Kelele za wanasiasa mazishini zatatiza wafu
Wakati J. M. Kariuki alipouawa Machi 1975, mbunge wa Kajiado Kaskazini wakati huo, John Keen alitamka maneno yaliyoakisi hisia za taifa; “Fisi wamekula mmoja wao.” Kauli hiyo ilikuwa shambulizi la moja kwa moja kwa mtandao wa wanasiasa wa Kiambu uliokuwa karibu na Rais Jomo Kenyatta. Keen alitamka kile ambacho wengi walihisim kwamba Kariuki hakufa mikononi mwa wageni, bali watu waliokuwa ndani ya mfumo.
Katika mazishi ya mbunge wa Ol Kalou David Kiaraho wiki iliyopita, Seneta wa Nyandarua John Methu aligeuza jukwaa la maombolezo kuwa la siasa alipomwambia Rais William Ruto kuwa anamheshimu lakini hamuogopi. Wakati huo huo, aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua alitumia fursa hiyo kumkosoa rais. Kwa ghafla, mazishi yakageuka uwanja wa siasa—kama ilivyotarajiwa.
Ili kuelewa hali hii, ni lazima kurejea enzi ambazo serikali ilibana demokrasia. Katika mazingira hayo, mazishi yalikuwa mojawapo ya majukwaa machache ya kujieleza. Mfano wa kwanza ulionekana wakati wa mazishi ya Pio Gama Pinto mwaka 1965. Oginga Odinga alitumia jukwaa hilo kuikosoa serikali ya Kenyatta na kuonya kuhusu waliokuwa wakilinda maslahi ya kibepari.
Baadaye, mgawanyiko kati ya Kenyatta na Odinga ulipozaa Kenya People’s Union mwaka 1966, upinzani ulilazimika kutafuta majukwaa mbadala. Serikali ilizuia mikutano na shughuli za kisiasa, na hivyo mazishi yakageuka “bunge mbadala” la wananchi.
Kifo cha Tom Mboya mwaka 1969 kilizidisha hali hiyo. Mazishi yake hayakuwa ya kawaida, yalikuwa ya hasira, mashaka na ghasia. Hata Daniel arap Moi alipigwa mawe na waombolezaji. Kuanzia hapo, ilidhihirika kuwa pale siasa zinapogeuka hatari, mazishi hayawezi kubaki ya kifamilia pekee.
Hali hiyo iliendelea hadi enzi za Moi, ambapo mateso, kizuizi na ukandamizaji vilikuwa kawaida. Kifo cha Robert Ouko kilifichua hofu iliyotanda ndani ya serikali. Mazishi yake yalikuwa ya ulinzi mkali lakini pia lawama na maswali zilitawala.
Katika mazishi ya Oginga Odinga mwaka 1994, James Orengo alimkabili Moi hadharani, akimshutumu kwa unafiki. Tukio hilo lilionyesha kuwa mazishi yalikuwa nafasi ya kusema yale ambayo hayangeweza kusemwa kwingine.
Hata wakati huu, hali hiyo inaendelea. Tukio la mwaka 2025 ambapo ujumbe wa rambirambi wa Rais Ruto ulikataliwa hadharani kaunti ya Embu linaonyesha mwendelezo wa utamaduni huu.
Hivyo basi, Methu na Gachagua hawakuwa wakibuni jambo jipya, walikuwa wakifuata mkondo wa historia ndefu. Mazishi nchini Kenya yamegeuka jukwaa la kisiasa kwa sababu mara nyingi ndiko pekee ukweli unaweza kusemwa bila kubanwa.
Historia inaonyesha wazi kuwa pale ambapo siasa zinabanwa, hata kaburi hugeuka jukwaa la mapambano ya kisiasa.