Chakula chenye sumu? Kesi yadai kemikali zinaua Wakenya
WAKENYA wanatumia chakula kilicholimwa kwa kutumia dawa za kuua wadudu na magugu zenye sumu na zinazosababisha saratani ambazo tayari zimepigwa marufuku katika mataifa yaliyoendelea, kwa mujibu wa kesi iliyowasilishwa katika Mahakama Kuu jijini Nairobi.
Hata hivyo, serikali na makampuni makubwa ya kimataifa ya kutengeneza dawa hizi kama Monsanto, Bayer na Syngenta zimeungana kupinga kesi hiyo kwa kudai kuwa kemikali 11 zinatajwa katika kesi, kama vile glyphosate, si hatari kwa afya ya binadamu wala mazingira.
Bodi ya Kudhibiti Bidhaa za Kuua Wadudu (PCPB), ambayo ni ya serikali, imesema kuwa agizo la mahakama la kuondoa dawa hizo sokoni kama walivyoomba walalamishi, litapelekea kupungua kwa mavuno na kuhatarisha utoshelevu wa chakula nchini.
Kesi hiyo iliwasilishwa na shirika la mazingira la African Centre for Corrective and Preventive Action pamoja na mkazi wa Nanyuki, Kelvin Mugambi Kubai, wakidai kuwa dawa hatari zinazotumika kwenye kilimo cha Kenya zinaweza kusababisha saratani na madhara mengine ya kiafya.
Wamedai kuwa tafiti mbalimbali za kisayansi kuhusu baadhi ya kemikali hizo, zimeonyesha kuwa zinaathiri maendeleo ya ubongo kwa watoto na kupunguza homoni inayosababisha nguvu za kiume..
Kemikali hizo 11 ni pamoja na: glyphosate, paraquat, imidacloprid, clothianidin, fipronil, chlorpyrifos, thiacloprid, thiamethoxam, fenitrothion, malathion, na dinotefuran. Zinasemekana kuwa zimepigwa marufuku barani Ulaya lakini bado zinatumika sana kwenye kilimo cha maua, mboga na mazao mengine nchini Kenya.
Kulingana na walalamishi, serikali na mashirika yake pamoja na watengenezaji wa kemikali hizi wameshindwa kulinda afya na usalama wa wakulima na watumiaji wa chakula nchini kwa kuidhinisha matumizi ya bidhaa ambazo zimepigwa marufuku kwingineko kwa sababu ya hatari zake kiafya.
Mfano, kesi inadai kuwa kemikali ya paraquat huathiri afya kwa kuharibu seli za wanyama na binadamu.
“Kugunduliwa kwa hata viwango vidogo vya paraquat katika utotoni kunaweza kuathiri vibaya ukuaji wa ubongo. Pia imehusishwa na kansa na kupunguza homoni inayosababisha nguvu za kiume. Chlorpyrifos inajulikana kuathiri maendeleo ya ubongo hasa kwa watoto, pamoja na mfumo wa uzazi na neva,” wanasema walalamishi.
“Shirika la Kimataifa la Utafiti wa Saratani (IARC) limeonyesha ushahidi kuwa glyphosate inaleta kansa kwa binadamu. Fenitrothion ni sumu kwa mfumo wa uzazi na hubadilisha mfumo wa homoni kwa binadamu,” wanasisitiza.
Wanaongeza kuwa kemikali hiyo ya Fenitrothion haichagui wadudu, na inaathiri samaki, nyuki, na viumbe vingine vya majini ambavyo ni muhimu katika uzalishaji wa chakula.
Pia wamenukuu kesi tisa zilizowasilishwa Amerika dhidi ya watengenezaji wa dawa hizi kwa kushindwa kuwaonya watumiaji kuhusu hatari za kiafya, ikiwemo kansa.
“Nimejulishwa kuhusu uchunguzi uliofanywa na Mwanasheria Mkuu wa Jimbo la New York dhidi ya Bayer Crop Science LP na Monsanto kuhusu matangazo ya uongo yaliyosema bidhaa zao hazina sumu,” anasema Bw Kubai katika hati ya kiapo.
Ameambatanisha nakala ya mkataba uliotiwa saini Juni 14 2023 kati ya ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa New York, Bayer Crop Science LP na Monsanto wakikubali kuacha kutoa matangazo ya kupotosha kuhusu usalama wa glyphosate.
Bw Kubai anasisitiza kuwa Wakenya wanastahili ulinzi sawa kama watumiaji wa bidhaa hizo nje ya nchi.
Lakini Bodi ya PCPB na makampuni zomepinga kesi hiyo wakisema kuwa haina msingi wowote.
Mkurugenzi Mkuu wa PCPB, Dkt Esther Kimani, anasema kesi hiyo inategemea taarifa za zamani za kisayansi ambazo hazina uzito wa kisheria.
Anadai hakuna mojawapo ya kemikali 11 zilizoorodheshwa iliyowahi kutambuliwa kama “hatari sana kwa afya” na kwamba kabla ya kuidhinisha dawa yoyote, PCPB hufanya majaribio ya kina kwa ushirikiano na taasisi za utafiti na vyuo vikuu.