Anavyohamasisha kilimohai, endelevu kwa kutengeneza fatalaiza ya maji
KINACHOMRIDHISHA zaidi Thuranira Thiaine ni kuona jinsi miti kwenye misitu inavyostawi na baadhi kuzalisha matunda bila kuwekwa pembejeo yoyote ile, jambo analoamini lingefanana na mashamba watu wangekuwa salama kiafya.
Hata hivyo, ni suala ambalo huenda likachukua miaka na mikaka kufuatia kudhoofika kwa afya ya udongo—sababu zilizochangiwa na binadamu kwa kuendelea kutumia fatalaiza na dawa zenye kemikali.
Hilo, linamkumbusha Thuranira kati ya 2015 na 2017, akihudumu kama afisa wa mawasiliano katika Kaunti ya Meru ambapo alikuwa akishuhudia foleni ndefu ya wakulima, wakisubiri kupata fatalaiza.

“Kilichonigusa zaidi si idadi yao pekee, bali nyuso zao—watu waliokula chumvi, yaani wazee waliolima maisha yao yote lakini sasa walikuwa mateka wa mfumo usiotosheleza mahitaji yao,” Thuranira anasema.
Maswali yalimtinga, mojawapo likiwa: kwa nini wakulima wahangaike kupata mbolea ilhali malighafi yapo kila mahali?
Ni swali lililoishia kuzaa Mazao Organic, kampuni inayobadilisha mtazamo wa wakulima kuhusu udongo, chakula na haja ya kilimo endelevu.
Wakati huo, Thuranira alikuwa bado mtumishi wa umma, akikerwa na taratibu ndefu kwenye serikali za ugatuzi na ile kuu kusuluhisha matatizo katika jamii.

Anakumbuka Mkenya aliyekuwa akifanya kazi Yemen katika kampuni ya kutengeneza mbolea asilia na fatalaiza, aliyependekeza ushirikiano wake na Kaunti ya Meru kuzalisha mbolea kwa wakulima wadogo. Ingawa wazo lilikuwa zuri, taratibu zilichelewesha kila kitu na fursa hiyo ikapotea.
Baada ya kuacha kazi ya kaunti na kujiingiza kwenye ajira binafsi, alirejea kwa Mkenya huyo.
Safari hii, anasema bila vizuizi vya utaratibu kwenye serikali, ndoto ya safari yake kuokoa wakulima iliona mwanga.
Aliungana na Charles Onyango, ambaye ni mhandisi, wakabuni Mazao Organic kwa lengo moja: kuwapatia wakulima mboleahai nafuu, inayoundiwa Kenya kwa kutumia malighafi ya ndani kwa ndani na inayorejesha uhai wa udongo.

Kampuni hiyo ya kuunda mboleahai ya maji, ilianzishwa mwaka 2020, katikati ya janga la Covid-19, kwa mtaji wa Sh5 milioni.
Ni hela ambazo Thuranira anasema wawili hao waasisi walikusanya kutoka kwa akiba yao, ikiwemo kuuza kipande cha shamba Meru kilichowapa Sh2.5 milioni.
“Haikuwa maamuzi rahisi, ikizingatiwa kuwa waanzilishi wengi wa biashara ukosefu wa fedha ndio changamoto kuu,” anaelezea, akikumbuka jinsi hata kupata mkopo kutoka kwa wanafamilia ilikuwa ngoma.
Miaka mitano baadaye, Mazao Organic imekuwa nguzo ya kuhamasisha kilimohai na endelevu si tu katika Kaunti ya Meru, bali taifa zima.
Fatalaiza ya maji wanayounda, kando na kusaidia kufufua hadhi ya udongo, ina chembechembe kukabiliana na wadudu waharibifu kwa mimea na magonjwa ya mimea.

“Kinachoendelea kudhoofisha udongo ni matumizi ya pembejeo haswa fatalaiza na dawa zenye kemikali. Kando na kuathiri mashamba, zinaleta madhara kwa miili ya binadamu,” anasikitika.
Kutimiza shabaha yao, Thuranira na Onyango wanatumia malighafi hai.
Aidha, hutumia samadi ya mifugo kama vile ng’ombe, mbuzi, kondoo na kuku, jivu pamoja na chembechembe hai kutoka kwenye misitu na mazingira ya chumvi.
“Chembechembe hizo; mesophiles, thermophiles na saline microbes, zinarahisisha muda wa kutengeneza mbolea kutoka miezi sita hadi chini ya siku 10,” akaambia Akilimali wakati wa mahojiano katika kiwanda cha kampuni hiyo Kianjai, Tigania West, Kaunti ya Meru.
Mbali na uundaji wa mbolea, Mazao Organic pia huunda Mazao Digester ambayo ni dawa dhidi ya vimelea vya choo na wadudu.

“Tunapozungumza kuhusu majitaka, Mazao Digester ndio suluhu ya kuangazia kero hiyo—kuyatibu kabla ya kuachiliwa na viwanda,” akasema.
“Isitoshe, ni kiungo muhimu kufupisha siku za kuunda fatalaiza ya maji.”
Jivu nalo, linapomaliza utendakazi wake hugeuzwa kuwa makaa aina ya briquettes.
Kwenye kiwanda, hakuna kinachopotea-—briquettes hutumia kwa minajili ya kuchoma kwenye taratibu zinazohitaji moto, Thuranira anafafanua.
Mbolea yao imesheheni Nitrogen, Phosphorous na Potassium (NPK).
“Tunakadiria ukuaji mkubwa,” Thuranira anakiri.

Leo hii, kiwanda cha Mazao Organic kinazalisha zaidi ya lita 1,000 ya fatalaiza kwa mwezi, kutoka lita 100 awali, na kuhudumia wakulima zaidi ya 5,000 kote nchini.
Lita moja inayouzwa Sh2,000 inatosha ekari moja.
Aidha, kampuni hiyo ina wafanyakazi 12 wa kudumu na vibarua wengine 120 wasio wa moja kwa moja.
Kabla ya kuingilia kilimo, Thuranira aliwahi kuhudumu kwenye sekta ya benki baada ya kuhitimu Chuo Kikuu 2005 kwa Digrii ya Masuala ya Mawasiliano.
Anasema benki ilimpa utulivu wa kifedha, lakini haikuwa na maana ya kina aliyokuwa akitafuta. Kilimo kilimvutia kwa sababu ni halisi na cha kugusa maisha ya watu.
