Kalonzo aanza kutumia mbinu maarufu za Raila
KIONGOZI wa Chama cha Wiper, Bw Kalonzo Musyoka, ameanza kuonyesha dalili za kufuata nyayo za aliyekuwa Waziri Mkuu, Bw Raila Odinga, katika kuongoza upinzani.
Bw Musyoka, ambaye alijitangaza kiongozi wa upinzani na hivyo kuvaa viatu vya kisiasa vya Bw Odinga wakati kiongozi huyo wa ODM alipojiunga na Rais William Ruto, ameanza kuvumisha siasa kama zile zilizokuwa zikitoka kwa Bw Odinga awali.
Katika ziara yake Pwani wikendi, Bw Musyoka na wenzake akiwamo aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua, alitangaza sikukuu ya kumbukumbu ya vijana waliouawa na polisi wakati wa maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha mwaka uliopita.
Huu ni mfumo ambao Bw Odinga alizoesha wafuasi wake wakati alikuwa kiongozi wa upinzani.
Vilevile, Bw Musyoka ametangaza maandamano mnamo Juni 25 akiwarai vijana na Wakenya wengine kuelekea hadi katika Bunge la Taifa na kuweka mishumaa kama kumbukumbu ya wale waliouwawa mwaka jana.
“Huu ndio wakati wa kusawazisha mambo. Ifikapo Juni 25, tunataka kuona hata kanisa pia likitenga muda ili sote twende hadi katika lango la Bunge. Wakenya wanafaa waende hapo kuwasha mishumaa na kuomba ili shetani aondoke pale kwa sababu damu ya watoto wetu ilimwagika pale. Tutawasha tu mishumaa nje ya Bunge,” akasema, akiwa kanisani Malindi, Kaunti ya Kilifi.
Bw Musyoka ambaye alikuwa mgombea mwenza wa Bw Odinga kwenye uchaguzi wa urais 2013 na 2017, anaonekana kufuata nyayo za Bw Odinga ili kuwa mpinzani mkali wa kumwondoa mamlakani Rais Ruto.
Sawa na jinsi Bw Odinga alivyokuwa akifanya awali, Bw Musyoka ameungana na viongozi mbalimbali ambao kwa pamoja wanatafuta ufuasi wa mapema katika pembe tofauti za nchi kabla Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Alisema mwaka jana wakati vijana walipovamia bunge hilo, wabunge ambao kazi yao ni ‘kumuabudu’ Rais walitoroka kwa kutumia handaki maalumu.
“Wakenya walikuwa wamechoka na hali ngumu hasa kupandishwa kwa ushuru. Wakenya walikuwa wamesema kufa dereva kufa makanga, walisema kama Rais Ruto anataka kumuondoa Naibu wake ambaye walichaguliwa pamoja basi walifaa waondoke pamoja,” alisema Bw Musyoka.
Sawa na mtindo wa Bw Odinga, makamu huyo wa rais wa zamani anatafuta uungwaji mkono wa vijana, huku akikosoa vikali serikali kwa uongozi mbaya.
Alisema vijana wa humu nchini walianzisha vuguvugu ambalo litahakikisha Rais anahudumu kwa muhula mmoja pekee.
Bw Musyoka alisema baada ya uchaguzi mkuu wa Agosti 2022, upinzani uliokuwa ukiongozwa na Bw Odinga, Martha Karua, Eugene Wamalwa pamoja naye ulikuwa sauti ya wanyonge.
Hata hivyo, Bw Odinga aliamua kujiunga na serikali ya Kenya Kwanza.
Alisema alisimama kidete na Bw Odinga ambaye ‘alisaliti’ Wakenya kwa kujiunga na serikali ya Bw Ruto.
“Nilimuuliza Bw Odinga kwa nini akubali kujiunga na serikali ambayo ina damu ya watoto wetu. Nilisimama naye kwa kipindi cha miaka 15. Nilikataa kuungana na serikali kwa sababu ya damu ya vijana wetu iliyomwagwa,” alisema Bw Musyoka.
Alisema mpaka sasa hakuna mtu ambaye alikamatwa na hata kuhukumiwa kutokana na vifo vya vijana.
“Mnamo Juni 25 itakuwa siku ya vijana waliouawa, hakuna kufanya kazi,” akaongeza.
Aliwasihi vijana wasake vitambulisho, kujiandikisha kuwa wapigakura na kujiunga na chama chake ili kumuondoa Bw Ruto mamlakani.
Alisema ataandika barua kwa msajili wa watu kutaka kujua ni vijana wangapi wamepewa vitambulisho kuanzia mwaka jana.