwa wakulima wadogo kwani matunda hayo yakipandwa kwa wingi, soko linaweza kuwa nzuri na rahisi kuwafikia wateja wengi.

Kwa vile wakulima wengi hawajui kuhusu ukulima huu wa yacon au jinsi ya kuikuza, idadi ya wateja wanaomtembelea shambani ni wachache na hii inafanya mauzo kupungua licha ya maelfu ya mizizi ambayo imeongezeka kwake shambani kwa muda wa miaka mitatu iliyopita tangu aanze kukuza matunda haya.

Mikakati yake

Dkt Njoroge ambaye ana shauku kubwa kupitia kilimo, anaeleza kuwa alitaka kufanya shahada katika kilimo lakini ilibidi asomee udaktari kwani ilikuwa rahisi kupatikana kwa wakati huo.

Mpango wake wa siku sijazo ni kufanya kilimo cha yacon kwa kiwango kikubwa katika ekari 10 za ardhi yake, kuunda ajira kwa vijana, kuwa na uzalishaji bora na kuuza matunda yake katika masoko ya humu nchini na kimataifa.

Kwa ajili ya kupata maarifa zaidi, mkulima huyu huwatembelea wakulima walioimarika ambao wamefanikiwa kulima kupitia nyanja tofauti.

Pia, huenda kwenye semina na kuwasiliana na maafisa kutoka idara za kilimo na kusoma makala za kilimo kwenye magazeti ili kuboresha ujuzi wake.

Kutoka kwa mashirika husika ya kilimo, pia amejifunza kuhusu usimamizi wa mazao, magonjwa na udhibiti wa wadudu.

Wataalamu wa lishe wanaangazia faida za mizizi ya yacon au matunda kamakatika umeng’enyaji chakula, kudhibiti uzani naa kuimarisha sukari ya damu na kuifanya iwe bora kwa wagonjwa wa kisukari au wale wanaotaka kudhibiti viwango vya sukari.

Uchunguzi unaonyesha kuwa nyuzinyuzi katika yacon huboresha ufyonzaji wa madini kama kalsiamu, ambayo ni muhimu kwa kudumisha mifupa.

“Ina virutubishi vingi, potasiamu nyingi, ni tamu na kwa mara nyingi huliwa ikiwa mbichi huku majani yakitumika kwa chai au kama mboga,” utafiti unaonyesha.

Profesa Hillary Bett, afisa wa usimamizi wa kilimo biashara katika Chuo Kikuu cha Egerton mjini Njoro, Kaunti ya Nakuru, anasema wakulima wanahitaji kufanya upimaji wa udongo na kufanya ukulima wa mzunguko kwa mazao yao ili kuongeza uzalishaji.

“Wakulima wanapopima udongo kabla ya kupanda, wataweza kujua aina ya mbolea ya kutumia na mazao ya kupanda katika mashamba yao,” anasema Prof Bett.