‘Ukijituma kisawasawa, kuvuna Sh1 milioni kwenye kilimo cha ‘nduma’ ni kazi rahisi’
KATIKA miaka ya hapo nyuma, Jared Ombati Mogere allikuwa akiishi jijini Nairobi ambapo alikuwa akijishughulisha na biashara ndogo ndogo.
Hata hivyo, mnamo 2021, aliugua na kuishia kutumia kiasi kikubwa cha pesa alizokuwa ameweka kwenye akiba.
Kwa bahati nzuri, Ombati ambaye pia ni mhubiri, alipata nafuu lakini alikuwa ametumia kiasi kikubwa cha fedha zake na hivyo basi akaamua kuwa hataendelea kuishi jijini.
Alifanya uamuzi wa kurudi nyumbani kwao Kisii akajishughulishe na maisha ya mashambani kwani kwa kiwango fulani, maisha humo si ghali namna yalivyo mijini.
Alipofika Kisii, Ombati alikuwa amekata kauli kuwa atajihusisha na kilimo cha nduma au majimbi kujiendeleza.
Mhubiri huyo alidokeza kuwa alipokuwa jijini, aliona jinsi nduma chache zilikuwa zikiuzwa kwa bei ghali na alipofika tu kijijini, alisema kilimo hicho ndichokitakachomuokoa.
“Nikiwa jijini Nairobi, niliona watu wakinunua nduma chache tu kwa pesa nyingi. Wafanyabiashara walikuwa wakivuna vinono kutoka kwa biashara hiyo na hivyo basi nilivutiwa na hilo na nikasema nitazamia kilimo hicho na kuzalisha nduma kwa wingi,” Ombati aliambia Akilimali ilipomzuru shambani kwake katika kijiji cha Nyambunde, eneobunge la Bobasi.
Mkulima huyu anamiliki zaidi ya mimea 200,000 ya nduma katika shamba lake dogo na mengine ambayo ameyakodisha kijijini kwao, katikati ya eneo la Itumbe na Igare.
“Ukulima wa nduma ni kama biashara ya dhahabu kwangu. Una pesa sana na ninawahimiza wale ambao bado wanawaza kuhusu kilimo chenye faida ambacho wanaweza kukifanya, wajaribu nduma,” Ombati anaongeza.
Anahoji kuwa ukulima wa nduma unaweza kumvusha mtu kutoka kiwango kimoja hadi kingine katika maisha iwapo atatia bidii na kutokufa moyo kwa changamoto atakazokumbana nazo.
Kulingana na mjasiriamali huyu, nduma hufanya vyema katika ardhi yenye unyevunyevu na iliyo na kiasi fulani cha kutosha.
Ndiyo maana anafanya kilimo chake karibu na fuo za Mto Kuja kwa shamba zaidi ya ekari mbili.
“Ardhi nyingi zenye unyevunyevu katika eneo la Gusii mara nyingi huachwa bure au hupandwa miti ya mikalatusi. Miti hiyo huchukua muda hadi wa miaka mitano ndiposa ikomae na kuuzwa lakini nduma huchukua miezi minane hadi mwaka mmoja kunawiri. Kwangu, nilikwenda kinyume na wakazi wengine ambao hupanda miti hiyo na kungoja hadi miaka mitano iishe ndiposa waivune na sijajutia kwa uamuzi niliochukua,” Ombati anaeleza.
Kabla ya kupanda nduma, shamba linafaa kuandaliwa vilivyo na mchanga kufanywa mwororo.
Magugu yote pia ni sharti yaondolewe kabla ya kuchimba mitaro ya karibu futi moja kwenda chini. Upana kati ya mtaro mmoja hadi mwingine usipite mita 50 ili shamba lisitiri mimea mingi.
Mitaro ikishachimbwa, mbolea asilia ambayo imeundwa kutokana na samadi ya ng’ombe au mifugo wengine humwagwa.
