Chama tawala UDA chageuka nyumba ya mizozo hesabu za 2027 zikiumiza vichwa
CHAMA tawala cha United Democratic Alliance (UDA) kinachoongozwa na Rais William Ruto kimeandamwa na mivutano ya ndani, mizozo ya uongozi, na vita vya kisiasa vinavyoashiria vita baridi kuelekea uchaguzi wa 2027.
Kilipotwaa madaraka mwaka wa 2022, UDA kilijitokeza kama chama kilichokuwa na umoja na maono ya kubadilisha nchi.
Hata hivyo, miaka michache baadaye, hali imebadilika kwa kasi. Malumbano ya hadharani miongoni mwa viongozi wa juu wa chama, vitendo vya kuhujumiana kisiasa, na mikutano ya siri imeonyesha kuwa UDA ni nyumba ya mizozo na ubabe.
Tukio la hivi punde zaidi ni mvutano baina ya Naibu Rais Prof Kithure Kindiki na Gavana wa Embu Cecily Mbarire, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kitaifa wa UDA. Mbarire, kwa hasira, alilalamikia hadharani njama za baadhi ya maafisa wa serikali kuu kumhujumu kisiasa.
Akihutubu katika sherehe za Madaraka Dei, Mbarire alilalamika kuwa viongozi fulani serikalini wanapanga mikutano ya usiku Embu bila kuwashirikisha viongozi waliochaguliwa.
Unajua mimi ni mwenyekiti wa Chama cha UDA, na kama kuna mtu aliyeteseka kwa sababu ya kuunga mkono serikali, ni mimi.
Aliongeza kuwa maafisa wa serikali wamekuwa wakisafiri kutoka Nairobi hadi Embu usiku kwa mikutano ya siri, kuendeleza njama yao kwa kushirikiana na viongozi wa mashinani bila kumfahamisha.
“Tulizunguka Embu yote pamoja na Madiwani na Naibu wangu, tukiwaomba watu waunga mkono serikali ili wanufaike, na sasa mnatoka Nairobi kuja kuvuruga Embu.
“Sitakubali hilo. Ninyi wenyewe mnajua. Nawathubutu mrudi Embu tena. Tutashughulikia kila mtu mmoja kwa mmoja. Mimi ni kiongozi aliyechaguliwa na watu wa Kaunti ya Embu, na mtaniheshimu,” alisema.
Ni hali ambayo ilizua maswali mengi kuhusu usimamizi wa chama hicho. Mkutano wa dharura kati ya Mbarire na Kindiki uliofanyika jana Karen, Nairobi, ulionekana kama juhudi za kutuliza joto la kisiasa, lakini hali halisi imeonyesha kuwa ufa wa kisiasa umeanza kupanuka.
Seneta wa Kakamega, Boni Khalwale, alijitokeza kufichua hali halisi ya kisiasa ndani ya UDA. Kupitia mitandao ya kijamii, alieleza kuwa Mbarire si wa kwanza kuhisi kutengwa, akimkumbusha kuwa yeye pamoja na Johnson Muthama walitengwa awali licha ya kuwa waanzilishi wa chama.
“Gavana Mbarire, hivyo ndivyo mambo huwa. Usilie; zoea,” alisema Dkt Khalwale.
Kulingana na seneta huyo, tatizo la migogoro ya ndani katika UDA halikuanza na masaibu na Mbarire. Licha ya mwenyekiti huyo kulalamika, mtangulizi wake Muthama, aliondolewa kimya kimya baada ya uchaguzi wa 2022, na Cleophas Malala akateuliwa Katibu Mkuu kwa kile seneta huyo alitaja kama kumpa yeye (Khalwale) funzo.
Muthama ambaye kwa sasa ni kamishna katika tume ya huduma ya bunge alisisitiza uaminifu wake kwa chama na Rais William Ruto.
Bw Malala alitemwa kufuatia ukuruba wake na aliyekuwa naibu kiongozi wa chama Rigathi Gachagua ambaye baadaye alitofautiana na kiongozi wa chama, Rais Ruto na akatimuliwa serikalini kupitia mchakato wa bunge. Kwa sasa, Gachagua na Malala wameungana katika chama cha DCP.
Ziara ya ghafla ya Naibu Rais Kindiki Embu bila kushirikisha viongozi wa eneo hilo, wakiwemo maafisa wa kaunti na hata Gavana Mbarire, ilianika zaidi mizozo ndani ya chama tawala.
Kwa mara ya kwanza, viongozi wa Embu walionekana kushangazwa na ujio wa afisa wa juu wa serikali. Hata Seneta wa Embu, Alexander Mundigi, aliyekuwa pamoja na naibu rais, hakupata fursa ya kuhutubia umma, tukio lisilo la kawaida kwa kiongozi wa hadhi yake.
Wachambuzi wa siasa wanasema ni wazi viongozi wakuu wa chama hawazungumzi kwa sauti moja, kutatua tofauti zao kwa njia za ndani, hatua ambayo inaweka UDA katika hatari.