KINAYA: Itakuwa vigumu kutimua mapepo ya UG yakiwa na hatimiliki!
WAKENYA tuna mchezo sana! Tumempa Mzee Msaba haki ya kusimama pale mpakani, upande wa Uganda, na kukojolea mimea yetu anavyotaka, tukilalamika kidogo atwambie tuzoee utundu wake, tuache kumsumbua kwa kuwa ndiye mwekezaji anayetuweka hai.
Tunawezaje kumwaminia Msaba mafuta yetu? Naambiwa amenunua asilimia kubwa ya hisa za Shirika la Kenya Pipeline (KPC), akapata na mamlaka ya kufanya maamuzi muhimu kuhusu usafirishaji na usambazaji mafuta.
Si hayo tu! Atakuwa na usemi wa mwisho kuhusu ajira ya msimamizi wa shirika hilo.
Hii ina maana kwamba, hata rais wa Kenya akitaka kumteua msimamizi, sharti kwanza awasiliane na Msaba ili apate idhini yake.
Na Msaba akiamua kutuletea bintiye asimamie KPC, kama ilivyo desturi ya dikteta huyo kuwapa wanawe nyama ya mafuta huku Waganda wakibaki kutafuta mifupa mikavu?
Na mwanawe kichaa, Jenerali Muhoozi, akiamua kuongoza majeshi yake kuvuka mpaka na kuingia Kenya, mitungi mikononi, kwa kisingizio kwamba wamekuja kuchota mafuta yao ambayo yanahifadhiwa kwa jirani?
Na Jenerali wa watu akitumia mafuta kama kisingizio cha kuiteka na kuitawala Nairobi ‘katika muda wa saa chache tu’ kama alivyotishia miaka kadha iliyopita?
Na, je, Msaba mwenyewe akiamua kufuata bomba linalosafirisha mafuta kutoka Mombasa hadi Nairobi, adai eti popote linapopita ni ardhi ya Uganda?
Ama unataka kuniambia umesahau kwamba amewahi kueleza hasira alizonazo kuhusu ubadilishanaji wa mamlaka miongoni mwa viongozi wa Kenya, ambao umemkosesha matumaini ya kuifikia Bahari ya Hindi na kuifungulia Uganda dunia nzima?
Hivi ilikuwaje tukafumba macho kiasi cha kutoona kwamba Uganda ikinunua hisa nyingi hivyo tutaanza kumuita Msaba ‘bwana’ na mwanawe ‘bwana mdogo’?
Ikiwa akili zako zinakwambia tunaweza kufunga bomba hilo na kuwatesa tutakavyo, basi jua kuwa ununuzi wa kampuni hiyo unawapa hata na uhuru wa kutushambulia kijeshi iwapo tutahatarisha uhuru wao wa kufikia mafuta wakati wowote.
Ninachomaanisha ni kwamba, hata Kenya ikiamua kufunga bomba la mafuta kutokana na mzozo wowote unaoweza kuzuka kati yetu na Uganda, wanajeshi wa Uganda watakuwa na kila haki ya kisheria kutushambulia kwa kisingizio kwamba wanalinda maslahi yao ya kitaifa.
Mambo huwa hivyo mnapotumia akili kama kofia, na matumbo ya minyoo kama ubongo, wakati wa uuzaji wa mashirika yenye umuhimu wa kitaifa.
Mnunuzi mjanja anaweza kutumia mawakala msiojua, mkatia saini mikataba ya kujiuza utumwani.
Walokole watakwambia hakuna kazi ngumu kama kujaribu kuyafukuza mapepo machafu kutoka eneo walilopewa haki za kuishi.
Msumbufu huwa wewe eti kwa kuwa umeingia ndani ya kumi na nane zao.
Ingawa baadhi yetu wanasema si neno hata nchi hii ikitafunwa kama karanga, imumunywe kama peremende, au inyofolewe kama mnofu wa mbuzi-choma, usalama wake unatuhusu sote.
Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)