Askofu Gwajima akaa ngumu hata baada ya kanisa lake kufungwa na serikali ya Tanzania
KANISA la Glory of Christ Tanzania lilifutwa kutoka sajili ya makanisa nchini humo Jumatatu Askofu ila Josephat Gwajima ameshikilia kuwa ataendelea kuhubiri injili na kukosoa maovu ya utawala wa Rais Samia Suluhu Hassan.
Kwenye video iliyosambaa mitandaoni Jumanne, Askofu huyo ambaye pia ni Mbunge wa Kawe anasema ataendelea kulaani visa vya utekaji nyara wa viongozi wa upinzani na wakosoaji wengine wa serikali ya nchi hiyo.
“Injli itaendelea. Sitayumba, Sitabadilika, Sitalegeza msimamo wangu… nitasimama nalo,” akaeleza Mhubiri huyo ambaye ni Mbunge wa chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM), chake Rais Samia.
“Sisi wanachama wa CCM sio watekaji nyara. Rais wa awamu ya kwanza Julius Nyerere hakutuachia chama cha CCM tukitumie kuendeleza utekaji nyara, John Pombe Magufuli naye hakutuachia chama hiki tukitumie kuendeleza maovu kama haya,” Askofu Gwajima akaongeza.
Alifichua kuwa kufikia sasa watu 80, wengi wao wakiwa wafuasi wa upinzani wametekwa nyara nchini Tanzania, baadhi yao wakipatikana wameuawa kwa njia ya kutatanisha.
Wiki jana, Gwajima alitifua vumbi kwenye kikao na wanahabari alipoibua malalamishi kuhusu kukithiri kwa visa vya utekaji nyara alivyodai vinaendeshwa na maafisa wa usalama wa serikali ya Tanzania.
Aliuliza iwapo serikali ingechelea kuchukua hatua zozote ikiwa waliotekwa wangekuwa “watoto au marafiki wa maafisa wanaoshikilia vyeo vya juu serikalini.”
Baada ya Askofu huyo kuishutumu serikali kwa maovu hao, Msajili wa Makundi vya Kiraia alifuta jina la Kanisa lake la Glory of Christ kutoka sajili ya makanisa nchini Tanzania. Aidha, matawi yote ya kanisa hilo nchini humo yalizimwa kuendesha shughuli za kawaida.
Kulingana barua iliyoandikiwa na Msajili wa Makundi ya Kiraia Emmanuel Kihampa, hatua hiyo ilichukuliwa kwa sababu kanisa hilo limekuwa likitoa mahubiri ya “kuchochea umma kisiasa.”
Bw Kihampa alieleza kuwa Kanisa la Glory of Christ lilivunja kifungu nambari 337 cha Sheria ya Makundi ya Kiraia kwa kuendesha mahubiri kwa njia inayogonganisha raia na serikali.
“Kupitia mamlaka niliyopewa, nafutilia mbali jina la Kanisa la Glory of Christ kutoka kwa orodha ya makanisa nchini Tanzania. Kwa hivyo, unapaswa kusitisha shughuli zote za kanisa hili mara moja,” akasema Bw Kihampa akiongeza kuwa Kanisa hilo linahatarisha amani na uthabiti nchini Tanzania.
Hata hivyo, barua hiyo ambayo ilinakiliwa kwa Inspekta Jenerali wa Polisi Cammilus Wambura, ilisema kuwa Askofu Gwajima amepewa mwanya wa siku 21 kukata rufaa dhidi ya hatua hiyo.
Lakini mnamo Jumanne, Juni 3, 2025, majira ya asubuhi, gazeti la “The Citizen” liliripoti kuwa maafisa 20 walizingira makao makuu ya Kanisa hilo katika eneo la Ubongo, jijini Dar es Salama.
Maafisa hao ambao walikuwa wamejihami kwa zana za kivita walizuia mtu yeyote kuingia ndani ya majengo ya Kanisa hilo la Glory of Christ.
Kanisa hilo limezimwa baada ya raia wa Kenya na wenzao wa Tanzania kurushiana cheche mitandaoni kufuatia kisa cha juzi ambapo mwanaharakati Boniface Mwangi (Mkenya) na wakili Agatha Atuhaire (Raia wa Uganda) walizuiliwa na kuteswa kwa siku kadhaa kabla ya kuachiliwa.
Wawili hao ni miongoni mwa wanaharakati wa kutetea haki za kibinadamu waliosafiri hadi Tanzania kuhudhuria kikao cha kusikizwa kwa kesi ya uhaini dhidi ya kiongozi wa upinzani Tundu Lissu.
Lissu ni mwenyekiti wa chama kikuu cha upinzani nchini humo, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na alikamatwa kwa kushinikiza mageuzi ya sheria za uchaguzi pamoja na kuwaraia raia kususia uchaguzi mkuu ulioratibiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.
Kiongozi wa chama cha People’s Liberation Party (PLP) Martha Karua, Jaji Mkuu wa zamani Willy Mutunga na wanaharakati Hussein Khalid, Hanifa Adan, Lynn Ngugi na wakili Gloria Kimani pia walienda Tanzania kuhudhuria kesi hiyo lakini wakazuiliwa na kurejeshwa Kenya kwa nguvu.
Hatua hiyo, imeshutumiwa vikali na makundi ya kitetea haki za kibinadamu na viongozi wa upizania nchini Kenya.