Vijana 122,000 walionufaika na pesa za NYOTA sasa kupokea mafunzo ya kukuza biashara
ZAIDI ya vijana 122,000 waliopokea mtaji wa kuanzisha biashara kupitia mradi wa National Youth Opportunities Towards Advancement (NYOTA) wataanza mpango unaolenga kuimarisha biashara zao na kuongeza nafasi za kuzikuza kwa muda mrefu.
Mpango huo ulianza Jumatatu, huku washauri wa biashara zaidi ya 4,879 wakiajiriwa kote nchini kuwasaidia vijana hao.
Katibu katika Idara ya Maendeleo ya Biashara Ndogo na za Kati, Susan Mang’eni, alisema kila mnufaika atapangiwa mshauri mwenye uzoefu wa biashara.
Kila mshauri atahudumia vijana wasiozidi 20.
Mpango huo utahusisha ziara za biashara, ushauri kati ya wafanyabiashara wenzao, uzoefu wa biashara, mafunzo, ushauri na kuwaunganisha na masoko.
Mpango huo ni sehemu ya juhudi za serikali kuwawezesha vijana kujiajiri kupitia mafunzo ya ujuzi na kupata mtaji wa kuanzisha biashara.
Mradi wa NYOTA ulizinduliwa Machi 2025 na hutumia teknolojia ya kidijitali kuwawezesha vijana kupata fursa katika maeneo mbalimbali nchini.
Mnamo Julai 10, 2026, serikali ilitoa mtaji kwa zaidi ya vijana 122,000 walionufaika na mpango wa kusaidia biashara ili waanzishe au kupanua shughuli zao.
Mradi huo unawahusisha vijana kutoka wadi zote 1,450 nchini, hasa wale walio katika viwango vya chini vya kiuchumi.
Serikali pia inaandaa njia mpya za ufadhili zitakazowawezesha wanufaika kupata fedha zaidi kupitia hazina za serikali.
Hatua hiyo inafuatia agizo la Rais William Ruto la kupanua upatikanaji wa fedha kwa vijana wa NYOTA.
Idara hiyo pia inashirikiana na serikali za kaunti kuandaa mfumo wa kuwaondolea wanufaika wa NYOTA baadhi ya ada za leseni za biashara ili kuwawezesha kupata masoko na maeneo bora ya kufanyia biashara.
Mafunzo ya Access to Government Procurement Opportunities (AGPO) yanatarajiwa kuanza mwezi ujao na yanalenga zaidi ya vijana 600,000.
Mafunzo hayo yatawapa ujuzi wa kushiriki katika zabuni za serikali.
Wakati huo huo, mpango wa On-the-Job Experience (OJE) unaendelea katika kaunti 18, ambako vijana wanapitia mafunzo ya kukuza ujuzi wa kijamii na kihisia.
BI Mang’eni aliwataka vijana kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo, akisema kukamilisha mpango huo ni sharti la kuendelea kupata msaada katika hatua inayofuata.
Lengo ni kuwapa vijana zaidi ya fedha za kuanzisha biashara, na pia maarifa, mitandao na mwongozo wa kuwasaidia kujenga biashara endelevu.