Hivi ndio waumini wa Legio Maria huzuru ‘Mecca’ yao iliyoko Mawego, Homa Bay
KILA mwaka Januari 24, maelfu ya waumini wa Kanisa la Legio Maria of African Church, hukongamana katika Kanisa la St Philips Rapar Mawego, Kaunti ya Homa Bay kwa maombi maalum.
Mahujaji hao hutumia nafasi hiyo pia kujenga imani yao na kukariri kujitolea kwao kuzingatia maadili na itikadi za kanisa hilo.
Waumini wa kanisa hilo lililoanzishwa miaka ya 1960 huamini kuwa maombi yanayofanywa katika St Philip Rapar kila mwaka ni maalum kwani huwafanya kuwa karibu na mbinguni.
Kwao wanarejelea kanisa hilo la Mawego kama “Dho ranga Polo” (yaani lango la Mbinguni, kwa dholuo).
Sawa na Waislamu ambao husafiri hadi Mecca kwa Haji kila mwaka kama mojawapo ya nguzo tano za dini hiyo, waumini wa kanisa la Legion Maria of African Church hufika Mawego kila mwaka kujenga imani yao kiroho.
Asili ya kongamano hilo la siku moja, kila mwaka, ni amri iliyotolewa na mwanzilishi wa kanisa hilo Baba Simeon Melchior Masihi Ondeto.
Aliwaagiza wafuasi wake wawe wakikutana Mawego kila mwaka kwa maombi.
Kama ishara ya kutii agizo hilo, waumini huweka kando shughuli zao zote za kiuchumi na kufika eneo hilo kutafuta lishe ya kiroho.
Baba Ondeto alitoa agizo hilo baada ya kuzuru Mawego mnamo Januari 24, 1967. Kama hangefanya ziara hiyo, Kanisa la St Philip Rapar lingesalia tu mahala pa kawaida pa kuabudu, lisilo tofauti na maeneo mengine.
Lakini ajali umbali wa kilomita moja kutoka kanisa hilo ilibadilisha historia ya kanisa hilo na kugeuza Mawego kuwa eneo takatifu.
Mnamo Januari 24, 1967 jioni Simeon alikuwa amehudhuria mazishi ya Mama Mtakatifu, mmoja wa waumini wa kanisa hilo.
Alikuwa katika eneo la Ondhoya kabla ya kuelekea Got Calvary (Got Kwer iliyoko Suna, Migori)- mahala patakatifu kwa kanisa hilo. Hapo ndipo hatimaye Simeon alizikwa.
Kutoka hapo alielekea Jerusalem, eneo la Kadem, ambako aliishi kwa muda mfupo kabla ya kuendelea na safari hadi Nazareth na hatimaye Kadhola.
Kulingana na Kasisi wa St Philip Rapar Mawego Gabriel Christopher Owino, Baba Simeon aliandamana na Kadinali Clemence Ange, dereva wake, Mama Susana Dira Ouma, Dalmas Oyier, Peter Okello Mumbo na Priska Nyar Okello na walikuwa wakisafiri kwa gari aina ya saloon.
Awali, kundi hilo lilipanga kusafiri moja kwa moja kutoka Migori hadi Kisumu, lakini akaamua kupita Mawego katika Homa Bay.
“Baba alitaka kutembelea mmoja wa mafundi wake wa nguo aliyeishi Mawego. Alijulikana kama Lucas,” Kasisi Gabriel akasema.
Safari kutoka Migori ilikuwa shwari hadi gari lao lilipokaribia Kanisa la St Philip Rapar.
Ilikuwa ni karibu saa nne za usiku na barabara kati ya Kendu Bay na Mawego ilikuwa katika hali mbaya.
Kasisi Clemence Ange alipokuwa akiendesha alipoteza udhibiti wa gari na likagonga mwamba mkubwa kando mwa barabara.
Kasisi Gabriel anaeleza kuwa dereva aliripotiwa kumwona Baba Simeon akiwa amesimama katikati mwa barabara ilhali kiongozi huyo alikuwa ameketi katika kiti cha abiria.
“Ghafla aligeuza gari ili asimgonge Baba, baada ya kuchanganyikiwa na kile alichokiona. Gari hilo liligonga mwamba na kusimama,” kasisi huyo akaeleza.
Ajali hiyo ilimsababishia Baba Simeon majeraha mdomoni na meno kadhaa yakang’oka. Safari ya Kisumu ilikatizwa. Habari kuhusu ajali hiyo ilifika haraka katika kanisa la St Philip Rapar.
Waumini waliacha kile walikuwa wakifanya na kuelekea katika eneo la tukio, umbali wa kilomita moja kutoka huko.
Waliwasaidia abiria kuondoka kwenye gari hilo na wakambeba Baba Simeon hadi katika kanisa hilo.