Azimio la Umoja kugeuka ‘Komboa Kenya Alliance’
MUUNGANO wa upinzani nchini umeanza kuchukua sura mpya baada ya kuibuka kwa pendekezo la kubadilisha jina la Azimio la Umoja kuwa “Komboa Kenya Alliance”.
Hatua hii inalenga kuimarisha nguvu za kisiasa dhidi ya Rais William Ruto kabla uchaguzi mkuu wa 2027.
Hatua hiyo, kwa mujibu wa duru za ndani, inalenga kukwepa changamoto za kisheria zinazoweza kutokea iwapo vyama vitahitajika kusajili muungano mpya kutoka mwanzo.
Badala yake viongozi wanapendekeza kutumia muungano uliopo wa Azimio la Umoja kama msingi, kisha kuubadilisha jina na muundo wake ili kuendana na hali ya sasa ya kisiasa.
Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka alithibitisha kuwepo kwa mazungumzo hayo katika mahojiano kwenye runinga ya Citizen TV akisema: “Kuna pendekezo mezani la kubadilisha Azimio. Napendekeza iwe Komboa Kenya ili kuleta nguvu zote za upinzani chini ya mwavuli mmoja.”
Aliongeza kuwa hatua hiyo inalenga kuharakisha maandalizi ya kampeni bila kupoteza muda mwingi katika taratibu za usajili, huku akisisitiza umuhimu wa upinzani kuungana.
Duru zinaeleza kuwa mojawapo ya sababu kuu ya mkakati huo ni hofu kwamba serikali ya sasa inaweza kuweka vizingiti katika usajili wa muungano mpya wa upinzani, jambo ambalo linaweza kuchelewesha au hata kudhoofisha mipango yao ya kisiasa.
Kwa kutumia muundo uliopo, upinzani utaweza kujipanga haraka na kuanza mikakati ya kampeni mapema.
Aidha, mabadiliko hayo yanatarajiwa kufungua mlango kwa vyama vilivyokuwa vimejiondoa kurejea katika muungano huo.
Chama cha People’s Liberation Party (PLP) chake Martha Karua kinatajwa kuwa miongoni mwa vile ambavyo vinaweza kurejea, huku kile cha Democracy for Citizens Party (DCP) kinachoongozwa na Rigathi Gachagua kikitarajiwa kujiunga upya.
Karua yupo katika muungano wa sasa wa upinzani.
Hatua hii pia inaonekana kuungwa mkono kimyakimya na Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, ambaye amekuwa akifanya juhudi za kufufua Azimio na kuleta pamoja viongozi wa upinzani.
Wachambuzi wanasema Kenyatta anajaribu kujenga muungano pana wa kisiasa utakaomenyana na serikali ya sasa ya Rais Ruto.
Mapema Februari Kenyatta alimteua Kalonzo kuwa kiongozi wa Azimio baada ya kifo cha Raila Odinga, huku akitema viongozi wa ODM wanaounga Serikali Jumuishi.
Mchanganuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki asema kwamba kubadilishwa kwa jina la muungano ni mkakati wenye uzito mkubwa.
“Haya si tu mabadiliko ya jina. Ni juhudi za kuunda taswira mpya itakayovutia wapigakura na kuunganisha vyama,” anaeleza.
Naye mchanganuzi Peter Katana anahoji kwamba mafanikio ya muungano huo yatategemea zaidi umoja wa viongozi kuliko jina.
“Jina linaweza kusaidia kisiasa, lakini kilicho muhimu ni kama viongozi wataweka kando maslahi ya kibinafsi na kufanya kazi pamoja kwa lengo moja,” alisema.
Dkt Katana anaongeza kuwa iwapo vyama kama DCP na PLP vitaungana na Azimio chini ya mwavuli mpya, basi upinzani unaweza kupata nguvu mpya.
Vyama vingine vikuu katika muungano huo ni Jubilee kinachoongozwa na Uhuru Kenyatta ambacho mgombea urais wake ni Uhuru, Wiper cha Musyoka, PNU chini ya uongozi wa Peter Munya ambacho kinaunga Jubilee katika urais, DP kinachoongozwa na Justin Muturi na DAP- Kenya cha Eugene Wamalwa.
Zaidi ya hayo, hatua ya kubadili jina inalenga pia kuvutia kizazi kipya cha wapiga kura, hasa vijana ambao wamekuwa wakitaka mwelekeo mpya wa kisiasa unaojali ajira, gharama ya maisha na uwajibikaji wa viongozi.
Wachambuzi wanasema jina “Komboa Kenya” lina ujumbe wa moja kwa moja unaolenga kuvutia wananchi wanaohisi kukandamizwa na hali ya sasa ya uchumi.
Hata hivyo, kuna changamoto zinazoweza kujitokeza, ikiwemo ushindani wa uongozi ndani ya muungano huo na suala la mgombea mmoja wa urais.
Baadhi ya wachambuzi wanasema kuwa bila mkakati wazi wa kushughulikia masuala hayo mapema, muungano huo unaweza kukumbwa na migawanyiko ya ndani.
Pia, kuna haja ya kuunda sera thabiti zitakazowashawishi Wakenya kuwa muungano huo ni mbadala halisi wa uongozi wa sasa.
Licha ya changamoto hizo, pendekezo la Komboa Kenya Alliance linaonekana kuleta matumaini mapya kwa wafuasi wa upinzani wanaotaka kuona umoja na mwelekeo mpya wa kisiasa.
Iwapo mpango huo utafanikiwa, unaweza kubadilisha kwa kiasi kikubwa siasa za Kenya kuelekea uchaguzi wa 2027, huku ukitoa changamoto kubwa kwa utawala wa Rais Ruto.
Muungano huo mpya unalenga kujiwasilisha kama jukwaa mbadala la uongozi, likiahidi kushughulikia changamoto za kiuchumi na kijamii zinazowakabili Wakenya.