• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 2:07 PM
CHOCHEO: Mvuto wa dume la pembeni

CHOCHEO: Mvuto wa dume la pembeni

Na BENSON MATHEKA

NI miaka mitano sasa tangu *Hellen afunge pingu za maisha na Daniel.

Kabla ya harusi na miaka minne ya ndoa yao, hakudhani kama kuna wanaume wengine duniani hadi mwaka 2019 alipokutana na Steve, mfanyakazi mwenzake aliyeteka moyo wake na kumpagawisha kabisa kimahaba.

“Siwezi kuficha, ninampenda Steve. Ninavyohisi kumhusu imenifanya kujitambua na kuchanganyikiwa,” asema Hellen. Hata hivyo, anasema ingawa huwa wanachat kwenye mitandao ya kijamii na kuzungumza wakiwa kazini, hajawahi kumweleza anavyohisi kumhusu.

“Nimeolewa lakini nimelemewa na hisia kwa jamaa huyu. Sijui nitafanyaje kwa sababu nimefungwa na viapo vya ndoa kwamba nitakuwa mwaminifu kwa mume wangu hadi kifo kitapotutenganisha,” asema mwanadada huyu.

Lakini kwa Glady’s* ndoa haikuwa kizingiti alipokutana na John, barobaro kutoka Nigeria aliyedunga mkuki wa mapenzi katika moyo wake.

“Tulifanya mipango kwa siri na baada ya muda nilimuacha mume wangu na kuondoka na barafu ya moyo wangu hadi Afrika Kusini kwa miaka sita kisha nikarejea nchini kuwasilisha kesi ya talaka,” asema.

Wataalamu wa masuala ya mapenzi wanasema kuwa ni kawaida ya akina dada walio katika ndoa au katika uhusiano wa mapenzi kujipata katika crush, wakizuzuliwa kimapenzi na wanaume wengine.

“Huwa inatendeka. Ni kawaida ya mtu kujipata amevutiwa na mwanamume mwingine kando na mumewe. Wakati mwingine hisia za mapenzi kwa mgeni huyo huwa na nguvu na kufanya mtu kuvunja ndoa akidhani amepata mwanamume bora kuliko mumewe,” aeleza mwanasaikolojia Lucy Karimi wa kituo cha Love Care jijini Nairobi.

Kulingana na Karimi, hii imefanya idadi ya wanawake walio na mipango ya kando kuongezeka.

“Kuna wanaoamua potelea mbali na kujitosa katika mapenzi nje ya ndoa na wanaume wanaowazuzua. Ninataka kusema ni kuwazuzua tu kwa sababu kwa kawaida huwa hakuna cha mno isipokuwa kujivinjari na kulishana uroda. Ni uhusiano ambao huwa hauna mipango ya maana isipokuwa kuchangamshana tu,” asema na kuongeza:

“Ole wao wanaovunja ndoa zao kwa sababu ya kupagawishwa na wapenzi wa kando.”

Anasema siku hizi, imekuwa rahisi kwa watu kuendeleza mipango ya kando kwa sababu ya mitandao ya kijamii lakini athari zake zimekuwa zikifanya wengi kujuta.

“Ni vizuri kujaribu kujiepusha nayo kwa sababu japo inaweza kuwa siri kwa muda, athari zake ni mbaya kwa wahusika wote,” aeleza.

Wataalamu wanasema makosa wanayofanya watu wengi ni kuchukulia hisia za mapenzi wanazopata kuhusu watu wengine kwa uzito.

“Watu wengi siku hizi hawaamini kuwa kuvutiwa kimapenzi na watu wengine nje ya ndoa ni kukosa heshima. Wanaamini kuwa hawafai kunyima moyo wao unachotaka. Wanasahau kwa kufanya hivyo, huwa wanatengeneza njia ya kuelekea masononeko,” asema Purity Kembi, mwanasaikolojia katika kituo cha Beyond Love jijini Nairobi.

“Fikiria mara mbili na zaidi, crush haiwi mapenzi ya dhati wanavyoamini watu wengi na hapa nazungumzia wanawake. Hatima yake huwa ni kuvunjwa moyo na hii inaweza kutokea baada ya mtu kumuacha mume wake wa ndoa. Usiache mbachao kwa msala upitao,” asema.

Karimi anasema wanawake wanaoamini kwamba wanafaa kujiachilia kwa crush wao huwa wanakata tiketi ya masononeko.

Mtaalamu huyu anakiri kwamba ujio wa mitandao ya kijamii iliyorahisisha mawasiliano umefanya watu wengi kuvuka mipaka ya ndoa na kuwa na mahusiano ya mapenzi isiyo na faida zaidi ya kuchangamkiana kwa ufuska.

“Enzi ambazo macho ya mtu yalikuwa yakimuona mume au mkewe pekee zinaonekana kutoweka. Enzi hizo, viwango vya talaka na dhuluma katika ndoa vilikuwa vya chini,” asema na kuongeza kuwa viwango vya maisha ya kijamii hubadilika katika kila kizazi.

Mtaalamu huyo anaonya watu dhidi ya kuacha wachumba wao wa dhati ili kuandama penzi la pembeni.

You can share this post!

FUNGUKA: ‘Hana mali, amejaza vimada ila...

MWANAMUME KAMILI: Mwanadada usiye na dili naye, afanya nini...

adminleo