Kenyatta alivyoandaa Moi kutwaa urais baada yake
DANIEL Toroitich arap Moi alizaliwa Septemba 2 mwaka wa 1924, katika kijiji cha Kurieng’wo, Sacho, wilayani Baringo (Kaunti ya Baringo kwa wakati huu).
Alikuwa mwana wa tano wa mke wa kwanza wa baba yake. Moi alipewa jina Toroitich, linalomaanisha “karibisha mifugo nyumbani”, ishara ya jukumu muhimu ambalo mifugo hutekeleza katika utamaduni wa jamii yake.
Baba ya Moi alifariki wakati yeye (Moi) alikuwa na umri wa miaka minne na kaka yake, Tuitoek, akawa mlezi wake.
Ni Tuitoek aliyemshawishi Moi kuenda shuleni akiwa na umri mdogo ili aepuke umaskini na dhuluma za kikoloni.Mnamo 1934, Moi alianza masomo katika shule ya Africa Inland Mission, Kabartonjo, takriban kilomita 45 kutoka nyumbani kwao.
Mnamo Oktoba 20, 1936, alibatizwa na kuitwa Daniel. Mnamo 1938, alihamishiwa shule ya African Inland Mission, Kapsabet na baadaye shule ya African School Kapsabet, ambapo alikuwa kiranja mkuu na nahodha wa timu ya soka.
Alifanya kazi za vibarua akiwa shuleni na nje ya shule ili kukimu mahitaji yake ya kimsingi.Mnamo 1945, Moi alichaguliwa kujiunga na shule ya upili ya Alliance lakini, kwa masikitiko, serikali ya kikoloni haikumruhusu. Badala yake, alitumwa chuo cha mafunzo ya ualimu.
Maswali yamekuwa yakiulizwa: Kwa nini serikali ya kikoloni ilimnyima Moi nafasi muhimu ya kusomea Alliance? Ni nini walikuwa wameona ndani yake?Alipomaliza mafunzo ya ualimu, alitumwa Kabarnet kuwa mwalimu mkuu.
Alisoma kibinafsi na kufuzu mtihani wa London Matriculation Examinations. Mnamo 1949, alipandishwa cheo na kuwa mwalimu wa kiwango cha P2 baada ya kozi fupi katika chuo cha mafunzo ya ualimu cha Kagumo.
Alihamishwa hadi Tambach Government African School kama mwalimu wa walimu. Moi alimuoa Helena (Lena) Bomet mwaka wa 1950 na kujaliwa watoto wanane – mabinti watatu na wavulana watano.Mnamo 1950 alihudhuria mafunzo katika Jeans School (sasa inajulikana kama Kenya School of Goverment) na baadaye akatumwa kufanya kazi Government African School, Kabarnet, ambako alifunza hadi 1955 alipojiunga na siasa.
Kujiunga na siasa kwa Moi, kulitokana na mkutano aliofanya na kundi la wapiganaji wa uhuru chini ya uongozi wa Brigedia Daniel Njuguna aliyemtembelea Juni, 1955. Aliunga vita vyao na baada ya kuwalisha na kuwakinga kwa wiki mbili, aliwapa chakula na Sh500.
Mnamo Oktoba 1955, Moi alichaguliwa kutoka orodha ya watu wanane walioteuliwa kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Joseph ole Tameno, ambaye alikuwa amejiuzulu kutoka kiti kisichokuwa rasmi katika Legco. Moi alipoketi Legco akiwa na wanachama wengine wanne pekee Waafrika mnamo Oktoba 18, 1955, hakujua yaliyokuwa yakimsubiri.
Hata hivyo, alikabiliana na changamoto hiyo mpya na mnamo 1956, aliwasilisha mswada kutaka walimu Waafrika, waruhusiwe kuunda chama chao wenyewe. Chama cha Kitaifa cha Muungano wa Walimu Kenya (Knut) kiliundwa na kusajiliwa 1957.
Alishirikiana na viongozi wengine kama vile Eliud Mathu, Ronald Ngala na Masinde Muliro, kutetea Jomo Kenyatta kuachiliwa kutoka kizuizini na idadi ya Waafrika katika Legco kuongezwa.
Mnamo 1959, aliongoza kundi la viongozi wengine kumtembelea Kenyatta kizuizini Lodwar.Mnamo 1960, Moi na wanachama wengine Waafrika katika Legco, walishiriki katika mazungumzo ya kikatiba katika Lancaster House jijini London katika maandalizi ya Uhuru wa Kenya kutoka kwa Uingereza. Waliporudi nchini, walinuia kuanzisha chama kimoja cha kitaifa cha kisiasa.
Lakini tofauti kati yao zilifanya waunde vyama viwili- KANU cha Gichuru, Odinga na Mboya kilichobuniwa Kiambu na KADU cha Ngala (Rais), Moi (mwenyekiti), Muliro (naibu- mwenyekiti) na Martin Shikuku (katibu- mkuu); walichounda wakiwa Ngong.Moi na wengine katika KADU, ambao walitoka jamii ndogo, walikataa KANU wakidai kilikuwa kikiwakilisha maslahi ya jamii kubwa, Waluo na Wakikuyu. Kwa hivyo, waliamua kuunda muungano wa makabila mengi.
Katika uchaguzi wa 1961, KANU ilishinda viti 19 na KADU 11. Lakini KANU ilikataa kuunda serikali hadi Kenyatta aachiliwe huru. Hata hivyo, KADU ilikubali na Moi akateuliwa Katibu wa Bunge (waziri msaidizi wakati huo) katika Wizara ya Elimu mnamo 1961.
Baadaye alihudumu katika wizara za Elimu na Serikali za Wilaya.Katika uchaguzi wa 1963 ambao uliletea Kenya uhuru, KADU ilikataa kuwasilisha wagombeaji kupinga KANU, kilichokuwa wakati huo chini ya uongozi wa Kenyatta baada ya kuachiliwa kutoka kizuizini 1961.
KADU ilishindwa na kuwa katika Upinzani. Kenyatta alichaguliwa Waziri Mkuu.Akiwa mwenyekiti wa KADU, Moi aliona utata wa siasa na akaamua kufuata mfumo wa umoja wa kitaifa. Hii ndiyo ilifanya KADU kuvunjwa Novemba, 1964.
Wanachama walijiunga na KANU na Kenya ikawa taifa la chama kimoja, japo si kisheria.Kenyatta alimteua Moi Waziri wa Mashauri ya Ndani, wadhifa ambao alihifadhi hata alipokuwa Makamu- Rais.
Wizara ya Mashauri ya Ndani ulikuwa wadhifa muhimu kwa sababu waziri alisimamia magereza, polisi na Idara ya Uhamiaji.Toleo la Africa Confidential la Juni, 1990, lilisema hivi kuhusu Moi na Wizara ya Mashauri ya Nyumbani: “Alifanya urafiki ambao ulimfaa miaka ya baadaye.
Jukumu lake la kutoa paspoti lilimkutanisha na wafanyabiashara kutoka bara Asia na kampuni kutoka Uingereza. Lilikuwa jukumu la Moi pia kuteua wakuu wa polisi, magereza na huduma za uhamiaji. Hatua hii ilimfaidi miaka ya baadaye wakati huduma ya polisi ilikuwa imejaaa watu walioteuliwa na Moi.”
TAFSIRI: BENSON MATHEKA