Makala

AKILIMALI: Usanii unaohitaji subira tele ingawa huvuta heri baadaye

July 4th, 2019 Kusoma ni dakika: 2

Na RICHARD MAOSI

UFINYANZI sawa na uchongaji vinyago kwa kutumia udongo ni sanaa ya kale miongoni mwa tamaduni nyingi za Afrika.

Karne hii ya 21 ni watu wachache wenye ujuzi huu huku wito ukitolewa kwa vijana wajifundishe kufanya kazi ya mikono.

Kutokana na tajriba ya kufanya ufinyanzi, binadamu anaweza kuhifadhi kumbukumbu za historia yake, kwa lengo la kuwavutia watalii wanaotembelea mataifa yao.

Wataalamu wanaamini kuwa ufinyanzi sio tu kwa kuhifadhi kumbukumbu za historia bali pia ni nyenzo muhimu wanayotumia wasomi na watafiti kuyaelewa mazingira yao.

Akilimali ilipata fursa ya kuzuru barabara ya Nakuru-Nairobi, kuzungumza na Johnson Kirago, 40, mjasiriamali anayetumia udongo katika shughuli za kila siku kujikimu kimaisha.

Johnson anasema udongo ni kama dhahabu sio tu kwa mkulima, bali pia kwa kizazi cha sasa kinachotegemea teknolojia na ufundi kutengeneza vyombo kwa matumizi ya binadamu.

Kupitia malighafi haya ya asilia anaweza kutengeneza vinyago vya aina na maumbo mbalimbali, kwa kutegemea mahitaji ya wateja wake, wanaomiminika kutoka ndani na nje ya kaunti ya Nakuru.

Anasema miaka ya mbeleni mbao zilikuwa ni tele, ndiposa watu wengi wangeweza kupata bidhaa za kuchonga kwa urahisi. Kinyume na siku hizi ambapo kampeni dhidi ya ukataji miti zimeshamiri.

“Haja ya kuhifadhi mazingira ilinifanya kugeukia mchanga usiovunjika kwa urahisi(clay) kutengeneza bidhaa zangu. Aidha ilinipasa kuwa mbunifu kila ninapokaa ndani ya karakana kuibua na kuunda miundo tofauti,” akasema.

Kulingana naye, vijana wanaohangaika kutafuta ajira wanaweza kuyatumia malighafi yanayopatikana kwenye mazingira yao kujiendeleza kimaisha, kama vile upepo, mvua, mawe na hata jua.

Ili wafanikiwe zaidi watahitajika kukaa karibu na wazee ambao wamekonga ili kujipatia ujuzi huu ambao umebakia mikononi mwa watu wachache tu.

Johnson anaeleza kuwa mbali na kuwa na stadi ya kuchonga vinyago yeyote anayezamia kazi hii lazima awe fundi stadi inapokuja kwenye suala la kupaka rangi.

Rangi ziendane na hali halisia ya maisha, akiamini watu wanapendelea rangi zenye mvuto. Kila umbo linatakiwa kukaushwa, kupambwa na kuchomwa kwa moto.

Na kwa njia hii ndipo anaweza kupata vyombo vilivyozoeleka kutumika nyumbani kama vile vyungu, mabakuli, vikombe na sahani au wakati mwingine mabirika.

 

Baadhi ya wateja waliomiminika kukagua bidhaa kutokana na ufinyanzi katika eneo la Section 58 Kaunti ya Nakuru. Picha/ Richard Maosi

Johnson anasema udongo wa mfinyanzi una chembechembe ndogo sana. Uwe ule unaoweza kuyashikilia maji kwa muda mrefu, uwe laini na wa kushikamana vyema, lakini unapokauka uwe mgumu kiasi.

Bidhaa

Nyingi ya bidhaa zake hapa ni zile za kupanda maua kwenye bustani au mitungi ya kuhifadhi maji.

Ingawa anasema leo hii vyombo vingi vya mfinyanzi hutengenezwa viwandani kwa sababu ya ukosefu wa nguvu kazi.

Mchanga unapatikana kwa wingi katika kaunti ya Nakuru, lakini Johnson alituelezea kuwa sio mchanga wa aina yeyote unaweza kutumika, isipokuwa ule unaokuwa mgumu kila baadaya kuchomwa.

Yeye hupata mchanga kutoka eneo la Menengai crater kwa Sh700 kila tani, kisha akausafirisha hadi kwenye karakana yake iliyo mkabala na njia kuu ya kuelekea Nairobi eneo linalofahamika kama Section 58.

Akishirikiana na vibarua wake huacha mchanga ukauke kabla ya kutumika, kwani anasema endapo mchanga hautakauka vyema unaweza kufanya umbo kuwa hafifu kwa kutengeneza nyufa.

Johnson anaona kuwa wanafunzi kati ya umri 8-12 wanaweza kufundishwa ustadi wa ufinyanzi na wakaiboresha tajriba yao wanapofikia umri wa miaka 15 hivi wakaboresha ujuzi na kufanya ufinyanzi kama taaluma.

Kulingana naye endapo mjasiria mali atazingatia hatua zote za ufinyanzi, anaweza kujiajiri na kuwaajiri watu wengine, anasema sanaa hii inaweza kuinua mtu kimaisha awe mtu wa kujitegemea.

Anapendekeza kozi maalum zinazoshirikisha ujuzi wa mikono, zianzishwe kwenye taasisi za mafunzo ya kiufundi kote nchini ili kukabiliana na ukosefu wa nafasi za ajira kote nchini.