“Baada ya kuweka mbolea hiyo, leta miche ya nduma na ipande kwa kuipa nafasi katika mitaro iliyochimbwa. Nduma zinapokua, hutoa mimea mingine michanga kando yake na hiyo yaweza kung’olewa na kupandwa kwenye mitaro. Pia, ukishavuna nduma, mashina yanayobaki baada ya kuondoa viazi yanaweza kupandwa tena na yakanawiri,” anaongeza mkulima huyu.
Nduma zikishamea na kuanza kupaliliwa, Ombati anahoji kuwa mkulima anafaa kuhakikisha kuwa hamna udongo mwingi unaokaribia mashina.
Hili linasaidisa kufanya mashina ya nduma kunenepa ili kuunda viazi vikubwa ambavyo vitanunuliwa kwa bei nzuri.
Tangu mkulima huyu aanze ukulima huu, hajawahi kushuhudia magonjwa mengi yanayoathiri zao hilo lakini anaonya kwamba mkulima asijaribu kutumia fatalaiza zinazonunuliwa madukani.
“Fatalaiza za kununua hazisikizani kabisa na nduma. Mbolea hiyo ina kemikali ambazo hukata mizizi ya mimea kuifanya inyauke. Ikiwa mmea ulikuwa umeweka viazi, vitaoza,” Ombati anahoji.
Tatizo jingine analosema amekumbana nalo mkulima huyu ni wezi wanaofika shambani mwake nyakati za usiku na kuvuna nduma zake.
Katika mkesha wa siku tuliyofika shambani kwa Ombati kwa mahojiano, wezi walikuwa wamemwibia nduma nyingi.Hata hivyo, alidokeza kuwa hilo halimbabaishi kwani nduma zilizosalia zina uwezo wa kumletea faida.
Amepanda nduma za aina ya majani mabichi yaliyokolea kabisa.
Kuna aina nyingine ya nduma zenye majani ya zambarau lakini mkulima huyu anadokeza kuwa zile za majani mabichi yaliyokolea zinampeleka vizuri.
Anaeleza kuwa kila nduma kubwa anayovuna huiuza Sh100.
Kutoka kwa shamba lake, Ombati huvuna angalau gunia 30 kila mwezi. Kila gunia analiuza kwa Sh 7,000, kumaanisha kwamba, mkulima huyo hutengeneza angalau Sh210,000 kwa mwezi.
Wateja wake wengi wapo katika mji wa Kisii, japo anaeleza kuwa wapo wanunuzi wanaotoka katika miji mingine.
Ili kuhakikisha wateja wake hawakosi nduma, Ombati ameligawanya shamba lake kusitiri mimea iliyo katika viwango tofauti tofauti vya ukuaji.
Kuna mimea ya nduma iliyomaliza miezi miwili, mingine minne na kuendelea. Hili anasema linamsaidia pakubwa kuvuna kwa wakati tofauti ili wateja wake wasisumbuke.
Wakulima wengine kijijini kwao wameanza polepole kukuza nduma na mkulima huyo amejitolea kuwapa mafunzo ya bure ili nao wafaidi maishani.
Yeye pia huhudhuria maonyesho ya kilimo ili kujifunza mengi kuhusu kilimo.
Anawarai wakulima wengine hasa vijana kuiga mtindo wake na kujiondoa kutoka umasikini kupitia kilimo hiki.
“Nduma zimenisaidia kuwasomesha wanangu, kujijengea nyumba nzuri na duka dogo kijijini kwetu. Ndizo pia zilizonipa mtaji wa kuanzisha biashara zingine kama vile ufugaji wa kuku na ng’ombe. Ukiwa mkulima, hufai kuwa na tegemeo moja bali vitu vingi ili kimoja kikianguka au kuletea hasara, kingine kitakuinua,” Ombati anadokeza.
Anawashauri vijana waliomaliza shule lakini hawana ajira kutosumbuka kutafuta kazi lakini kujaribu kilimo kama chake.
“Kuna pesa ardhini. Vijana waje wapokee mafunzo na wafanye kilimo kama hiki. Ikiwa watakizamia, hakuna yule atakayewaza kuhusu kuajiriwa tena,” akasema Ombati.
Mkulima huyu ameajiri zaidi ya watu 30 wanaomsaidia kupalilia nduma zake na wanapokea malipo mazuri kutoka kwake.