Makala

Haya ndiyo matakwa yetu: Familia za waliouawa na polisi zasaka haki

Na NDUBI MOTURI June 21st, 2025 Kusoma ni dakika: 3

MWAKA mmoja baada ya maandamano dhidi ya serikali kusababisha vifo vya watoto wao, familia za waathiriwa zinasema ahadi zilizotolewa na Rais William Ruto na maafisa wa juu serikalini hazijatimizwa.

Familia hizo sasa zimepanga maandamano ya amani Juni 25 kudai haki.

Mnamo Julai 5, 2024, Bi Jacinta Ochieng alipokea simu kutoka kwa Mkuu wa Miradi Maalum ya Rais na Uchumi wa Ubunifu, Dennis Itumbi.

Simu hiyo haikudumu sana, na baada ya dakika chache za mazungumzo, Bw Itumbi alimfahamisha kuwa Rais angempigia simu muda mfupi baadaye.

Na kweli, dakika chache baadaye Rais alimpigia simu.

“Nilikuwa nyumbani na marafiki zangu, nikawaambia watulie, kisha nikawasha spika ya simu,” anakumbuka Bi Ochieng.

Rais baadaye aliomba msamaha kwa kauli zake za awali na akamfariji.

Pia, aliahidi kumwalika binafsi Ikulu ili kuhakikisha anapata haki kwa kifo cha mwanawe.

Lakini mwaka mmoja baadaye, Bi Ochieng anasema ahadi hiyo haijawahi kutimizwa. Juhudi zake za kutafuta haki kwa mwanawe zimegonga mwamba.

Wakati wa sherehe za Madaraka Day ambazo Rais Ruto aliongoza huko Homa Bay, Bi Ochieng alisababisha taharuki aliposimama mbele ya jukwaa kutaka kuzungumza.

Jana, mama huyo wa watoto wawili kwa machozi alisema kuwa njia pekee iliyosalia ni kuungana na akina mama wengine barabarani Juni 25 kudai haki.

“Singeweza kuvumilia alichokuwa anasema. Nilisimama na kudai haki kwa mwana wangu. Nilikuwa na maumivu moyoni na ndiyo sababu nilifanya hivyo,” aliambia Taifa Dijitali.

Huku taifa likikumbuka mwaka mmoja tangu tukio hilo, Bi Ochieng anasema hana matumaini atapata haki.

Jana, aliandamana na akina mama wengine kuwasilisha taarifa rasmi kwa serikali kuhusu maandamano ya amani yanayotarajiwa Juni 25.

Machozi yalitiririka, sauti zilitetemeka kwa huzuni huku familia zilizofiwa zikitoa wito wa haki mwaka mmoja baada ya wapendwa wao kuuawa katika maandamano ya Juni 25, 2024 jijini Nairobi.

Katika mkutano wa waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa kumbukumbu ya mlipuko wa bomu wa Agosti 7, akina mama waliovaa shuka nyeusi na kushika picha za wana wao waliopotea walishindwa kuficha huzuni.

Kila neno lililozungumzwa lilikuwa na uzito wa maumivu yasiyoweza kufichwa.

Familia hizo zinataka msamaha hadharani kutoka kwa Rais William Ruto kuhusu tukio la Juni 25, kukamatwa na kushtakiwa kwa polisi waliotajwa kuhusika, haki kwa familia zilizoachwa na majeraha ya kiakili na kijamii, pamoja na mabadiliko ya kina ndani ya polisi ili kukomesha mauaji ya kiholela na ukwepaji wa sheria.

Wameomba pia polisi kuwapa ulinzi wakati wa maandamano hayo ya amani.

“Kwa Huduma ya Polisi ya Taifa na mashirika mengine ya usalama, tunawaarifu rasmi. Haya ni maandamano ya amani yaliyo halali. Tunatarajia ushirikiano, utaalamu na ustahimilivu. Jaribio lolote la kuvuruga maombolezo yetu au kutumia nguvu dhidi ya mkutano wetu wa amani, litaongeza maumivu ya kitaifa. Kenya inatazama,” alisema Bi Meriwas.

Familia hizo zinatarajiwa kuweka maua kwenye maeneo muhimu jijini Nairobi ambapo watoto wao walipigwa risasi na kuuawa.

“Kisha tutaelekea kuwasilisha hati katika Bunge na Ofisi ya Rais. Hati hii si ombi. Ni takwa. Takwa la haki ambayo imecheleweshwa kwa muda mrefu. Takwa la hatua, si maneno. Takwa la utu wa binadamu, ambao watoto wetu walinyimwa walipokuwa hai na hata walipokufa,” waliongeza.

Kwa baadhi ya akina mama, imekuwa vigumu kuanza upya maisha yao.

Bi Maria Shikwe, mama wa Austin Makokha mwenye umri wa miaka 17, mtoto mwenye matatizo ya akili aliyepigwa risasi mjini Nakuru alisema hawezi kufanya chochote kwani mtoto wake mwingine pia ni mlemavu.

“Alikuwa ameenda kumchukua nduguye kumpeleka nyumbani kwa chakula cha mchana. Hakuwa sehemu ya waandamanaji, lakini aliuawa. Inaniumiza sana. Sasa siwezi kufanya kazi yoyote wala kuenda popote. Mimi sasa ni ombaomba,” alisema huku akilia.

Mary Muthoni, mama wa Kenneth Njeru mwenye umri wa miaka 20 aliyepigwa risasi karibu na bunge, alisema mwanawe hajawahi kupumzika kwa amani.

“Mwanangu hakuwa na hatia na hataweza kupumzika kwa amani hadi haki ipatikane. Ndiyo maana maandamano haya ni muhimu sana kwangu. Ni njia ya pekee iliyosalia kumkumbuka na kudai haki,” alisema.

Kwa Bi Gillian Munyao, safari ya kutafuta haki baada ya kifo cha mwanawe Rex Masai katika maandamano haijawa rahisi. Anasema mashahidi kadhaa waliokuwa wamekubali kuzungumza walijiondoa na kucheleweshwa kwa uchunguzi kunaendelea kufanya hali kuwa mbaya zaidi.

“Wengi wao wamejiondoa. Tuna hofu kwamba kutokana na ucheleweshaji huu, huenda tusipate haki kwa mtoto wetu,” aliongeza.

Bi Caroline Mutuku Mutisya, mama wa Erickson Mutisya aliyeuawa katika maandamano, alisema licha ya taarifa nyingi, hajapata msaada wowote.

“Alikuwa mwanangu, na kila mara ninapokumbuka asubuhi ile alipouawa, machozi hunitoka. Tumeenda kwa Chama cha Wanasheria Kenya, kwa IPOA, lakini hakuna kilichotokea,” alisema.

Bw Tom Mwadime, ambaye kaka yake Kelvin Mwawasi alipigwa risasi usiku Githurai 45, alisema familia yao imetatizika sana. “Mama yangu ni mgonjwa na hawezi hata kutembea. Ametafuta msaada ili tupate haki, lakini hakuna lolote limefanikiwa,” alisema Bw Mwadime.

Kwa Bw Daniel Otieno, aliyempoteza kaka yake Kelvin Odhiambo katika maandamano jijini Nairobi, kilichosalia ni kumbukumbu. Kwake, haki ni kupata majibu ya ni nani alimuua kaka yake siku hiyo.

“Kile tunachotaka ni haki tu na si kingine. Kaka yangu alikuwa na umri wa miaka 17 tu na aliuawa katikati mwa jiji la Nairobi. Kwa nini hawataki kutusaidia kupata haki?” aliambia Taifa Dijitali.