Jamvi La Siasa

KINAYA: Jinsi watu huingia boksi Sikukuu ya Valentino, ndivyo wengi hushika mimba za kisiasa

Na DOUGLAS MUTUA February 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HIVI uko tayari kuwajibikia vituko na sarakasi ulizoshiriki jana kisa na maana Siku ya Wapendanao?

Kuna picha maarufu mtandaoni ambapo mvulana anamkimbiza kidosho akimsihi akubali mambo yake Siku ya Wapendanao; chini ya hiyo ipo nyingine, miezi tisa baadaye, ambapo sasa msichana, ujauzito kamfika shingoni, anamkimbiza mvulana!

Labda nikuulize: jana ulipendwa, au ulisimama peke yako kama mlingoti wa bendera, ukawa unarembua macho tu kuajabia wapenzi na miondoko yao?

Kupenda na kupendwa ni raha, lakini kwa wasiopendwa, mapenzi hukaa kama maigizo ya wanafiki wanaotamaniana kwa hisia za sasa, kesho kuna Mungu, kila mmoja ajipange kivyake.

Tuchukulie tu kwamba jana ulipendwa kikweli, hukusisimkia maua, peremende na pombe za watu kisha uanze kujuta siku si nyingi zaijazo. Ulipopendwa ulipendeka?

Ulipata maua kutoka kwa dhati ya moyo wa ‘jambazi’, au yalitumika kama hongo kukushawishi kufanya mambo ambayo bure tu hungeyafikiria wala kuyashiriki.

Nimegundua siku hizi walaji hongo ni wengi huku nje, lakini tuna pupa ya kuilaumu serikali na maafisa wake kwa kitu ambacho tumechukulia kuwa desturi kwetu.

Mathalan, kuna kauli za ajabu kama vile ‘mapenzi ni pesa’, ‘utamu wa penzi ni hela’, ‘ni heri kulilia ndani ya Mercedes Benz kuliko kulilia juu ya bodaboda’.

Aghalabu pendekezo la posa likitoka, unasikia: “Ana hela au tutakula hewa?” Aliyethubutu kuposa akisitasita anaambiwa bila huruma “Katafute hela kwanza, mapenzi yana gharama zake.”

Hata kauli safi ya wahenga kwamba mkono mtupu haulambwi inatumiwa vibaya katika muktadha usiofaa kitu, watu wakijaribu kutusadikisha kuwa tamaa ya pesa, ngono ya malipo na maovu mengineyo, yanafaa.

Mara nyingi unapata masichana anayetoa masharti hayo magumu ya hela ametokea familia maskini kiasi kwamba hata ushirikiano wa baba yake na kaka zake hauwezi kumudu vitu vyote anavyoitisha.

Wavulana, baada ya kuona kwamba bahati imechelewa kusimama, ama wanazika nia ya kuoa katika kaburi la sahau, au wanawekwa rumenya na wanawake wa rika la mama zao. Mwisho wa siku kinazuka kizazi kivivu chenye tabia za paka wa dukani anayejipenda kupita kiasi.

Nao warembo waliosubiri vijana wapate pesa bila mafanikio yoyote wanaanza kuwanyemelea baba zetu, wanaishia kunywa pombe nyingi kuliko gari aina ya Ford linavyokunywa mafuta!

Mwishowe tunajikuta na kizazi kisichooa wala kuolewa, chenye hasira za mkizi. Thubutu kukishauri, utaambiwa ‘ambia serikali ikutafutie kazi’. Unapiga ubwete sana eti.

Hivyo ndivyo mambo yanavyokwenda kwenye ulingo wa siasa pia. Viongozi wazuri wanajitokeza, wanauza sera kwa haiba kubwa, mwishowe mwananchi anawauliza, “Umekuja na nini au ni kelele tu?”

Aliyekuwa kiongozi anageuka mwanasiasa, anatafuta mahela hata ya kuiba, anakuonjesha kama njugu karanga, unamchagua, ukimkumbusha ahadi za wakati wa kampeni anakwambia muamala wa kibiashara kati yako naye ulikamilika, kila mtu ajipange. Una mimba tayari!

Tumia akili; usikubali tamaa ya pesa ikupe mimba ya kisiasa. Hiyo hubebwa miaka mitano, si miezi tisa.

– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)