Alianzisha mradi wa mbuzi wa maziwa ambao ni bora zaidi nchini akiwa angali chuoni
MAJAJI walipotembelea banda la maonyesho la Caleb Mwenda katika Maonyesho ya Kimataifa ya Kilimo na Kibiashara ya Nairobi 2025 yaliyoandaliwa na Agricultural Society of Kenya (ASK) Jamhuri Grounds, Nairobi, mkulima huyo mchanga hakujua jitihada zake katika ufugaji wa mbuzi zingetambuliwa.
Kwake, ilikuwa fursa nyingine tu ya kuonyesha mbuzi wake aina ya Toggenburg.
Lakini matokeo yalipotangazwa, Mwenda alishindwa kuamini alichosikia—mmoja wa mbuzi wake alitangazwa kuwa Bingwa Mkuu (Supreme Champion) kwenye daraja la wafugaji wa mbuzi, heshima ya juu kabisa katika kundi hilo.
Ushindi huo ulimfanya kijana huyu wa miaka 26 kuwa kivutio kikubwa kwa wageni na washirika waliotaka kujua siri ya mafanikio yake. “Sikuamini ningetambuliwa Kenya nzima! Mbuzi huyu ameshiriki mara kadhaa kwenye mashindano, hata hivyo, mwaka huu (2025) ndio ameng’aa,” Mwenda akaambia Akilimali Dijitali kwenye mahojiano ya kipekee.
Dume lililoshinda, bridi ya Toggenburg, lina uzito wa karibu kilo 60 na lina sifa zote za mbuzi bora wa maziwa. Rangi yake ya kahawia, maskio marefu yaliyolegea, umbo lililosawazika na mwili wenye nguvu, maumbile yote hayo yalivutia majaji.

Mwenda anasema walizingatia aina ya uzao, umbo, tabia na jinsi mnyama alivyowasilishwa—na mbuzi wake aliafikia mahitaji na viwango vyote.
Anaeleza mafanikio hayo yametokana na uchaguaji makini wa mbegu na ufugaji bora. “Tangu kuzaliwa, ilikuwa dhahiri ni mbuzi wa kipekee. Mama yake alikuwa mkubwa na mwenye afya, na baba yake alikuwa wa kizazi bora,” alisema.
Safari ya Mwenda ilianza akiwa bado mwanafunzi wa mwaka wa kwanza katika Chuo Kikuu cha Maasai Mara, alikosomea Digrii ya Masuala ya Uchumi na Takwimu.
Kwa akiba ya Sh40,000, alinunua mbuzi wawili jike, akajenga zizi na kununua chakula. Mradi wa Chamugo Dairy Goats ukazaliwa.
Miaka ya awali haikuwa rahisi. Kusawazisha masomo na ufugaji ilikuwa kibarua na changamoto, na faida zilikuwa haba. “Lakini sikukata tamaa,” alisema.
Baada ya kuhitimu, alijitosa kikamilifu, akizuru wafugaji wa mbuzi waliobobea kujifunza kuhusu uzalishaji, lishe na jinsi ya kudhibiti magonjwa.
Leo hii, mradi wake wa Chamugo Dairy Goats una zaidi ya mbuzi 100, wakiwemo 15 wanaokamuliwa na madume sita ya kujamiisha.
Aidha, barobaro huyu ameajiri wafanyakazi wanne wa kudumu.

Mbuzi hulishwa majani na matawi ya mahindi yaliyokauka, Lucerne, majani mabichi na vyakula vya madukani kama vile dairy meal na pia kuwapa madini yenye virutubisho.
“Niko makini sana na ratiba ya chakula na zaidi ya yote mlo wanaokula, chanjo na matibabu,” anaelezea. Hali ya usafi kwenye mabanda ya mbuzi wake ni ya hadhi ya juu.
Kila mbuzi, anafichua huzalisha lita tatu hadi tano za maziwa kwa siku, kila lita akiuza Sh150, hasa kwa hospitali za eneo analotoka, Meru.
Isitoshe, hupata kipato kupitia huduma za kujamiisha mbuzi ambapo hutoza Sh1,500 na vilevile kuuza madume yanayogharimu Sh70,000 kila mmoja.
Licha ya mafanikio, anakumbana na changamoto za magonjwa, gharama ya juu ya chakula hasa cha madukani na hali ya hewa – kiangazi kufuatia athari za mabadiliko ya tabianchi.
Hata hivyo, anaendelea kuwekeza kwenye ufugaji-biashara wa mbuzi na kuhakikisha uendelevu, nidhamu na uaminifu zikiwa nguzo kuu.