Uboreshaji soko la avokado kupitia chama cha ushirika
KILICHOANZA kama mazungumzo yasiyo rasmi kati ya viongozi wa wakulima waliokuwa wamechoshwa na kero za mabroka na mawakala kwenye uuzaji wa avokado Murang’a, sasa kimegeuka kuwa jukwaa linalowapa wakulima haswa wa mashamba madogo afueni kimapato.
Wakulima wa matunda hayo ambayo pia yanajulikana kama maparachichi, wanaweza kuwahi soko la nje lenye faida bora.
Hii ndiyo hadithi ya Murang’a Avocado Farmers’ Co-operative Union Limited, ambayo kulingana na Meneja wake wa Miradi na Uhamasishaji wa Raslimali, John Ruoho Wangechi, chama hicho cha ushirika kilianzishwa kutokana na changamoto zilizokuwa zikikabili wakulima.
Kwa miaka mingi, wakulima walipunjwa na madalali, udanganyifu wa mazao shambani na masoko yasiyotabirika. “Mabroka wakija shambani, kando na kupunja mkulima kipesa na kisoko, walikuwa wakipakia avokado kupita kiasi au kiwango wanachokubaliana,” anaelezea.
Ruoho anasema wakati wazo la kuunda chama hicho lilipoibuka, maparachichi yakuwa yakiuzwa kwa bei ya Sh2 hadi Sh10 kwa kila tunda, bila kujali ukubwa au ubora. Mfumo huo uliwaacha wakulima bila kujitetea kupata malipo bora.
Hata hivyo, kuanzishwa kwa Murang’a Avocado Farmers’ Co-operative Union Limited kumeleta mabadiliko makubwa, hasa baada ya kuhamia mfumo wa malipo kwa njia ya kilo badala ya kuhesabu matunda. “Sasa tunatumia mfumo wa kilo. Shamba likisimamiwa vizuri na kutoa mazao bora, mkulima hulipwa vyema na zaidi,” anasema.

Chama hicho cha ushirika na kilichosajiliwa rasmi Januari 2020, kilianza na vyama vidogo vinane lakini sasa vimefika 22, huku vikihudumia takriban wakulima 8,700 wanaoleta mazao bila kukosa. Kina zaidi ya wanachama 15,000 waliosajiliwa na zaidi ya wakulima 50,000 wa avokado, kulingana na rejista.
Hutoa huduma za kitaalamu, ikiwemo mafunzo ya usimamizi wa mashamba, kilimo bora na matumizi ya miche iliyoidhinishwa. “Mazao hukusanywa kwa pamoja na kuuzwa kupitia wauzaji na waagizaji wa nje wanaokidhi viwango vya kimataifa kama vile GlobalGAP,” Ruoho akaambia ‘Akilimali’ kwenye mahojiano ya kipekee.
Ulaya na Nchi za Milki ya Kiarabu haswa Mashariki ya Kati ndizo masoko makuu ya maparachichi ya Kenya, huku China ikiwa soko lenye uwezo mkubwa lakini lenye masharti makali ya udhibiti.
Msimu uliopita, chama kilikusanya karibu kilo 574,000 za avokado. Hata hivyo, kiasi hicho kilikuwa chini ya matarajio kwa sababu ya kuchelewa kwa vibali vya udhibiti na mabadiliko ya hali ya hewa yaliyosababisha matunda kukomaa mapema.
Ruoho anasema wakulima kwa sasa hupata kati ya Sh80 na Sh90 kwa kilo katika soko la ndani kwa ndani, huku bei ikibadilika kulingana na mahitaji na ubora.
Murang’a Avocado Farmers’ Co-operative Union Limited ilikuwa kati ya washirika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Shirika la Wakulima Duniani (WFO) wa mwaka huu, 2026, uliofanyika Nairobi kati ya Juni 8 na 11, ambapo cham hicho cha ushirika kilionyesha bidhaa zake, avokado. Kongamano hillo lilihudhuriwa na viongozi na wadauhusika wa kilimo nchini na pia kutoka sehemu mbalimbali duniani.
Akizungumza wakati wa ufunguzi rasmi, Waziri wa Kilimo na Maendeleo ya Mifugo Mutahi Kagwe alisisitiza umuhimu wa wakulima kujipanga kwenye mashirika ili kubadilisha sekta ya kilimo. “Wakulima wa mashamba madogo ndio uti wa mgongo kuboresha mifumo yetu ya chakula. Wapojipanga, hupata sauti ya majadiliano, kuimarisha sera na kupata heshima katika uzalishaji, kilele chake kikiwa kupata soko bora,” Waziri Kagwe alisema.

Kaulimbiu ya kongamano hilo lililoandaliwa na Shirikisho la Kitaifa la Wakulima wa Kenya (KENAFF) kwa ushirikiano na Shirika la Wakulima Duniani (WFO), ilikuwa “Future Fields: Investing in Farmers’ Organisations and Empowering Communities for Sustainable Agriculture.”
Kilimo cha maparachichi kimekuwa chanzo cha utajiri maeneo ya mashambani, kikisaidia familia kugharamia elimu, kuboresha maisha na uchumi.
Hata hivyo, sekta hii inakabiliwa na changamoto za hasara hasa baada ya mavuno, zinazokadiriwa kufikia asilimia 60–65, pamoja na ushindani kutoka kwa wachakataji wa mafuta ya maparachichi. Wasindikaji wa mafuta hulipa wakulima kati ya Sh18–20 kwa kilo, ikilinganishwa na zaidi ya Sh80 kwa kilo katika soko la nje.
Ruoho anasema tofauti hiyo ya bei inawashawishi baadhi ya wakulima kuvuna mapema na kuelekeza mazao yao kwenye viwanda vya mafuta, jambo linalopunguza uuzaji wa avokado kwenye masoko ya nje.
Kwa upande mwingine, teknolojia imekuwa nguzo muhimu katika shughuli za Murang’a Avocado Farmers’ Co-operative Union Limited, huku malipo yakifanywa kwa njia ya simu, utunzaji wa kumbukumbu kidijitali na majukwaa ya mitandao ya kijamii yakisaidia kuboresha mawasiliano na masoko.
Chama hicho cha ushirika kimekuwa kikipigwa jeki na shirika la We Effect, hasa katika uimarishaji wa masuala ya uongozi, uwekezaji wa fedha, kuhamasisha usawa wa kijinsia na matumizi ya teknolojia.