Jamvi La Siasa

Kiini cha masaibu ya Mbarire katika UDA

Na MWANGI MUIRURI June 5th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

Kilichoanza miezi mitano iliyopita kama onyo kali kutoka kwa Naibu Rais Kithure Kindiki kwa Gavana wa Embu, Cecily Mbarire, sasa kimechacha, na kinatishia kuangusha taaluma yake ya kisiasa ya miongo mitatu.

Gavana Mbarire anaonywa kwamba huenda akawa mhanga mwingine wa mkakati wa kisiasa wa “tumika halafu utupwe mbali,” mkakati ambao tayari umewalenga washirika wakuu kadhaa. Hata hivyo, Rais William Ruto naye anaonywa kwamba Mbarire huenda anapanga kujiondoa serikalini, kuashiria uasi unaoweza kulipuka eneo la Mlima Kenya.

Mnamo Januari 30. 2025 Bi Mbarire, ambaye kwa sasa ndiye mwenyekiti wa muda wa chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA), alikosolewa hadharani na Naibu Rais Kindiki, baada ya Rais Ruto kuzomewa alipokuwa Embu, tukio ambalo limerudiwa katika ziara kadhaa za rais katika kaunti hiyo.

“Nilizungumza na dada yangu Cess, Gavana wa Embu na rafiki yangu wa muda mrefu kisiasa. Inawezekanaje kiongozi wa chama, Rais, aje mji wa nyumbani na azomewe? Kama hauwezi kuzuia hayo, una sababu gani ya kubaki katika uongozi wa chama?” aliuliza Kindiki wakati huo.

Badala ya kujibu moja kwa moja, Bi Mbarire alielekea kwa wananchi mashinani kutetea nafasi yake.

Hata hivyo, wakati wa ziara ya Rais Ruto mnamo Aprili huko Embu, kuzomwa kulizidi huku umati ukimtuhumu Rais kwa “uongo wa kupindukia.”

Mzozo huo ulijitokeza waziwazi  Juni 1 2025, wakati Gavana Mbarire katika hotuba yake ya Madaraka Dei huko Makima aliwashutumu maafisa wakuu wa serikali kwa kupanga njama dhidi yake.

“Kuna watu ndani ya serikali hii ninaowatetea kila siku lakini sasa wananifanyia njama kisiasa. Wanakutana usiku kwa siri. Vitisho hivi visipoisha, nitawafichua,” alisema.

Jumanne iliyofuata, alisusia mkutano wa jumbe kutoka Embu ulioandaliwa na Naibu Rais katika makazi yake ya Karen uliolenga masuala ya kiuchumi ya Kaunti ya Embu. Waliokuwepo walikuwa Seneta Alexander Mundigi, Mwakilishi wa Wanawake Njoki Njeru, Wabunge Eric Muchangi (Runyenjes), Nebart Muriuki (Mbeere Kusini), na Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku, ambaye ni mbunge wa zamani wa Mbeere Kaskazini.

Hata hivyo, siku ya Jumatano, gavana alikutana na naibu rais peke yake akiandamana na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kaunti ya Embu, Peter Muriithi.

Prof Kindiki alisema mkutano huo ulikuwa wa mashauriano kuhusu miradi ya serikali ya kitaifa Embu na mikakati ya kulinda sekta muhimu za kilimo kama vile muguka, chai, na macadamia.

“Hakuna tatizo lolote kati yangu na Gavana Mbarire wala kiongozi mwingine yeyote wa Embu. Wanaonifahamu na viongozi wa Embu wanajua tumetembea safari ndefu pamoja,” Prof Kindiki alisema akiwa Embu.

Aliwashutumu baadhi ya wanasiasa kwa kujaribu kuchochea uhasama kati ya serikali ya kitaifa na watu wa Embu.

“Kuna baadhi ya wanasiasa wanatafuta kuchochea matatizo, lakini kwa sasa hakuna tatizo, tunashirikiana na gavana,” alisema Kindiki.

Wachambuzi wa siasa wanasema matamshi ya wazi ya Mbarire ni ishara ya kwamba anashinikizwa kutoka kwa uongozi wa kitaifa na mashinani.

“Kiongozi wa chama tawala anapolalamika hadharani, hiyo ni ishara kwamba kuna matatizo juu—huenda yanatoka kwa Rais mwenyewe,” alisema mchambuzi mmoja.

Mbunge wa Manyatta, Gitonga Mukunji, aliongeza, “Hali Embu inazidi kuwa ngumu kwa yeyote asiye upande wa Gachagua. Mbarire anajibu shinikizo.” Alidai pia kuwa Mbarire ana hofu ya uchaguzi mdogo wa Mbeere Kaskazini ambapo nafasi ya upande wake kushinda ni ndogo.

Wakati huo huo, Mwanasheria Mkuu wa zamani, Justin Muturi, ameibuka kuwa mkosoaji mkubwa wa Rais, akifichua siri za ndani za serikali.

Kumnyamazisha Muturi, Rais Ruto alimteua aliyekuwa mbunge wa Mbeere Kaskazini, Geoffrey Ruku, katika baraza la mawaziri — hatua inayotarajiwa kusababisha uchaguzi mdogo unaoweza kuzidisha migawanyiko katika siasa za Embu.

Katika hotuba yake ya Madaraka Dei, gavana alidokeza kuwa anajua kuhusu minong’ono hiyo. “Kila siku nakumbana na chuki mashinani nikiitetea serikali hii. Uaminifu wangu unastahili kulipwa kwa heshima,” alisema.

Kiongozi wa chama cha The Service Party na mshirika wa karibu wa Rais, Mwangi Kiunjuri, alipuuza madai ya njama dhidi ya Mbarire.

“Mimi huzungumza mara kwa mara na washauri wa ndani wa Rais, na jina lake halijawahi kutajwa kuwa tatizo,” alisema Kiunjuri.

Hata hivyo, Seneta wa Kakamega Boni Khalwale alimshauri gavana kuukubali ukweli wa kisiasa.

“Huenda kichwa chake ndicho kinachofuata kukatwa na Ruto. Nimepitia hapo. Hata Johnstone Muthama pia. Usilie, endelea na maisha,” aliandika kwenye mitandao ya kijamii Juni 2, 2025.

Khalwale alidai Mbarire sasa ni mwathirika wa hali katika UDA. “Ulimrithi Muthama kama mwenyekiti wa UDA, kama vile mimi nilivyong’olewa na Cleophas Malala, ambaye hata hakuwa wa chama chetu. Huu ndio mtindo: tumia na utupe,” alisema.