Makala

Imekuwa maneno matupu bila matendo kumaliza ufisadi

Na CHARLES WASONGA June 17th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

LICHA ya kutoa ahadi nyingi namna serikali yake ingepambana na jinamizi la ufisadi, Rais William Ruto hajafanikiwa kutokomeza uovu huo tangu Septemba 13, 2022 alipoingia mamlakani.

Ulegevu wa serikali ya Kenya Kwanza katika vita dhidi ya ufisadi ndio mojawapo ya masuala yaliyochochea maandamano yaliyoitishwa na viongozi wa upinzani mapema mwaka wa 2023 na vijana  wa Gen Z mnamo Juni na Julai 2024.

Ripoti ya kamati ya kitaifa ya mazungumzo (NADCO) iliyotolewa wazi mnamo Novemba 23, 2023 imependekeza kwamba serikali iziwezesha zaidi kifedha taasisi za kupambana na ufisadi nchini kama vile Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC), Mdhibiti wa Bajeti (CoB) miongoni mwa zingine.

Hata hivyo, hilo halifanyika kwani asasi kama EACC imekuwa ikilalamikia uhaba wa fedha za kuiwezesha kuajiri wapelelezi zaidi wa sakata za ufisadi.

“Ufinyu wa fedha ni mojawapo ya changamoto zinazotusibu kama tume. Hii ndio maana chunguzi kuhusu baadhi ya kesi za ufisadi zinazowasilishwa mbele yetu huchukua muda mrefu kukamilishwa. Hata hivyo, tumepiga hatua kubwa katika kukomboa mali ya umma iliyoibwa kwani tangu Januari 2023 tumekomboa mali ya thamani ya Sh2.8 bilioni,” mwenyekiti wa EACC David Oginde akasema mnamo Januari 3, mwaka huu alipotoa ripoti kuhusu utendakazi wa tume hiyo.

Katika mwaka wa kifedha wa 2025/2026, EACC imetengewa Sh4.2 bilioni kama mgao wa bajeti, fedha ambazo tume hiyo inasema haziwezi kutosha kufadhili majukumu yake.

“Kwa mfano, kila moja ya afisi zetu za kikanda inayo wachunguzi watano na maafisa wawili wa kisheria. Kila afisi inahitaji angalau wapelelezi 10 lakini hilo halijawezekana kutokana na uhaba wa fedha za kuwaajiri maafisa zaidi,” Kasisi Oginde akaeleza.

Ni kutokana na uhaba huu wa fedha ambapo Afisa Mkuu Mtendaji wa EACC Abdi Mohamud wiki jana alipendekeza kwamba sheria ya tume hiyo ifanyiwe marekebisho ili kuipa nafasi ya kutumia sehemu ya fedha na mali nyinginezo za ufisadi inayokomboa.

“Tume hii imekuwa ikikomboa kiasi kikubwa cha mali kutokana na kesi za ufisadi, ilhali tunakumbwa na changamoto kubwa ya kifedha. Ikiwa tutahifadhi sehemu fulani ya mali tunayokomboa, tunaweza kuimarisha uwezo wetu wa kutekeleza majukumu yetu,” Bw Abdi akaiambia Kamati ya Seneti kuhusu Uhasibu wa Pesa za Umma (CPAIC) inayoongozwa na Seneta wa Homa Bay Moses Kajwang’.

Kulingana na afisa huyo, ikiwa pendekezo hilo linaweza kupitishwa, katika marekebisho ya sheria, bajeti ya EACC inaweza kupanda kwa angalau Sh2.5 bilioni kila mwaka, pesa ambazo zitaiwezesha kuajira maafisa zaidi.

Baada ya maandamano ya vijana wa Gen Z mwaka jana, Rais Ruto aliahisi kuwa serikali ya ingepiga jeki vita dhidi ya ufisadi kwa kuongeza ufadhili kwa asasi za kuendesha mchakato huo.

Kikao na wanahabari katika Ikulu ya Nairobi mnamo Julai 15, kiongozi wa taifa pia aliahidi serikali yake itaifanyia marekebisho Sheria kuhusu Utoaji wa Ushahidi, Kanuni za Kushughulikia Kesi za Uhalifu, miongoni mwa mabadiliko mengine, ili kuwezesha kukamilishwa kwa kesi za ufisadi ndani ya miezi sita.

Vilee vile, Dkt Ruto aliahidi kuwa serikali yake ingependekeza mabadiliko kadhaa yafanyiwe Sheria ya Kuwalinda Mashahidi ili kuwapa ulinzi zaidi na moyo wa kufichua sakata za ufisadi.

“Hii itaimarisha ulinzi kwa Wakenya wazalendo wanaofichua visa vya ufisadi na kuwapa moyo wengine kujitokeza na kuwaanika waovu hao,” Dkt Ruto akasema.

Ili kuzima mianya ya wizi wa pesa za umma kupitia ununuzi wa bidhaa na huduma serikali, Rais Ruto alipendekeza kuimarishwa kwa mfumo wa utoaji zabuni za serikali kupitia ukumbatiaji wa teknolojia ya kisasa.

“Ili kufikia hilo serikali yangu itapendekeza marekebisho kadhaa yafanyiwe Sheria ya Usimamizi wa Pesa za Umma na Sheria ya Ununuzi wa Umma ndani ya siku 90 zijazo,” akaeleza.

Isitoshe, Rais Ruto alipiga marufuku mwenendo wa maafisa wa serikali, wakiwemo wabunge na maseneto kushiriki michango ya kuchanga pesa.

“Kwa hivyo, nimemwagiza Mwanasheria Mkuu  kuandaa Mswada wa sheria kudhibiti harambee ili ilisitumiwe kuendeleza ufisadi na wizi wa pesa za umam”, akaeleza.

Lakini tangu wakati huo, mswada huo haujawasilishwa bungeni na Rais Ruto mwenyewe amekuwa mstari wa mbele kuchanga mamilioni ya fedha haswa kufadhili miradi mbalimbali makanisani.

Kulingana na aliyekuwa Afisa Mkuu Mtendaji wa Shirika la Kimataifa la Kupambana na Ufisadi (TI), tawi la Kenya Samuel Kimeu, serikali ya Kenya Kwanza haina nia na msukumo wa kupambana na jinamizi la ufisadi.

“Utosefu wa nia ya kisiasa kutoka ngazi ya juu katika utawala huu ndio kikwazo kikubwa katika vita dhidi ufisadi. Kenya inayosheria nyingi na asasi za kutosha kuendesha mchakato wa kupambana na uovu lakini serikali ya sasa haijaziwesha ipasavyo. Rais Ruto mwenyewe hutoa ahadi nyingi kuhusu suala hilo lakini anachelea kuzitimiza,” Bw Kimeu anaeleza.