Jicho Pevu: Hofu misimamo yake mikali itamkosesha ugavana 2027
MBUNGE wa Nyali Mohammed Ali maarufu kama ‘Jicho Pevu’ amejitokeza kugombea kiti cha ugavana Kaunti ya Mombasa lakini ni mbunge wa kipekee aliye na mwelekeo tofauti na wenzake watano wa kaunti hiyo.
Huku viongozi wote wa Mombasa wakijitokeza kuunga mkono Rais William Ruto kwa muhula wa pili, Bw Ali licha ya kuchaguliwa kwa nafasi hiyo kwa muhula pili kwa tiketi ya UDA, anaonekana kuchukua mwelekeo tofauti na wenzake na kuwa upande wa upinzani.
Lakini hii si mara ya kwanza Bw Ali kuonekana kuwa na msimamo tofauti na wanasiasa wenzake eneo hilo kwani mwaka wa 2022, huku kila mwanasiasa alipokuwa akiimba ODM, mbunge huyo alishinda kupitia UDA chama kilichokikashifiwa vikali.
Vivyo hivyo, mwaka wa 2017, aliponyimwa tiketi ya ODM, alijitosa uwanjani kama mgombeaji huru na kuibuka mshindi licha ya kupingwa na wawaniaji wote wa ODM.
Suala ibuka ni iwapo msururu wa ushindi ambao amekuwa akipata licha ya msimamo wake mkali ya kisiasa utaendelea kushuhudiwa 2027.
Licha ya wengi kumuona Bw Ali kama mtaalamu wa mikakati ya kisiasa ambaye hajakosa shabaha kwani kugombea kiti cha Nyali alikumbana na changamoto si haba lakini akafaulu kushikilia kiti hicho kwa mihula miwili.
Hata hivyo, ni wazi kwamba mawimbi ya kiti cha ugavana kinahitaji uwezo mkubwa na hivyo ni lazima akaze kamba.
“Jicho Pevu ameweza kupigana na vita kwani alipotaka kiti cha Nyali, aliyekuwa gavana wa Mombasa enzi hizo ambaye sasa ni Waziri wa Madini na Uchumi wa Baharini Ali Hassan Joho, alichangia kumnyima tiketi na kumpa mmoja wa jamaa yao Bw Saidi Abdalla maarufu kama Saido lakini akamwangusha debeni, lakini kwenye kiti cha ugavana ni lazima aweke mikakati kabambe ili kukitwaa” akasema Bw Hamisi Mboya, mkazi wa Nyali.
Bw Ali hata hivyo, anatarajia kukumbana na upinzani mkali kwani wabunge, seneta na viongozi wengine wakiongozwa na Bw Joho wameanzisha kampeni kali ya kuunga mkono Rais Ruto.
Hivi majuzi akielezea sababu za kujitenga na wenzake, alisema, “Simba hatembei na kondoo, na jogoo hatembei na vifaranga,” akihalalisha kutohudhuria vikao vya viongozi wa Pwani ambao hivi karibuni walitangaza kumuunga mkono Rais Ruto.
Licha ya hayo yote, Mbunge huyo anaamini kwamba maendeleo aliyoleta katika eneo bunge la Nyali pamoja na uongozi wa uaminifu aliodhihirisha utachangia pakubwa katika kampeni zake za ugavana mwaka wa 2027.
“Tangu uhuru, viongozi wetu hawajawahi kuwekeza katika elimu. Waliwekeza katika anasa. Badala ya kuwapeleka watoto wa maskini shuleni ili wabadilishe maisha yao na kuketi kwenye meza ya ajira pamoja na watoto wa matajiri, waliamua kuwaletea dera, leso na pakiti za unga ili kuua kizazi chenu,” alisema Ali.
Amesema aliposhinda ubunge mnamo 2017, eneobunge la Nyali lilikuwa na shule moja tu ya upili ya umma.
“Leo, Nyali ina zaidi ya shule 15, zikiwemo Mwembeni, Kongowea, Kengeleni na Pentrose,” alisema.
Kwa sasa amesema pia anashirikiana na vuguvugu la viongozi vijana akiwemo mbunge wa Embakasi Mashariki, Bw Babu Owino, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na viongozi wanaotaka kukomboa Kenya.
“Viongozi wetu ni wa kuleta leso, madera na pakiti za unga. Endeleeni kuzipokea kwa sababu ni mali yenu. Kuleni hivyo vitu wanavyowaletea lakini kura mnipe mimi kwani kiti cha Mombasa si cha urithi au jamii fulani,” alisema Bw Ali.
Katika kinyang’anyiro hicho, Bw Ali anatarajiwa kupigana na Gavana wa sasa ambaye pia ni Naibu kinara wa ODM Abdulswamad Nassir, aliyekuwa mbunge wa Kisauni Ali Mbogo, Bunge la Afrika Mashariki (EALA) Hassan Omar na mwenzake Suleiman Shahbal.
Hata hivyo, ndoa ya ODM na UDA katika serikali ya muungano inaonekana kuendelea kugawanya chama cha ODM kote nchini kwani chama cha UDA kimeweza kutumia ushirikiano wao wa serikali ya muungano kuvunja ngome za ODM jambo ambalo Bw ali anategemea kutumia kujizolea ushindi.
Katika uchaguzi mkuu uliopita, Bw ali aliongoza wanasiasa wa UDA na kujizolea zaidi ya asilimia 40 ya kura Kaunti ya Mombasa licha ya kupingwa na wanasiasa wengine watano, jambo ambalo lilionekana si la kawaida kwani kwa miaka 15 kabla uchaguzi huo, ODM imekuwa ikiongoza kwa kura zaidi ya asilimia 85.