Akili MaliMakala

Dada wawili wanavyookoa ndizi kwa kuzichakata

Na SAMMY WAWERU February 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UNAPOZURU masoko mengi nchini, hutakosa kukutana na mkusanyiko wa mazao mabichi ya shambani yaliyotupwa; yaliyobondeka, baadhi kuiva kupita kiasi na mengine kuoza, yakigeuzwa kuwa taka.

Matunda yanaongoza kwenye orodha hiyo. Ndizi, maembe, maparachichi (avocado) na machungwa ni miongoni mwa mazao yanayopotea kwa wingi.

Taswira hii inaashiria haja ya kuwapiga jeki wakulima na wafanyabiashara kwa miundombinu bora ya uhifadhi na uchakataji ili kuongeza au kurefusha muda wa matumizi ya mazao.

Ndizi aina ya plantain zilizochakaa lakini bado ni bora. Picha|Sammy Waweru

Gapu hiyo ndiyo humpa motisha kila siku Triza Mwaniki anapofungua milango ya huduma za Lynt’s Limited, kampuni ya kuchakata ndizi maalum aina plantain iliyoko Kahawa West, Nairobi.

“Upotevu wa chakula ni changamoto kubwa nchini. Kenya hupoteza kati ya asilimia 20 hadi 30 ya mazao ya kilimo kutokana na hasara za baada ya mavuno, usafirishaji na masoko,” anasema Triza, ambaye ni mwanzilishi mwenza na mkurugenzi wa kampuni hiyo.

Anaongeza, “Tunachofanya ni kupunguza hasara hizo ambazo huishia kuwa upotevu mkubwa wa chakula.”

Triza Mwaniki akikagua ndizi kwenye ghala la Lynt’s Limited. Picha|Sammy Waweru

Lynt’s Ltd inamilikiwa na dada wawili, Triza na Lynn Mwaniki.

Wazo la kuunda kripsi za ndizi lilizaliwa mwaka 2017 wakati Lynn alipokuwa akisoma Uganda, ambako plaintain hutumiwa sana haswa kwenye mapishi.

“Niligundua nchini Kenya zilipuuzwa, licha ya kuwa na ladha tamu na zilizosheheni virutubisho,” Lynn anaelezea.

Mwaka 2021, baada ya msururu wa majaribio, Triza alifanikiwa kupata taratibu (recipe) za mapishi sahihi kuunda kripsi.

Triza Mwaniki akielezea kuhusu biashara ya uchakataji ndizi kuwa kripsi. Picha|Sammy Waweru

Kufikia 2023, anadokeza kwamba waliingia rasmi sokoni baada ya kupata leseni zinazohitajika.

Awali walitegemea ndizi kutoka Uganda, lakini changamoto za mipakani wakati wa janga la Covid-19 ziliwalazimisha kutafuta soko la ndani kwa ndani Kenya.

Triza, kwenye mahojiano ya kipekee na Akilimali anasema waligundua kuwa wakulima kutoka Kirinyaga, Embu na Meru walikuwa wakizalisha ndizi za plantain bila kupata soko lenye mapato bora.

“Kwa sasa, hununua kutoka Kirinyaga na kujiivishia kwenye kiwanda chetu,” akafichua.

Lynt’s Limited imejikita kwenye uchakataji ndizi aina ya plantain ambapo inaokoa wakulima kutoka Kirinyaga. Picha|Sammy Waweru

Iliwagharimu mtaji wa Sh300,000 kuanzisha biashara ya kuongeza ndizi thamani, ukipigwa jeki na michango ya wazazi na kutoka kwenye chama.

“Kufikia tulipo, imetugharimu kima cha Sh3 milioni,” Triza anasema.

Leo hii, Lynt’s Ltd huzalisha tani mbili za kripsi kwa mwezi, kutoka kilo 200 walipoanza biashara.

Triza Mwaniki akikatakata ndizi kuwa vipande. Picha|Sammy Waweru

“Bidhaa yetu ni ya asili, hatutumii kemikali zozote zile kuchakata,” anasema Triza.

Kilo nne za ndizi mbichi hutoa kilo moja ya kripsi. Wakati ndizi mbichi zinauzwa kati ya Sh100 hadi Sh200 kwa kilo, uchakataji huongeza thamani maradufu.

Pakiti ya gramu 160 huuzwa kwa Sh350, huku pakiti ndogo ikiuzwa Sh200.

Kripsi (chips) za plantain tayari kupakiwa. Picha|Sammy Waweru

Kripsi za Lynt’s Ltd zinapatikana kwenye maduka ya kijumla nchini.

“Soko lipo tayari na kwa kiwango kikubwa, lakini tumepenya karibu asilimia moja tu ya soko hilo,” anasema Lynn, ambaye ni Afisa Mkuu Mtendaji wa kampuni hiyo.

Maelezo hayo yanaashiria pengo kubwa lililosalia kwenye uchakataji na ambalo likiangaziwa litapiga jeki wakulima.

Triza Mwaniki akipakia ndizi za plantain. Picha|Sammy Waweru

Kupitia uongezaji thamani, hatua ya kina dada hao si tu ya kujipa mapato bali pia wanapunguza upotevu wa chakula na kuhakikisha wakulima wanapata soko la ndizi bila kukandamizwa na mabroka au mawakala.

Kulingana nao, ni hatua ambayo serikali na wadauhusika wakiikumbatia kikamilifu kwa karibu kila mimea na mazao italetea wakulima afueni. Isitoshe, uongezaji mazao thamani ni siri ya pesa kwenye kilimo na itakayosaidia kupiga jeki ukusanyaji pato la taifa (GDP).

Kripsi za Lynt’s Limited tayari kuingia sokoni. Picha|Sammy Waweru